Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 56

Yosia Aliipenda Sheria ya Mungu

Yosia Aliipenda Sheria ya Mungu

Yosia alianza kutawala akiwa mfalme wa Yuda alipokuwa na umri wa miaka minane. Katika siku hizo, watu walikuwa wakifanya uchawi na kuabudu sanamu. Yosia alipokuwa na umri wa miaka 16, alianza kujifunza jinsi ya kumwabudu Yehova kwa njia inayofaa. Alipokuwa na umri wa miaka 20, alianza kuharibu sanamu na madhabahu katika nchi yote. Kisha Yosia alipokuwa na umri wa miaka 26, aliagiza hekalu la Yehova lirekebishwe.

Kuhani mkuu, Hilkia, alipata kitabu cha kukunjwa cha Sheria ya Yehova katika hekalu. Huenda hicho ndicho kitabu kilekile cha kukunjwa kilichoandikwa na Musa. Shafani, mwandishi wa mfalme alimpelekea Yosia kitabu hicho cha kukunjwa na kuanza kusoma Sheria kwa sauti kubwa. Yosia alipokuwa akisikiliza, alitambua kwamba watu walikuwa wamemwasi Yehova kwa miaka mingi. Mfalme Yosia akamwambia Hilkia hivi: ‘Yehova ametukasirikia sana. Nenda uzungumze naye. Yehova atatuambia tunachopaswa kufanya.’ Yehova akajibu kupitia Hulda nabii wa kike na kusema hivi: ‘Watu wa Yuda wameniacha. Wataadhibiwa lakini si wakati wa utawala wa Yosia, kwa sababu yeye amejinyenyekeza.’

Mfalme Yosia aliposikia ujumbe huo, akaenda hekaluni na kuwakusanya watu wa Yuda. Kisha akasoma Sheria ya Yehova kwa sauti kubwa mbele ya taifa lote. Yosia na watu wote wakaahidi kumtii Yehova kwa moyo wao wote.

Taifa la Yuda halikuwa limesherehekea Pasaka kwa miaka mingi. Lakini Yosia aliposoma katika Sheria kwamba Pasaka inapaswa kusherehekewa kila mwaka, akaliambia taifa lote hivi: ‘Tutafanya Pasaka kwa Yehova.’ Kisha Yosia akatayarisha dhabihu nyingi na akapanga kuwe na waimbaji hekaluni. Taifa lote likafanya Pasaka, halafu wakafanya Sherehe ya Keki Zisizotiwa Chachu, ambayo iliendelea kwa siku saba. Pasaka kama hiyo haikuwa imefanywa tangu  siku za Samweli. Yosia aliipenda sana Sheria ya Mungu. Je, wewe unafurahia kujifunza kumhusu Yehova?

“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru ya njia yangu.”​—Zaburi 119:105