Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 70

Malaika Watangaza Kuzaliwa kwa Yesu

Malaika Watangaza Kuzaliwa kwa Yesu

Mtawala wa Milki ya Roma, Kaisari Augusto, alitoa amri kwamba Wayahudi wote warudi kwenye majiji yao ili waandikishwe. Kwa hiyo, Yosefu na Maria wakasafiri kwenda Bethlehemu, ambako Yosefu alizaliwa. Kwa wakati huo, Maria alikuwa karibu kuzaa.

Walipofika Bethlehemu, mahali pekee walipopata ni katika zizi. Hapo ndipo Maria alipomzaa mwana wake Yesu. Akamfunga kwa vitambaa na kumlaza kwa wororo katika hori.

Karibu na Yerusalemu, wachungaji fulani walikuwa nje wakati wa usiku, wakichunga makundi yao ya mifugo. Ghafula, malaika akasimama kando yao na utukufu wa Yehova ukamulika pande zote. Wachungaji hao wakaogopa, lakini malaika akawaambia hivi: ‘Msiogope, nina habari zenye kusisimua. Leo Masihi amezaliwa Bethlehemu.’ Wakati huohuo, malaika wengi wakatokea katika mbingu, wakisema: ‘Utukufu juu kwa Mungu, na amani juu ya dunia.’ Kisha malaika hao wakatoweka. Wachungaji hao walitendaje?

Wachungaji hao wakasemezana hivi: ‘Twendeni moja kwa moja hadi Bethlehemu.’ Nao wakaenda haraka na kuwakuta Yosefu na Maria katika hori wakiwa na mtoto wao mchanga.

Wote waliosikia juu ya mambo ambayo malaika aliwaambia wachungaji walistaajabu. Maria alifikiria sana kuhusu maneno ya yule malaika na hakuyasahau kamwe. Basi wachungaji wakarudi kwenye makundi yao ya mifugo, wakimshukuru Yehova kwa ajili ya mambo yote waliyosikia na kuona.

“Nilitoka kwa Mungu nami nipo hapa. Sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe, bali Yeye ndiye aliyenituma.”​—Yohana 8:42