Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 72

Yesu Akiwa Kijana

Yesu Akiwa Kijana

Yosefu na Maria waliishi Nazareti pamoja na Yesu na wana na binti zao wengine. Yosefu aliitegemeza familia yake kwa kufanya kazi ya useremala, na aliwafundisha kumhusu Yehova na Sheria yake. Familia hiyo ilienda katika sinagogi kwa ukawaida ili kuabudu, na pia jijini Yerusalemu kila mwaka ili kusherehekea Pasaka.

Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, kama ilivyokuwa kawaida, familia yao ilifunga safari ndefu kuelekea Yerusalemu. Jiji hilo lilikuwa limejaa watu waliokuwa wamekuja kusherehekea Pasaka. Baadaye, Yosefu na Maria wakaanza safari ya kurudi nyumbani, wakifikiri kwamba Yesu alikuwa akisafiri katika kikundi chao. Lakini walipomtafuta kati ya watu wao wa ukoo, hawakumpata.

Wakarudi Yerusalemu na kumtafuta mwana wao kwa siku tatu. Hatimaye, wakaenda hekaluni. Wakampata hekaluni, akiwa ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza kwa makini na kuwauliza maswali. Walimu hao walipendezwa sana na Yesu hivi kwamba wakaanza kumuuliza maswali. Nao walishangazwa na majibu yake. Waliona kwamba alielewa sheria ya Yehova.

Yosefu na Maria walikuwa wamepatwa na wasiwasi sana. Maria akasema hivi: ‘Mtoto, tumekuwa tukikutafuta kila mahali! Umekuwa wapi?’ Yesu akajibu hivi: ‘Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe hapa katika nyumba ya Baba yangu?’

Yesu akaenda nyumbani Nazareti pamoja na wazazi wake. Yosefu alimfundisha Yesu kazi ya useremala. Unafikiri Yesu alikuwa mtu wa aina gani alipokuwa kijana? Alipoendelea kukua, Yesu alifanya maendeleo katika hekima akizidi kupata kibali kwa Mungu na wanadamu.

“Ee Mungu wangu, ninafurahia kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu kabisa.”​—Zaburi 40:8