Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

45

Ufalme Unagawanyika

Ufalme Unagawanyika

Wakati wote wenye Sulemani alikuwa anamuabudu Yehova, amani ilikuwa mu Israeli. Lakini Sulemani alioa wanamuke wengi wa inchi zingine, na wale wanamuke walikuwa wanaabudu sanamu. Sulemani alianza kubadilika polepole, naye pia akaanza kuabudu sanamu. Yehova alikasirika. Aliambia Sulemani: ‘Nitanyanganya familia yako taifa la Israeli na litagawanywa mu sehemu mbili. Nitapatia mumoja wa watumishi wako sehemu kubwa, na familia yako itatawala sehemu ya kidogo.’

Yehova alitumia pia njia ingine juu ya kuonyesha waziwazi uamuzi wake. Siku moja Yeroboamu, mutumishi moja wa Sulemani, alikuwa mu safari. Akakutana na nabii Ahiya. Ahiya akapasua nguo yake mu vipande 12 na kuambia Yeroboamu: ‘Yehova atatosha ufalme wa Israeli mu familia ya Sulemani na kuugawanya mu sehemu mbili. Kamata vipande kumi juu utatawala makabila kumi.’ Wakati Mufalme Sulemani alisikia vile, alitaka kuua Yeroboamu! Mara moja, Yeroboamu alikimbilia Misri. Kisha wakati fulani, Sulemani alikufa na mutoto wake Rehoboamu akakuwa mufalme. Kwa hiyo, Yeroboamu akaona kama hakuna tena hatari na kama anaweza sasa kurudia mu inchi ya Israeli.

Wazee wa Israeli waliambia Rehoboamu hivi: ‘Kama unafanyia watu mambo ya muzuri, watakuwa washikamanifu kwako.’ Lakini marafiki wa Rehoboamu, wenye walikuwa vijana sawa yeye walimuambia: ‘Usibembeleze watu! Uwalazimishe kufanya kazi ya nguvu sana!’ Rehoboamu akafuata mashauri ya vijana wenzake. Akatendea watu kwa ukali sana na watu wakaasi. Wakafanya Yeroboamu akuwe mufalme wa makabila kumi, yenye iliitwa sasa ufalme wa Israeli. Makabila ingine mbili iliitwa ufalme wa Yuda. Watu wa makabila mbili waliendelea kuwa washikamanifu kwa Rehoboamu. Ni vile makabila 12 ya Israeli iligawanyika.

Yeroboamu hakupenda watu wake waende kuabudu kule Yerusalemu kwenye kulikuwa ufalme wa Rehoboamu. Unajua ni juu ya nini? Yeroboamu aliogopa kama watu watamugeukia na kuunga mukono Rehoboamu. Kwa hiyo, alitengeneza vitoto-dume mbili vya ngombe vya zahabu na kuambia watu wake: ‘Yerusalemu iko mbali sana. Munaweza kuabudu hapa.’ Basi, watu walianza kuabudu vile vitoto-dume vya ngombe vya zahabu na walimusahau Yehova tena.

“Musifungwe nira yenye haiko sawa pamoja na watu wenye hawako waamini. Kwa maana kuko uhusiano gani kati ya haki na uvunjaji wa sheria? . . . Ao muamini iko na ushirika gani na mutu mwenye haiko muamini?”—2 Wakorinto 6:14, 15