Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 64

Danieli Ndani ya Shimo la Simba

Danieli Ndani ya Shimo la Simba

Mfalme mwingine wa Babiloni alikuwa Dario Mmedi. Dario alitambua kwamba Danieli alikuwa mwanamume wa pekee. Akampa Danieli mamlaka juu ya wanaume wengine wote wenye mamlaka nchini. Wanaume hao walimwonea wivu Danieli nao wakataka kumwua. Walijua kwamba Danieli alisali kwa Yehova mara tatu kila siku, hivyo wakamwambia Dario hivi: ‘Ee mfalme, kunapaswa kuwa na sheria kwamba kila mtu asali kwako pekee. Yeyote atakayekosa kutii sheria hiyo atatupwa ndani ya shimo lenye simba wengi.’ Dario alifurahishwa na wazo hilo, hivyo akatia sahihi sheria hiyo.

Mara tu Danieli aliposikia kuhusu sheria hiyo, akaenda nyumbani kwake. Akapiga magoti mbele ya dirisha lake lililokuwa wazi, na kusali kwa Yehova. Wale wanaume wenye wivu wakajazana ndani ya nyumba ya Danieli na kumkuta akisali. Wakakimbia kwenda kwa Dario na kumwambia hivi: ‘Danieli hakutii. Anasali kwa Mungu wake mara tatu kila siku.’ Dario alimpenda Danieli, naye hakutaka afe. Mchana kutwa akawa anafikiria jinsi atakavyomwokoa Danieli. Lakini hata mfalme hangeweza kubadili sheria ambayo yeye mwenyewe alikuwa ametia sahihi. Alilazimika kuwaamuru watu wake wamtupe Danieli ndani ya shimo lenye simba wakali.

Usiku huo Dario alikuwa na wasiwasi sana kumhusu Danieli hivi kwamba hakuweza kupata usingizi. Asubuhi ilipofikia, akakimbia kwenda kwenye shimo la simba na kumwuliza hivi Danieli: ‘Je, Mungu wako alikuokoa?’

Dario akasikia sauti. Sauti ya Danieli! Akamjibu hivi Dario: ‘Malaika wa Yehova alifunga vinywa vya simba. Hawakunidhuru hata kidogo.’ Dario alifurahi sana! Akaagiza kwamba Danieli atolewe kwenye shimo. Danieli hakuwa hata na mkwaruzo. Kisha mfalme akaamuru hivi: ‘Watupeni wanaume waliomshtaki Danieli ndani ya shimo la simba.’ Wanaume hao walipotupwa, simba wakawararua.

Dario akawaamuru watu wote hivi: ‘Kila mtu lazima amwogope Mungu wa Danieli. Alimwokoa Danieli kutoka katika shimo la simba.’

Je, wewe husali kwa Yehova kila siku, kama Danieli?

“Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa kutoka kwenye jaribu watu wenye ujitoaji-kimungu.”​—2 Petro 2:9