Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 47

Yehova Amwimarisha Eliya

Yehova Amwimarisha Eliya

Yezebeli aliposikia kilichowapata manabii wa Baali, alikasirika sana. Akamtumia Eliya ujumbe unaosema hivi: ‘Kesho, utakuwa umekufa kama tu hao manabii wa Baali.’ Eliya akaogopa sana na kukimbilia jangwani. Akasali: ‘Yehova, siwezi kuvumilia zaidi. Acha nife.’ Eliya akalala usingizi chini ya mti kwa kuwa alikuwa amechoka.

Malaika akamwamsha Eliya na kumwambia hivi kwa sauti tulivu: ‘Amka ule.’ Eliya akaona mkate wa mviringo uliokuwa juu ya mawe yenye moto na gudulia la maji. Akala na kunywa kisha akalala tena. Malaika akamwamsha tena baadaye na kusema: ‘Kula. Unahitaji nguvu kwa ajili ya safari.’ Kwa hiyo, Eliya akala tena. Kisha akasafiri kwa siku 40 mchana na usiku, hadi alipofika kwenye Mlima Horebu. Eliya akaingia ndani ya pango ili alale. Lakini Yehova akazungumza naye. Akamwambia: ‘Unafanya nini hapa, Eliya?’ Eliya akamjibu: ‘Waisraeli wamevunja agano lako. Wamebomoa madhabahu zako na kuua manabii wako. Sasa wanajaribu kuniua mimi pia.’

Yehova akamwambia: ‘Nenda usimame kwenye mlima.’ Kwanza, upepo wenye nguvu ukapita kwenye pango hilo. Kisha, kukawa na tetemeko halafu moto. Mwishowe, Eliya akasikia sauti tulivu, ya chini. Akafunika uso wake kwa koti lake na akasimama nje ya pango hilo. Kisha Yehova akamuuliza kwa nini alikuwa akikimbia. Eliya akasema: ‘Nimebaki peke yangu.’ Lakini Yehova akamwambia: ‘Hujabaki peke yako. Kuna watu wengine 7,000 katika Israeli ambao bado wananiabudu. Nenda umweke rasmi Elisha awe nabii badala yako.’ Mara moja, Eliya akaenda na kufanya kama Yehova alivyomwambia afanye. Je, unafikiri Yehova atakusaidia unapofanya kile ambacho yeye anataka ufanye? Ndiyo. Acheni tujifunze jambo lingine lililotendeka wakati wa ukame.

“Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu.”​—Wafilipi 4:6