Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 73

Yohana Anatayarisha Njia

Yohana Anatayarisha Njia

Yohana, mwana wa Zekaria na Elisabeti, alikuwa nabii alipokuwa mtu mzima. Yehova alimtumia Yohana kuwafundisha watu kuhusu Masihi aliyekuwa karibu kuja. Lakini badala ya kufundisha katika masinagogi au katika miji, Yohana alihubiri nyikani. Watu walitoka Yerusalemu na sehemu zote za Yudea ili wafundishwe na Yohana. Aliwafundisha kwamba ili wampendeze Mungu, walihitaji kuacha kufanya mambo mabaya. Baada ya kumsikiliza Yohana, wengi walitubu dhambi zao, na Yohana akawabatiza katika Mto Yordani.

Yohana aliishi maisha rahisi. Alivaa mavazi yaliyotengenezwa kwa manyoya ya ngamia na chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwituni. Watu walishangazwa na Yohana. Hata Mafarisayo na Masadukayo wenye kiburi walikuja kumwona. Yohana aliwaambia hivi: ‘Mnahitaji kubadili njia zenu na kutubu. Msifikiri kwamba ninyi ni watu wa pekee kwa sababu tu mnasema ninyi ni watoto wa Abrahamu. Hilo halimaanishi ninyi ni watoto wa Mungu.’

Watu wengi walimwendea Yohana na kumuuliza: ‘Tunapaswa kufanya nini ili tumpendeze Mungu?’ Yohana akawaambia Wayahudi: ‘Ikiwa una mavazi mawili, mpe moja yule aliye na uhitaji.’ Unajua kwa nini alisema hivyo? Alitaka wanafunzi wake wajifunze kwamba ili wampendeze Mungu, lazima wawapende watu.

Yohana aliwaambia hivi wakusanya-kodi: ‘Iweni wanyoofu na msimdanganye mtu yeyote.’ Aliwaambia askari-jeshi hivi: ‘Msichukue rushwa wala kusema uwongo.’

Makuhani na Walawi walimwendea Yohana na kumuuliza: ‘Kila mtu anataka kujua, wewe ni nani?’ Yohana akawaambia: ‘Mimi ni sauti nyikani inayowaongoza watu kwa Yehova, kama tu Isaya alivyotabiri.’

Watu walipenda sana mambo ambayo Yohana alikuwa akiwafundisha. Wengi walijiuliza ikiwa Yohana ndiye Masihi. Lakini akawaambia: ‘Kuna mtu mwenye nguvu kuliko mimi anayekuja. Sistahili hata kufungua kamba ya viatu vyake. Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa roho takatifu.’

“Mtu huyo alikuja akiwa shahidi, ili atoe ushahidi kuhusu nuru, ili watu wa namna zote waamini kupitia kwake.”​—Yohana 1:7