Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 69

Gabrieli Amtembelea Maria

Gabrieli Amtembelea Maria

Elisabeti alikuwa na mtu wa ukoo kijana aliyeitwa Maria, ambaye aliishi katika mji wa Nazareti huko Galilaya. Maria alikuwa mchumba wa Yosefu, aliyekuwa seremala. Elisabeti alipokuwa na mimba ya miezi sita, malaika Gabrieli alimtokea Maria. Akamwambia hivi: ‘Siku njema, Maria. Yehova amekupendelea sana.’ Hakuelewa kile ambacho Gabrieli alimaanisha. Kisha akamwambia hivi: ‘Utachukua mimba na kuzaa mwana, nawe utamwita Yesu. Atatawala akiwa Mfalme. Ufalme wake hautakuwa na mwisho.’

Maria akamwambia: ‘Lakini mimi silali na mwanamume. Hilo litawezekenaje?’ Gabrieli akajibu: ‘Hakuna lolote lisilowezekana kwa Yehova. Roho takatifu itakuja juu yako, nawe utapata mwana. Elisabeti mtu wa jamaa yako amechukua mimba pia.’ Kisha Maria akasema: ‘Mimi ni kijakazi wa Yehova. Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.’

Maria akaenda kumtembelea Elisabeti kwenye jiji lenye milima. Maria alipomsalimu, Elisabeti alihisi mtoto aliyekuwa tumboni mwake akiruka. Akiwa amejawa na roho takatifu, akasema hivi: ‘Maria, Yehova amekubariki. Ni pendeleo kuwa na mama ya Bwana wangu nyumbani kwangu.’ Maria akajibu hivi: ‘Nafsi yangu yote inamtukuza Yehova.’ Maria akaishi na Elisabeti kwa miezi mitatu, kisha akarudi nyumbani kwake Nazareti.

Yosefu alipogundua kwamba Maria alikuwa na mimba, alitaka kumtaliki. Lakini malaika akamtokea katika ndoto na kumwambia hivi: ‘Usiogope kumchukua awe mke wako. Hajafanya kosa lolote.’ Hivyo, Yosefu akamchukua Maria awe mke wake na akaenda naye nyumbani kwake.

“Yehova hufanya kila jambo apendalo mbinguni na duniani.”​—Zaburi 135:6