Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 82

Yesu Anawafundisha Wanafunzi Wake Jinsi ya Kusali

Yesu Anawafundisha Wanafunzi Wake Jinsi ya Kusali

Lengo la mambo mengi ambayo Mafarisayo walifanya lilikuwa tu ili waonekane kwa watu. Kwa mfano, waliwatendea wengine kwa fadhili ili kujionyesha. Walisali kwenye maeneo yenye watu wengi ili kila mtu awaone. Pia, walikariri sala ndefu na kuzirudia rudia walipokuwa wanasali kwenye masinagogi au kwenye njia panda ili wengine wawasikie. Kwa hiyo, watu walishangaa Yesu alipowaambia hivi: ‘Msisali kama Mafarisayo. Wao hufikiri kwamba Mungu atafurahishwa na maneno mengi, lakini sivyo ilivyo. Sala ni kati yako wewe na Yehova. Msiseme mambo yaleyale tena na tena. Yehova anataka umwambie jinsi unavyohisi kikweli.

‘Mnapaswa kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”’ Aliwaambia kwamba wanapaswa kusali pia kuhusu mahitaji ya chakula cha siku hiyo, kuomba msamaha wa makosa yao, na kuhusu mambo mengine ya kibinafsi.

Yesu alisema hivi: ‘Msiache kamwe kusali. Endeleeni kumwomba Baba yenu, Yehova, mambo mazuri. Kila mzazi hupenda kumpa mtoto wake vitu vizuri. Ikiwa mtoto wako ataomba mkate, je, utampa jiwe? Akiomba samaki, je, utampa nyoka?’

Kisha, Yesu akafafanua somo la mfano huo: ‘Ikiwa ninyi mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba yenu, Yehova, hatawapa ninyi roho takatifu? Mnapaswa kuendelea kuomba.’ Je, unafuata ushauri wa Yesu? Wewe huwa unasali kuhusu mambo gani?

“Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.”​—Mathayo 7:7