Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 75

Ibilisi Anamjaribu Yesu

Ibilisi Anamjaribu Yesu

Baada ya Yesu kubatizwa, roho takatifu ilimwongoza aingie nyikani. Hakula kitu chochote kwa siku 40, naye akawa na njaa sana. Kisha Ibilisi akaja kumjaribu Yesu na kumwambia hivi: ‘Ikiwa wewe ni Mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mkate.’ Lakini Yesu akajibu kwa kunukuu Maandiko akisema: ‘Imeandikwa kwamba mtu anahitaji mengi zaidi ya chakula ili aendelee kuishi. Anahitaji kusikiliza kila neno ambalo Yehova anasema.’

Kisha, Ibilisi akamjaribu Yesu na kumwambia: ‘Ikiwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu, jitupe kutoka kwenye sehemu ya juu zaidi ya hekalu. Imeandikwa kwamba Mungu atawatuma malaika zake wakuchukue mikononi mwao.’ Lakini kwa mara nyingine Yesu akanukuu Maandiko na kusema: ‘Imeandikwa kwamba hupaswi kumjaribu Yehova.’

Kisha, Shetani akamwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu, utajiri wake, na utukufu wake naye akasema: ‘Nitakupa falme hizi zote na utukufu wake ikiwa utaniabudu mara moja tu.’ Lakini Yesu akajibu hivi: ‘Nenda zako, Shetani! Imeandikwa kwamba unapaswa kumwabudu Yehova peke yake.’

Kisha Ibilisi akaondoka, na malaika wakaja na kumpa Yesu chakula. Kuanzia wakati huo na kuendelea, Yesu akahubiri habari njema ya Ufalme. Hiyo ndiyo kazi aliyotumwa duniani kufanya. Watu walipenda sana mambo ambayo Yesu aliwafundisha, nao wakamfuata kila mahali alipoenda.

“[Ibilisi] anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” ​—Yohana 8:44