Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 61

Hawakuinamia Sanamu

Hawakuinamia Sanamu

Muda fulani baada ya kuota ndoto kuhusu sanamu hiyo, Mfalme Nebukadneza alitengeneza sanamu kubwa ya dhahabu. Akaisimamisha katika nchi tambarare ya Dura na kuwaita watu wenye mamlaka zaidi nchini, kutia ndani Shadraki, Meshaki, na Abednego, wakusanyike mbele ya sanamu hiyo. Mfalme akaamuru hivi: ‘Mara tu mtakaposikia sauti ya tarumbeta, vinubi, na zumari, mwiname chini na kuiinamia sanamu! Yeyote ambaye hataiinamia na kuiabudu atatupwa ndani ya tanuru inayowaka moto.’ Je, Waebrania hao watatu wangeiinamia sanamu hiyo, au wangemwabudu Yehova pekee?

Kisha mfalme akaagiza muziki upigwe. Kila mtu akaanguka na kuiabudu sanamu, isipokuwa Shadraki, Meshaki, na Abednego. Baadhi ya watu wakaona jambo hilo na kumwambia hivi mfalme: ‘Wale Waebrania watatu wamekataa kuiabudu sanamu yako.’ Nebukadneza akawatuma watu wawaite na kuwaambia hivi: ‘Nitawapa nafasi nyingine ili mwabudu sanamu niliyoisimamisha. Ikiwa hamtaiabudu, nitawatupa ndani ya tanuru ya moto. Hakuna mungu anayeweza kuwaokoa kutoka mikononi mwangu.’ Wakamjibu hivi: ‘Hatuhitaji nafasi nyingine. Mungu wetu anaweza kutuokoa. Lakini hata asipotuokoa, Ee mfalme, hatutaibudu sanamu yako.’

Nebukadneza akakasirika sana. Akawaambia wanaume wake hivi: ‘Ongezeni moto ndani ya tanuru uwe mara saba zaidi ya kawaida!’ Kisha akawaamuru maofisa wake hivi: ‘Wafungeni wanaume hawa, na mwatupe ndani ya tanuru!’ Tanuru ilikuwa moto sana hivi kwamba maofisa hao walipokaribia, walikufa papo hapo. Wale Waebrania watatu wakaanguka ndani ya moto. Lakini Nebukadneza alipotazama ndani ya tanuru, aliona kwamba kulikuwa na wanaume wanne wakitembea ndani ya tanuru badala ya wanaume watatu. Naye akaogopa na kuwauliza maofisa wake hivi: ‘Je, hatukuwatupa wanaume watatu ndani ya moto? Ninaona wanaume wanne, na mmoja wao anafanana na malaika!’

Nebukadneza akakaribia mlango wa tanuru na kupaaza sauti hivi: ‘Tokeni nje, enyi watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi!’ Kila mtu alishangaa kuona Shadraki, Meshaki, na Abednego wakitoka ndani ya moto bila madhara yoyote. Ngozi, nywele, na mavazi yao hayakuwa yameungua, wala hawakuwa na harufu ya moto.

Nebukadneza akasema hivi: ‘Mungu wa Shadraki, Meshaki, na Abednego ni mkuu. Alimtuma malaika ili kuwaokoa. Hakuna mungu kama yeye.’

Kama wale Waebrania watatu, je, umeazimia kuwa mshikamanifu kwa Yehova hata nini kikupate?

“Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”​—Mathayo 4:10