Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 79

Yesu Anafanya Miujiza Mingi

Yesu Anafanya Miujiza Mingi

Yesu alikuja duniani kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Ili kuonyesha mambo ambayo Yesu atatimiza akiwa Mfalme, Yehova alimpa roho takatifu ili afanye miujiza. Angeweza kuponya ugonjwa wowote. Popote alipoenda wagonjwa walimwendea ili awasaidie, naye akawaponya wote. Vipofu waliona, viziwi wakasikia, vilema wakatembea, na wale waliosumbuliwa na roho waovu wakawekwa huru. Waliponywa hata walipogusa tu upindo wa vazi lake. Watu walimfuata Yesu popote alipoenda. Hata alipotaka kuwa peke yake, kamwe Yesu hakumfukuza mtu yeyote.

Pindi moja, watu walimleta mwanamume aliyekuwa amepooza katika nyumba ambayo Yesu alikuwa akiishi. Lakini nyumba hiyo ilikuwa imejaa sana hivi kwamba hawangeweza kumwingiza ndani. Kwa hiyo, wakatoboa tundu kwenye paa na kumshusha mwanamume huyo kwa Yesu. Kisha Yesu akamwambia mwanamume huyo: ‘Simama utembee.’ Aliposimama, watu walishangaa sana.

Pindi nyingine, Yesu alipokuwa akiingia katika kijiji fulani, wanaume kumi waliokuwa na ukoma walisimama mbali na kumwambia Yesu kwa sauti kubwa: ‘Yesu, tusaidie!’ Katika siku hizo, watu wenye ukoma hawakuruhusiwa kuwakaribia watu wengine. Yesu akawaambia wanaume hao waende hekaluni, kwa kuwa Sheria ya Yehova ilisema watu wenye ukoma wanapaswa kwenda hekaluni baada ya kuponywa. Walipokuwa njiani, wakaponywa. Mmoja wao alipotambua kwamba ameponywa, alirudi kumshukuru Yesu na kumsifu Mungu. Kati ya wanaume wote kumi, ni huyo mmoja tu aliyemshukuru Yesu.

Mwanamke ambaye alikuwa mgonjwa kwa miaka 12 alitaka sana kuponywa. Alikuja nyuma ya Yesu akiwa katikati ya umati na kugusa upindo wa vazi lake la nje. Mara moja, akaponywa. Hilo lilipotukia, Yesu akauliza: “Ni nani aliyenigusa?” Ingawa mwanamke huyo aliogopa sana, alijitokeza na kumwambia ukweli. Yesu alimfariji kwa kumwambia: ‘Binti yangu, nenda kwa amani.’

Ofisa anayeitwa Yairo alimsihi Yesu hivi: ‘Njoo nyumbani kwangu! Binti yangu ni mgonjwa sana.’ Lakini kabla ya Yesu kufika nyumbani kwa Yairo, yule msichana akafa. Yesu alipofika, aliona watu wengi wakiomboleza na familia hiyo. Yesu akawaambia: ‘Msilie; msichana huyu amelala tu.’ Kisha akamshika msichana huyo mkono na kusema: “Msichana, inuka!” Yule msichana akainuka mara moja, na Yesu akawaambia wazazi wake wampe chakula. Hebu wazia jinsi wazazi hao walivyohisi!

“Mungu [alimtia] mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi, kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.”​—Matendo 10:38