Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 39

Mfalme wa Kwanza wa Israeli

Mfalme wa Kwanza wa Israeli

Ingawa Yehova alikuwa amewapatia Waisraeli waamuzi, bado walitaka kuwa na mfalme. Walimwambia Samweli hivi: ‘Mataifa yote yanayotuzunguka yana wafalme. Sisi pia tunataka mfalme.’ Samweli hakupendezwa na jambo hilo, hivyo alisali kwa Yehova. Yehova alimjibu hivi: ‘Watu hawa hawajakukataa wewe. Wamenikataa mimi. Waambie kwamba wanaweza kuwa na mfalme, lakini mfalme atadai mambo mengi kutoka kwao.’ Hata hivyo, watu wakamjibu na kusema: ‘Tunataka mfalme!’

Yehova alimwambia Samweli kwamba Sauli atakuwa mfalme wa kwanza wa Waisraeli. Sauli alipoenda kumtembelea Samweli huko Rama, Samweli alimweka rasmi kuwa mfalme kwa kummiminia mafuta kichwani.

Kisha, Samweli aliwaita Waisraeli wote ili wamwone mfalme wao mpya. Hata hivyo, Sauli hakuonekana popote. Unajua ni kwa nini? Kwa sababu alikuwa amejificha kwenye mizigo. Walipompata, walimleta na kumsimamisha katikati ya watu. Sauli alikuwa mrefu kuliko watu wengine wote, na alikuwa mwenye sura nzuri. Samweli akawaambia: ‘Mwoneni yule ambaye Yehova amemchagua.’ Watu wakapiga kelele na kusema: ‘Mfalme na aishi milele!’

Mwanzoni, Mfalme Sauli alimsikiliza Samweli na kumtii Yehova. Hata hivyo, baadaye alibadilika. Kwa mfano, mfalme hakupaswa kutoa dhabihu. Wakati fulani, Samweli alimwambia Sauli amngojee, lakini Samweli akachelewa kufika. Hivyo, Sauli aliamua kutoa dhabihu. Samweli alitendaje? Alimwambia hivi: ‘Ulipaswa kumtii Yehova.’ Je, Sauli alijifunza somo lolote kutokana na kosa lake?

Baadaye, Sauli alipoenda kupigana na Waamaleki, Samweli alimwambia awaangamize wote. Hata hivyo, Sauli hakumuua Mfalme Agagi. Yehova akamwambia Samweli: ‘Sauli ameniacha, naye hanisikilizi.’ Samweli alihuzunika sana na kumwambia Sauli hivi: ‘Kwa kuwa hukumtii, Yehova atamchagua mfalme mwingine.’ Samweli alipogeuka ili kuondoka, Sauli alishika upindo wa koti la Samweli nalo likararuka. Kisha, Samweli akamwambia Sauli: ‘Yehova ameurarua utawala wa kifalme kutoka kwako.’ Yehova angempa ufalme mtu mwingine ambaye atampenda na kumtii.

“Kutii ni bora kuliko dhabihu.”​—1 Samweli 15:22