Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 77

Mwanamke Kisimani

Mwanamke Kisimani

Baada ya Pasaka, Yesu na wanafunzi wake wakasafiri kupitia Samaria walipokuwa wakirudi Galilaya. Yesu akafika katika sehemu iliyoitwa kisima cha Yakobo, karibu na jiji la Sikari. Alipokuwa akipumzika, wanafunzi wake wakaenda jijini kununua chakula.

Mwanamke mmoja akaja kwenye kisima hicho kuchota maji. Yesu akamwambia: “Nipe maji ninywe.” Mwanamke huyo akasema: ‘Kwa nini unazungumza nami? Mimi ni mwanamke Msamaria. Wayahudi hawazungumzi na Wasamaria.’ Yesu akamwambia: ‘Ikiwa ungejua mimi ni nani, ungeniomba nikupe maji yaliyo hai.’ Mwanamke huyo akamuuliza, ‘Unamaanisha nini? Huna hata ndoo.’ Yesu akasema: ‘Kila mtu anayekunywa maji ninayompa hatapatwa na kiu tena.’ Mwanamke huyo akasema: “Bwana, nipe maji hayo.”

Yesu akamwambia: ‘Nenda, ukamwite mume wako mje hapa kisimani.’ Mwanamke huyo akasema: ‘Sina mume.’ Yesu akamwambia: ‘Umesema kweli. Wewe umeolewa mara tano, na sasa unaishi na mwanamume ambaye si mume wako.’ Mwanamke huyo akasema: ‘Ninaona kwamba wewe ni nabii. Watu wetu wanaamini kwamba tunaweza kumwabudu Mungu katika mlima huu, lakini Wayahudi wanasema tunapaswa tu kuabudu kule Yerusalemu. Mimi ninaamini kwamba Masihi atakapokuja, yeye atatufundisha jinsi ya kuabudu.’ Kisha Yesu akamwambia jambo ambalo hakuwa amemwambia mtu mwingine yeyote: ‘Mimi ndiye Masihi.’

Mwanamke huyo akaenda upesi kwenye jiji la nyumbani kwake na kuwaambia Wasamaria hivi: ‘Nafikiri nimempata Masihi. Anajua kila kitu kunihusu. Njooni mwone!’ Wakamfuata hadi kisimani na kumsikiliza Yesu akifundisha.

Wasamaria walimkaribisha Yesu akae katika jiji lao. Kwa siku mbili, alifundisha katika jiji hilo, na watu wengi wakamwamini. Wakamwambia huyo mwanamke Msamaria hivi: ‘Baada ya kumsikiliza mwanamume huyu, tunajua kwamba kwa kweli yeye ndiye mwokozi wa ulimwengu.’

“‘Njoo!’ Na yeyote aliye na kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”​—Ufunuo 22:17