Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 71

Yehova Alimlinda Yesu

Yehova Alimlinda Yesu

Katika nchi fulani iliyo upande wa mashariki mwa Israeli, kulikuwa na watu walioamini kwamba nyota zingeweza kuwaongoza. Pindi moja wakati wa usiku, wanaume fulani kutoka sehemu za mashariki waliona kile kilichoonekana kama nyota yenye kung’aa ikisonga angani, na wakaifuata. “Nyota” hiyo ikawaongoza hadi Yerusalemu. Wanaume hao wakaanza kuwauliza watu hivi: ‘Yuko wapi yule mtoto ambaye atakuwa mfalme wa Wayahudi? Tumekuja kumsujudia.’

Herode, mfalme wa Yerusalemu, aliposikia kuhusu mfalme mpya, akawa na wasiwasi sana. Akawauliza wakuu wa makuhani hivi: ‘Ni wapi huyu mfalme alipaswa kuzaliwa?’ Wakamwambia hivi: ‘Manabii walisema kwamba angezaliwa Bethlehemu.’ Kwa hiyo, Herode akawaita wale wanaume kutoka mashariki na kuwaambia hivi: ‘Nendeni Bethlehemu mkamtafute mtoto huyo. Kisha, mrudi na kunieleza yuko wapi. Mimi pia ninataka kumsujudia.’ Lakini alikuwa akisema uwongo.

“Nyota” ile ikaanza kusonga tena. Wanaume wale wakaifuata hadi Bethlehemu. “Nyota” ile ikatua juu ya nyumba fulani na wanaume hao wakaingia ndani ya nyumba hiyo. Wakampata Yesu akiwa na mama yake, Maria. Wakamsujudia mtoto yule na kumpa zawadi za dhahabu, ubani, na manemane. Je, kweli Yehova alikuwa amewatuma wanaume hao wamtafute Yesu? Hapana.

Usiku huo, Yehova akamwambia hivi Yosefu kupitia ndoto: ‘Herode anataka kumwangamiza Yesu. Mchukue mke na mwana wako na mkimbie kuingia Misri. Kaeni huko hadi niwaambie ni salama kwenu kurudi.’ Mara moja, Yosefu na familia yake wakaenda Misri.

Yehova alikuwa amewaambia wanaume waliotoka mashariki kwamba wasirudi kwa Herode. Herode alipotambua kwamba wanaume hao hawatarudi, akaingiwa na ghadhabu kubwa. Kwa kuwa hangeweza kumpata Yesu, aliagiza wavulana wote waliokuwa rika la Yesu walioko Bethlehemu wauawe. Lakini Yesu alikuwa salama katika nchi ya mbali ya Misri.

Baada ya muda, Herode akafa. Yehova akamwambia Yosefu hivi: ‘Sasa ni salama kwako kurudi.’ Yosefu, Maria, na Yesu wakarudi Israeli, na kuishi katika jiji la Nazareti.

“Hivyo ndivyo neno langu linalotoka katika kinywa changu litakavyokuwa . . . , na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”​—Isaya 55:11