Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 46

Jaribu Kwenye Mlima Karmeli

Jaribu Kwenye Mlima Karmeli

Kulikuwa na wafalme wengi wabaya katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi, lakini Ahabu alikuwa mmoja kati ya wale wabaya zaidi. Alimwoa mwanamke mwovu ambaye aliabudu Baali. Jina lake lilikuwa Yezebeli. Ahabu na Yezebeli walijaza ibada ya Baali katika nchi yote na wakawaua manabii wa Yehova. Yehova alifanya nini? Alimtuma nabii Eliya ampe Ahabu ujumbe.

Eliya akamwambia Mfalme Ahabu kwamba kwa sababu ya ubaya wake, hakungekuwa na mvua katika Israeli. Kwa zaidi ya miaka mitatu, hakuna mimea iliyokua na watu walikuwa na njaa kali. Baadaye, Yehova akamtuma Eliya arudi kwa Ahabu. Mfalme akamwambia: ‘Wewe umetuletea taabu! Tunateseka kwa sababu yako.’ Eliya akamjibu: ‘Mimi sikuleta ukame huu. Wewe ndiye uliyeuleta kwa kuabudu Baali. Tutafanya jaribu. Kusanya taifa lote na manabii wa Baali juu ya Mlima Karmeli.’

Watu wakakusanyika kwenye mlima huo. Eliya akasema: ‘Fanyeni uamuzi. Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni. Ikiwa Baali ndiye Mungu wa kweli, basi mfuateni. Acheni tufanye jaribu hili. Manabii 450 wa Baali na watayarishe toleo na kumwitia Mungu wao, na mimi nitatayarisha toleo na kumwitia Yehova. Yule atakayejibu kwa moto ndiye Mungu wa kweli.’ Watu wakakubali.

Manabii wa Baali wakatayarisha toleo lao. Siku nzima walimwitia mungu wao: ‘Ee Baali, tupe jibu!’ Baali alipokosa kuwajibu, Eliya akamdhihaki. Akasema hivi: ‘Iteni kwa sauti kubwa zaidi. Labda amelala, na anahitaji mtu amwamshe.’ Manabii wa Baali waliendelea kuita hadi jioni. Lakini Baali hakuwajibu.

Eliya akaweka toleo lake juu ya madhabahu na kulimwagia maji. Kisha akasali: ‘Ee Yehova, tafadhali unijibu ili watu hawa wajue kwamba wewe ndiye Mungu wa kweli.’ Mara moja Yehova akashusha moto kutoka mbinguni na kuteketeza toleo hilo. Watu wakasema kwa sauti: ‘Yehova ndiye Mungu wa kweli!’ Eliya akasema: ‘Msiache manabii wa Baali waponyoke!’ Siku hiyo, manabii 450 wa Baali wakauawa.

Wingu dogo lilipoonekana juu ya bahari, Eliya akamwambia Ahabu: ‘Kuna dhoruba inayokuja. Funga gari, uende nyumbani.’ Mawingu mazito yakatanda angani, kukawa giza, pepo zikavuma, na mvua kubwa ikaanza kunyesha. Mwishowe, ukame ukaisha. Ahabu akaendesha gari lake kwa kasi kadiri alivyoweza. Lakini kwa msaada wa Yehova, Eliya akakimbia mbio kuliko gari hilo lililokokotwa na farasi! Lakini je, shida zote za Eliya zilikuwa zimekwisha? Acheni tuone.

“Na watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”​—Zaburi 83:18