Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 63

Mwandiko Ukutani

Mwandiko Ukutani

Baada ya muda, Belshaza akawa mfalme wa Babiloni. Usiku mmoja, mfalme aliwaalika kwenye karamu watu elfu moja wenye mamlaka zaidi nchini. Akawaagiza watumishi wake walete vikombe vya dhahabu ambavyo Nebukadneza alikuwa amechukua kutoka hekalu la Yehova. Belshaza na wageni wake wakatumia vikombe hivyo kunywa na wakatukuza miungu yao. Ghafula, mkono wa mtu ukatokea hewani na kuanza kuandika maandishi ya ajabu kwenye ukuta wa jumba la kulia chakula.

Belshaza akaogopa sana. Akawaita wafanya mazingaombwe na kuwaahidi hivi: ‘Mtu yeyote atakayeeleza maana ya maneno haya, nitamfanya kuwa wa tatu katika mamlaka nchini Babiloni.’ Wakajaribu mmoja baada ya mwingine, lakini hakuna aliyeweza kueleza maana ya maneno hayo. Kisha malkia akaja na kusema hivi: ‘Kuna mtu anayeitwa Danieli, naye alikuwa akimweleza Nebukadneza maana ya mambo magumu. Anaweza kukueleza maana ya maneno haya.’

Danieli akaja mbele ya mfalme. Belshaza akamwambia hivi: ‘Ukiweza kusoma maandishi haya, nitakupa mkufu wa dhahabu na nitakufanya uwe wa tatu katika mamlaka nchini Babiloni.’ Hata hivyo, Danieli akasema hivi: ‘Sitaki zawadi zako, lakini nitakwambia maana ya maneno hayo. Baba yako, Nebukadneza, alikuwa mwenye kiburi, na Yehova akamnyenyekeza. Unajua kila kitu kilichompata, lakini umemvunjia Yehova heshima kwa kunywa divai ukitumia vikombe vya hekalu Lake. Kwa hiyo Mungu ameandika maneno haya: Mene, Mene, Tekeli, na Parsini. Maneno hayo yanamaanisha kwamba Wamedi na Waajemi watashinda Babiloni, nawe hutaendelea kuwa mfalme.’

Ilionekana kana kwamba hakuna anayeweza kushinda Babiloni. Jiji hilo lilikuwa limezingirwa na ukuta mrefu na mto wenye kina kirefu. Lakini usiku huohuo, Wamedi na Waajemi wakashambulia. Koreshi, mfalme wa Uajemi, aligeuza mkondo wa mto hivi kwamba majeshi yake yakavuka na kufika kwenye malango ya jiji. Walipofika, waliyakuta yakiwa wazi! Majeshi yakaingia ndani, yakaliteka jiji, na kumwua mfalme. Kisha Koreshi akawa mfalme wa Babiloni.

Kabla ya mwaka mmoja kuisha, Koreshi akatangaza hivi: ‘Yehova ameniagiza nijenge upya hekalu lake la Yerusalemu. Mtu yeyote ambaye angependa kusaidia ujenzi huo, yuko huru kwenda.’ Kwa hiyo, kama Yehova alivyokuwa ametabiri, Wayahudi wengi walirudi nyumbani miaka 70 baada ya Yerusalemu kuharibiwa. Koreshi akarudisha vikombe vya dhahabu na fedha na vyombo ambavyo Nebukadneza alikuwa amevichukua kutoka hekaluni. Je, unaona jinsi Yehova alivyomtumia Koreshi kuwasaidia watu Wake?

“Ameanguka! Babiloni Mkubwa ameanguka, naye amekuwa makao ya roho waovu.”​—Ufunuo 18:2