Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 42

Yonathani Alikuwa Jasiri na Mshikamanifu

Yonathani Alikuwa Jasiri na Mshikamanifu

Yonathani, mwana wa kwanza wa Sauli, alikuwa shujaa wa vita mwenye uhodari. Daudi alisema kwamba Yonathani alikimbia mbio kuliko tai na alikuwa na nguvu kuliko simba. Siku moja, Yonathani aliona askari-jeshi Wafilisti 20 wakiwa juu ya mlima. Akamwambia mchukua-silaha wake hivi: ‘Tutawashambulia ikiwa tu Yehova atatupa ishara. Wafilisti wakituambia twende mahali walipo, hiyo itakuwa ishara kwamba tunapaswa kuwashambulia.’ Wafilisti wakapaaza sauti: ‘Njooni tupigane!’ Kwa hiyo, wanaume hao wawili wakapanda huo mlima na kuwashinda askari-jeshi hao.

Kwa kuwa Yonathani alikuwa mwana mwenye umri mkubwa wa Sauli, yeye ndiye aliyepaswa kuwa mfalme baada ya baba yake. Lakini Yonathani alijua kwamba Yehova alikuwa amemchagua Daudi kuwa mfalme wa Israeli anayefuata. Yonathani hakumwonea Daudi wivu. Yonathani na Daudi wakawa marafiki wazuri. Waliahidi kulindana na kuteteana. Yonathani akampa Daudi koti, upanga, upinde, na mshipi wake kama ishara ya urafiki wao.

Daudi alipokuwa akimkimbia Sauli, Yonathani alimwendea na kumwambia hivi: ‘Usiogope, uwe jasiri. Yehova amekuchagua kuwa mfalme. Hata baba yangu anajua jambo hilo.’ Je, ungependa kuwa na rafiki mzuri kama Yonathani?

Zaidi ya mara moja, Yonathani alihatarisha maisha yake ili kumsaidia rafiki yake. Alijua kwamba Mfalme Sauli alitaka kumuua Daudi, kwa hiyo akamwambia baba yake hivi: ‘Ukimuua Daudi utakuwa ukifanya dhambi; hajafanya kosa lolote.’ Sauli alimkasirikia Yonathani. Miaka michache baadaye, Sauli na Yonathani wakafa vitani.

Baada ya Yonathani kufa, Daudi alimtafuta Mefiboshethi, mwana wa Yonathani. Daudi alipompata Mefiboshethi, alimwambia hivi: ‘Kwa sababu baba yako alikuwa rafiki yangu wa karibu, nitakutunza maisha yako yote. Utaishi katika nyumba yangu ya kifalme na utakula mezani pangu.’ Daudi hakumsahau kamwe rafiki yake Yonathani.

“Mpendane kama vile nilivyowapenda. Hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.”​—Yohana 15:12, 13