Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 58

Yerusalemu Laharibiwa

Yerusalemu Laharibiwa

Tena na tena, watu wa Yuda walimwacha Yehova na kuabudu miungu ya uwongo. Yehova alijaribu kuwasaidia kwa miaka mingi. Aliwatuma manabii wengi ili kuwaonya lakini hawakusikiliza. Badala yake, waliwadhihaki. Yehova alikomeshaje ibada yao ya sanamu?

Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, alikuwa akishinda taifa moja baada ya lingine. Mara ya kwanza aliposhinda Yerusalemu, alimteka Mfalme Yehoyakini, wakuu, mashujaa, na mafundi, na kuwapeleka Babiloni. Pia, alichukua hazina zote zilizokuwa kwenye hekalu la Yehova. Kisha, Nebukadneza akamfanya Sedekia kuwa mfalme wa Yuda.

Mwanzoni, Sedekia alimtii Nebukadneza. Hata hivyo, mataifa jirani na manabii wa uwongo walimshauri Sedekia aasi utawala wa Babiloni. Lakini Yeremia alimwonya hivi: ‘Ukiasi, kutakuwa na mauaji, njaa, na magonjwa katika Yuda.’

Baada ya kutawala kwa miaka minane, Sedekia aliamua kuuasi utawala wa Babiloni. Akaomba jeshi la Misri limsaidie. Kisha Nebukadneza akatuma jeshi lake lishambulie Yerusalemu, nalo likapiga kambi kulizunguka jiji. Yeremia akamwambia Sedekia: ‘Yehova amesema, mkimtumikia mfalme wa Babiloni, ninyi pamoja na jiji lenu mtaendelea kuishi. Msipofanya hivyo, Wababiloni watateketeza Yerusalemu kwa moto na kukuchukua ukiwa mfungwa.’ Sedekia akasema: ‘Sitamtumikia!’

Mwaka mmoja na nusu baadaye, jeshi la Babiloni lilivunja kuta za Yerusalemu na kuliteketeza jiji hilo. Waliteketeza hekalu, wakaua watu wengi, na kuwachukua maelfu ya watu wakiwa wafungwa.

Sedekia alitoroka Yerusalemu, lakini Wababiloni walimfuatilia. Wakamkamata karibu na jiji la Yeriko na kumleta kwa Nebukadneza. Mfalme wa Babiloni alimlazimisha Sedekia ashuhudie watoto wake mwenyewe wakiuawa. Halafu akampofusha Sedekia na kumfunga gerezani, ambako alikufa baadaye. Lakini Yehova aliwaahidi hivi watu wa Yuda: ‘Baada ya miaka 70, nitawarudisha nyumbani Yerusalemu.’

Vijana waliopelekwa wakiwa wafungwa Babiloni wangepatwa na nini? Je, wangeendelea kuwa washikaminifu kwa Yehova?

“Yehova Mungu, Mweza-Yote, hukumu zako ni za kweli na za uadilifu.”​—Ufunuo 16:7