Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 45

Ufalme Wagawanyika

Ufalme Wagawanyika

Sikuzote ambazo Sulemani alimwabudu Yehova, kulikuwa na amani katika Israeli. Lakini Sulemani akaoa wanawake wengi kutoka katika nchi nyingine, na wake hao waliabudu sanamu. Hatua kwa hatua, Sulemani alibadilika, naye pia akaanza kuabudu sanamu. Yehova alikasirika. Akamwambia Sulemani hivi: ‘Israeli litararuliwa vipande viwili kutoka kwa familia yako. Nitampa mmoja wa watumishi wako kipande kikubwa, na familia yako itatawala kipande kidogo.’

Yehova alitumia njia nyingine kuonyesha wazi uamuzi wake. Yeroboamu, mtumishi mmoja wa Sulemani alikuwa akisafiri barabarani alipokutana na nabii Ahiya. Ahiya akararua vazi lake vipande 12 na kumwambia Yeroboamu: ‘Yehova atachukua ufalme wa Israeli kutoka kwa familia ya Sulemani na kuugawanya vipande viwili. Chukua vipande kumi kati ya hivi kwa kuwa utatawala juu ya makabila kumi.’ Mfalme Sulemani alisikia kuhusu jambo hilo na akataka kumuua Yeroboamu! Kwa hiyo, Yeroboamu akakimbia na kwenda Misri. Baada ya muda, Sulemani akafa na mwana wake Rehoboamu akawa mfalme. Hivyo, Yeroboamu akahisi kwamba ilikuwa salama kwake kurudi Israeli.

Wazee wa Israeli wakamwambia Rehoboamu hivi: ‘Ikiwa utawatendea watu vizuri, watakuwa washikamanifu kwako.’ Lakini rafiki za Rehoboamu waliokuwa vijana wakamwambia: ‘Unapaswa kuwa mkali kwa watu hao! Fanya kazi yao iwe ngumu zaidi!’ Rehoboamu akafuata ushauri wa vijana wenzake. Akawa mkatili kwa watu nao wakaasi. Wakamfanya Yeroboamu kuwa mfalme wa makabila kumi, ambayo yakaja kujulikana kama ufalme wa Israeli. Makabila yale mengine mawili yaliitwa ufalme wa Yuda. Watu wa makabila hayo wakaendelea kuwa washikamanifu kwa Rehoboamu. Sasa yale makabila 12 ya Israeli yalikuwa yamegawanyika.

Yeroboamu hakutaka watu wake waende kuabudu Yerusalemu, jiji ambalo lilikuwa katika ufalme wa Rehoboamu. Unajua sababu? Yeroboamu aliogopa kwamba wangemwasi na kumuunga mkono Rehoboamu. Kwa hiyo, akatengeneza ndama wawili wa dhahabu na kuwaambia watu wake: ‘Yerusalemu liko mbali sana. Mnaweza kuabudu hapa.’ Watu wakaanza kuabudu ndama hao wa dhahabu na wakamsahau Yehova tena.

“Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya uadilifu na uasi-sheria? . . . Au mwamini ana ushirika gani na mtu asiye mwamini?”​—2 Wakorintho 6:14, 15