Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 35

Hana Alisali Apate Mtoto

Hana Alisali Apate Mtoto

Elkana alikuwa mwanaume Mwisraeli aliyekuwa na wake wawili, Hana na Penina, lakini Elkana alimpenda Hana zaidi. Penina alimdhihaki Hana wakati wote kwa sababu yeye alikuwa na watoto wengi na Hana hakuwa na mtoto hata mmoja. Kila mwaka, Elkana pamoja na familia yake walienda kuabudu katika maskani iliyokuwa Shilo. Siku moja, walipokuwa huko, alimwona mke wake mpendwa Hana akiwa amehuzunika sana. Akamwambia hivi: ‘Hana, tafadhali usilie. Mimi nipo. Ninakupenda.’

Baadaye, Hana alienda kusali. Akiwa analia, alisali kwa Yehova na kumwomba msaada. Alitoa ahadi hii: ‘Yehova, ikiwa utanipa mtoto, nitamtoa akutumikie maisha yake yote.’

Kuhani Mkuu Eli alimwona Hana akilia naye akafikiri kwamba Hana alikuwa amelewa. Hana akamjibu: ‘Hapana, Bwana wangu, mimi sijalewa. Nina tatizo zito nami ninamweleza Yehova kulihusu.’ Eli alitambua kwamba alikuwa amekosea, kwa hiyo akamwambia hivi: ‘Mungu na akutimizie ombi lako.’ Hana alihisi vizuri, kisha, akaenda zake. Ndani ya mwaka mmoja, alipata mtoto naye akamwita jina lake Samweli. Hebu wazia jinsi Hana alivyofurahi kupata mtoto!

Hana hakusahau ahadi aliyotoa kwa Yehova. Baada ya Samweli kuacha kunyonya, alimpeleka ili akatumikie katika maskani. Hana alimwambia Eli hivi: ‘Huyu ndiye mtoto ambaye nilisali kumhusu. Ninamtoa amtumikie Yehova maisha yake yote.’ Kila mwaka, Elkana na Hana walimtembelea Samweli na kumletea koti lisilo na mikono. Yehova alimbariki Hana naye akapata wana watatu na mabinti wawili.

“Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.”​—Mathayo 7:7