Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 86

Yesu Amfufua Lazaro

Yesu Amfufua Lazaro

Yesu alikuwa na marafiki watatu wa karibu sana ambao waliishi Bethania. Marafiki hao ni Lazaro na dada zake wawili, Maria na Martha. Siku moja, Yesu alipokuwa ng’ambo ya Yordani, Maria na Martha walimtumia ujumbe huu wa dharura: ‘Lazaro ni mgonjwa sana. Tafadhali, njoo upesi!’ Hata hivyo, Yesu hakuenda mara moja. Alisubiri kwa siku mbili, kisha, akawaambia wanafunzi wake: ‘Twendeni Bethania. Lazaro amelala, nami ninaenda kumwamsha.’ Mitume wakamwambia hivi: ‘Ikiwa Lazaro amelala, hiyo itamsaidia kupata nafuu.’ Kwa hiyo, Yesu akawaambia hivi waziwazi: ‘Lazaro amekufa.’

Yesu alipofika Bethania, siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro alipozikwa. Umati mkubwa wa watu ulikuwa umekuja kuwafariji Martha na Maria. Baada ya Martha kusikia kwamba Yesu amekuja, alikimbia ili akampokee. Akamwambia hivi: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Yesu akamwambia: ‘Ndugu yako atafufuka. Martha, unaamini jambo hili?’ Akajibu: ‘Ninaamini kwamba atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.’ Yesu akamwambia: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.”

Kisha, Martha akaenda kwa Maria na kumwambia: ‘Yesu amekuja.’ Maria akatoka na kumkimbilia Yesu, nao umati ukamfuata. Alipofika, akaanguka miguuni pake huku akibubujikwa na machozi. Akamwambia Yesu: ‘Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu asingekufa.’ Yesu alipoona jinsi Maria anavyohuzunika, akatokwa na machozi. Umati ulipomwona akilia, wakasema: ‘Ona, jinsi Yesu alivyompenda Lazaro.’ Lakini wengine wakawa wakiuliza: ‘Kwa nini hakuzuia rafiki yake asife?’ Yesu angefanya nini?

Yesu alienda kwenye kaburi ambalo lilikuwa limefungwa kwa jiwe. Akawaamuru na kusema: “Liondoeni jiwe.” Martha akajibu: ‘Lakini siku nne zimepita! Mwili wake utakuwa unanuka.’ Hata hivyo, wakaliondoa jiwe, naye Yesu akasali na kusema: ‘Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia. Ninajua kwamba sikuzote wewe hunisikia; lakini ninasema kwa sauti ili watu hawa waamini kwamba umenituma.’ Kisha, akaita kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” Jambo la kushangaza likatokea: Lazaro akatoka kaburini, akiwa amefungwa kwa vitambaa. Yesu akawaambia: ‘Mfungueni, mwacheni aende.’

Wengi walioshuhudia ufufuo huo wakaanza kumwamini Yesu. Lakini wengine wakaenda na kuwaambia Mafarisayo. Tangu siku hiyo, Mafarisayo wakapanga njama ya kumuua Lazaro na Yesu. Yuda Iskariote, mmoja wa wale mitume 12, akaenda kisiri kwa Mafarisayo na kuwauliza: ‘Mtanipa nini nikiwasaidia kumkamata Yesu?’ Wakakubaliana kumpa vipande 30 vya fedha, hivyo, Yuda akawa akitafuta nafasi ya kumsaliti Yesu kwa Mafarisayo.

“Kwetu, Mungu wa kweli ni Mungu anayeokoa; Na Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu huokoa kutoka katika kifo.”​—Zaburi 68:20