Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 50

Yehova Amlinda Yehoshafati

Yehova Amlinda Yehoshafati

Yehoshafati, mfalme wa Yuda, alibomoa madhabahu na sanamu za Baali katika nchi yote. Alitaka watu wajue sheria za Yehova. Kwa hiyo, akawatuma wakuu na Walawi katika nchi yote ya Yuda ili wawafundishe watu sheria za Yehova.

Mataifa yaliyokuwa karibu yaliogopa kushambulia Yuda kwa kuwa yalijua Yehova yuko pamoja na watu wake. Hata walimletea Mfalme Yehoshafati zawadi. Lakini Wamoabu, Waamoni, na wale walioishi kwenye eneo la Seiri wakaja kushambulia Yuda. Yehoshafati alijua kwamba anahitaji msaada wa Yehova. Akawakutanisha wanaume, wanawake, na watoto wote Yerusalemu. Akiwa mbele yao, Yehoshafati akasali hivi: ‘Yehova, bila wewe, hatuwezi kushinda. Tafadhali tuambie tufanye nini.’

Yehova akajibu sala hiyo akisema: ‘Msiogope. Nitawasaidia. Simameni mahali penu, simameni tuli, nanyi mtaona jinsi nitakavyowaokoa.’ Yehova aliwaokoaje?

Siku iliyofuata, Yehoshafati akachagua waimbaji na kuwaambia waende mbele ya jeshi. Walitembea kutoka Yerusalemu hadi kwenye uwanja wa vita katika eneo linaloitwa Tekoa.

Waimbaji walipokuwa wakimsifu Yehova kwa sauti kubwa za shangwe, Yehova aliwapigania watu wake. Aliwafanya Waamoni na Wamoabu wachanganyikiwe sana hivi kwamba wakaanza kupigana wenyewe kwa wenyewe, na hakuna hata mmoja wao aliyeokoka. Lakini Yehova akawalinda watu wa Yuda, askari-jeshi, na makuhani. Watu wote katika nchi zilizowazunguka walisikia kuhusu jambo ambalo Yehova alikuwa amefanya, nao wakajua kwamba bado Yehova anawalinda watu wake. Yehova anawaokoaje watu wake? Kwa njia nyingi. Hahitaji msaada wa wanadamu kufanya hivyo.

“Hamtahitaji kupigana vita hivi. Simameni mahali penu, simameni tuli, muuone wokovu wa Yehova kwa ajili yenu.”​—2 Mambo ya Nyakati 20:17