Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 66

Ezra Alifundisha Sheria ya Mungu

Ezra Alifundisha Sheria ya Mungu

Miaka 70 hivi ilikuwa imepita tangu Waisraeli warudi Yerusalemu, lakini baadhi yao bado walikuwa wakiishi katika maeneo mbalimbali ya Milki ya Uajemi. Mmoja wao alikuwa kuhani aliyeitwa Ezra, ambaye alifundisha Sheria ya Yehova. Ezra aliambiwa kwamba watu huko Yerusalemu hawakuwa wakifuata Sheria, hivyo akataka kwenda kuwasaidia. Mfalme Artashasta wa Uajemi akamwambia hivi: ‘Mungu alikupatia hekima ili ufundishe Sheria yake. Unaweza kwenda pamoja na mtu yeyote atakayetaka kuandamana nawe.’ Ezra akakutana na wote waliotaka kurudi Yerusalemu. Wakasali kwamba Yehova awalinde katika safari yao ndefu, na kisha wakaondoka.

Miezi minne baadaye, wakafika Yerusalemu. Wakuu waliokuwa Yerusalemu wakamwambia Ezra hivi: ‘Waisraeli wamekataa kumtii Yehova na wameoa wanawake wanaoabudu miungu ya uwongo.’ Ezra alifanya nini? Ezra alipiga magoti mbele ya watu na kusali hivi: ‘Yehova, umetufanyia mambo mengi sana, lakini tumekutendea dhambi.’ Watu wakatubu, lakini wakaendelea kufanya mambo fulani yasiyo sawa. Ezra akawachagua wazee na waamuzi wachunguze mambo hayo. Kwa miezi mitatu iliyofuata, wale ambao hawakumwabudu Yehova wakafukuzwa.

Miaka 12 ikapita. Katika kipindi hicho, kuta za Yerusalemu zikajengwa upya. Hivyo, Ezra akawakusanya watu kwenye kiwanja cha watu wote ili awasomee Sheria ya Mungu. Ezra alipofungua kitabu hicho, watu wakasimama. Ezra akamsifu Yehova, na watu wakainua mikono kuonyesha kwamba wamekubali walichosikia. Kisha Ezra akasoma na kufafanua Sheria, na watu wakasikiliza kwa makini. Wakakiri kwamba walikuwa wamemkosea Yehova tena, na wakalia. Siku iliyofuata, Ezra akawasomea sehemu nyingine ya Sheria. Wakagundua kwamba walipaswa kusherehekea Sherehe ya Vibanda. Mara moja, wakaanza kujitayarisha kwa ajili ya sherehe hiyo.

Katika siku saba za sherehe hiyo, watu walishangilia na kumshukuru Yehova kwa kupata mavuno mazuri. Hawakuwa wamefanya Sherehe ya Vibanda kama hiyo tangu siku za Yoshua. Baada ya sherehe hiyo, wakakusanyika na kusali hivi: ‘Yehova ulituokoa kutoka utumwani, ukatulisha jangwani, na kutupatia nchi hii maridadi. Lakini tena na tena, tulikosa kutii. Ukawatuma manabii watuonye, lakini hatukusikiliza. Bado, ukatuonyesha subira. Ukatimiza ahadi yako kwa Abrahamu. Sasa tunakuahidi kwamba tutakutii.’ Wakaandika ahadi yao, na wakuu, Walawi, na makuhani wakatia muhuri wao juu yake.

“Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”​—Luka 11:28