Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 48

Mwana wa Mjane Afanywa Kuwa Hai Tena

Mwana wa Mjane Afanywa Kuwa Hai Tena

Wakati wa ukame, Yehova alimwambia Eliya hivi: ‘Nenda Sarefathi. Mjane fulani huko atakupa chakula.’ Akiwa kwenye malango ya jiji, Eliya alikutana na mjane maskini akikusanya kuni. Akamwomba kikombe cha maji. Alipokuwa akienda kuyaleta, Eliya akamwita na kumwambia: ‘Tafadhali niletee kipande cha mkate.’ Lakini mjane huyo akamwambia: ‘Sina mkate wowote wa kukupa. Nina unga na mafuta yanayotosha kutayarisha chakula kidogo tu kwa ajili yangu na mwanangu.’ Eliya akamwambia: ‘Yehova ameahidi kwamba ukinitayarishia mkate, unga wako na mafuta yako hayatakwisha hadi mvua zitakaporudi.’

Kwa hiyo, yule mjane akarudi nyumbani na kutayarisha mkate kwa ajili ya nabii wa Yehova. Kama tu Yehova alivyoahidi, yule mjane na mwana wake walikuwa na chakula kipindi chote cha ukame. Mitungi yake ya unga na mafuta haikupungua.

Kisha jambo fulani baya likatendeka. Mvulana wa yule mjane akawa mgonjwa sana hivi kwamba akafa. Yule mjane akamsihi Eliya amsaidie. Eliya akamchukua yule mvulana na kumbeba hadi kwenye chumba cha darini. Akamlaza juu ya kitanda na kusali: ‘Yehova, tafadhali mfanye mvulana huyu awe hai tena.’ Ikiwa Yehova angefanya hivyo, je, unajua kwa nini hilo lingekuwa jambo la ajabu? Kwa sababu kwa kadiri tujuavyo, kabla ya hapo hakuna mtu aliyewahi kurudishwa kuwa hai. Na huyo mjane na mwana wake hawakuwa Waisraeli.

Lakini mvulana huyo akawa hai tena naye akaanza kupumua! Eliya akamwambia mjane huyo: ‘Ona! Mwana wako yuko hai.’ Akashangilia sana na kumwambia Eliya hivi: ‘Kwa kweli wewe ni mtu wa Mungu. Ninajua hilo kwa sababu unasema tu kile ambacho Yehova anakuambia useme.’

“Waangalieni kunguru: Hawapandi mbegu wala hawavuni; hawana bohari wala ghala; lakini Mungu huwalisha. Je, ninyi si wenye thamani kuliko ndege?”​—Luka 12:24