Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 57

Yehova Amtuma Yeremia Akahubiri

Yehova Amtuma Yeremia Akahubiri

Yehova alimchagua Yeremia awe nabii wa watu wa Yuda. Alimwambia awahubirie watu hao na kuwaonya waache kufanya mambo mabaya. Yeremia alisema hivi: ‘Lakini Yehova, mimi ni mvulana tu. Sijui jinsi ya kuzungumza na watu.’ Yehova akamwambia hivi: ‘Usiogope. Nitakuambia kile utakachosema. Nitakusaidia.’

Yehova akamwambia Yeremia akusanye wanaume wazee, avunje chupa ya udongo mbele yao, na kusema: ‘Yerusalemu litavunjwa jinsi hii.’ Yeremia alipofanya kama Yehova alivyomwagiza, wazee hao wakakasirika sana. Kuhani anayeitwa Pashuri akampiga Yeremia na kumweka katika mikatale. Yeremia hangeweza kusonga usiku kucha. Pashuri alipomwachilia asubuhi iliyofuata, Yeremia alisema hivi: ‘Siwezi kuvumilia tena. Nitaacha kuhubiri.’ Lakini, je, aliacha kuhubiri? Hapana. Yeremia alipotafakari kuhusu jambo hilo, alisema hivi: ‘Ujumbe wa Yehova ulikuwa kama moto unaowaka ambao umefungiwa ndani yangu. Siwezi kuacha kuhubiri.’ Yeremia aliendelea kuwaonya watu hao.

Miaka kadhaa ilipita, na kukawa na mfalme mwingine  nchini Yuda. Makuhani na manabii wa uwongo walichukia ujumbe wa Yeremia. Waliwaambia wakuu hivi: ‘Mtu huyu anastahili kufa.’ Yeremia akasema hivi: ‘Mkiniua, mtamwua mtu asiye na hatia. Maneno ninayosema si yangu, ni ya Yehova.’ Wakuu waliposikia maneno hayo, wakasema hivi: ‘Mtu huyu hastahili kufa.’

Yeremia aliendelea kuhubiri, na wakuu wakakasirika sana. Wakamwambia mfalme amwue. Mfalme Sedekia akawaambia kwamba wanaweza kumfanyia Yeremia chochote walichotaka. Wakamchukua na kumtupa ndani ya kisima kirefu chenye matope, wakitumaini kwamba angefia humo. Yeremia akaanza kuzama ndani ya matope.

Kisha ofisa mmoja wa makao ya mfalme aliyeitwa Ebedmeleki akamwambia mfalme hivi: ‘Wakuu wamemtupa Yeremia ndani ya kisima! Tukimwacha humo, atakufa.’ Sedekia akamwamuru Ebedmeleki achukue wanaume 30 na kumtoa Yeremia katika kisima hicho. Je, hatupaswi kumwiga Yeremia ambaye hakuruhusu kitu chochote kimzuie kuhubiri?

“Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu, lakini atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—Mathayo 10:22