Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 68

Elisabeti Apata Mtoto

Elisabeti Apata Mtoto

Miaka zaidi ya 400 baada ya kuta za Yerusalemu kujengwa upya, kuhani anayeitwa Zekaria na mke wake Elisabeti, waliishi karibu na jiji hilo. Walikuwa wamefunga ndoa kwa miaka mingi lakini hawakuwa na watoto. Siku moja Zekaria alipokuwa akifukiza uvumba katika patakatifu pa hekalu, malaika Gabrieli akamtokea. Zekaria akaogopa sana, lakini Gabrieli akamwambia: ‘Usiogope. Ninakuletea habari njema kutoka kwa Yehova. Mke wako, Elisabeti, atapata mtoto na utamwita jina lake Yohana. Yehova amemchagua Yohana afanye kazi ya pekee.’ Zekaria akauliza: ‘Ninawezaje kukuamini? Mimi na mke wangu ni wazee sana tusiweze kupata mtoto.’ Gabrieli akamwambia: ‘Nimetumwa na Mungu kukupatia habari hizi. Lakini kwa sababu hukuniamini, hutaweza kuzungumza mpaka mtoto huyo azaliwe.’

Zekaria alikaa katika patakatifu muda mrefu kuliko kawaida. Hivyo, mwishowe alipotoka nje, watu waliokuwa wakingoja walitaka kujua kilichotokea. Lakini Zekaria hakuweza kuzungumza. Angeweza tu kutoa ishara kwa mikono yake. Kisha watu wakatambua kwamba Zekaria alikuwa amepata ujumbe kutoka kwa Mungu.

Baada ya muda, Elisabeti akapata mimba na kuzaa mtoto mvulana, kama malaika alivyosema. Rafiki na watu wa ukoo wakaja kumwona mtoto. Walifurahi sana. Elisabeti akasema: ‘Ataitwa Yohana.’ Wakamwambia: ‘Hakuna yeyote katika familia yenu anayeitwa kwa jina hilo. Mwite Zekaria, jina la baba yake.’ Lakini Zekaria akaandika maneno haya: ‘Yohana ndilo jina lake.’ Wakati huohuo, Zekaria akaanza kuzungumza tena! Habari kuhusu mtoto huyo zikaenea kotekote katika Yudea, na watu wakajiuliza hivi: ‘Mtoto huyu atakuwa wa namna gani?’

Kisha Zekaria akajawa na roho takatifu. Akatoa unabii huu: ‘Na abarikiwe Yehova. Alimwahidi Abrahamu kwamba angemtuma mwokozi, Masihi ili kutuokoa. Yohana atakuwa nabii, atatayarisha njia kwa ajili ya Masihi.’

Maria, mtu wa ukoo wa Elisabeti pia alipata tukio la pekee. Acheni tuchunguze jambo hilo katika sura inayofuata.

“Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”​—Mathayo 19:26