Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 87

Mlo wa Mwisho wa Yesu

Mlo wa Mwisho wa Yesu

Wayahudi walisherehekea Pasaka kila mwaka katika siku ya 14 ya mwezi wa Nisani. Hilo liliwakumbusha jinsi Yehova alivyowakomboa kutoka katika utumwa nchini Misri na kuwaleta kwenye Nchi ya Ahadi. Katika mwaka wa 33 W.K., Yesu na mitume wake walisherehekea Pasaka katika chumba cha juu jijini Yerusalemu. Mwishoni mwa mlo huo, Yesu alisema hivi: ‘Mmoja wenu atanisaliti.’ Mitume walishtuka na kumuuliza Yesu: ‘Ni nani huyo?’ Yesu alijibu: ‘Ni mtu ambaye nitampa mkate.’ Kisha, akampa mkate Yuda Iskariote. Mara moja, Yuda akaondoka katika chumba hicho.

Baada ya hapo, Yesu akasali, akaumega mkate vipandevipande, na kuwagawia mitume waliokuwepo. Akasema hivi: ‘Kuleni mkate huu, unawakilisha mwili wangu, ambao nitautoa kwa ajili yenu.’ Halafu, akasali kwa ajili ya divai na kuwapa mitume wake. Akasema: ‘Kunyweni divai hii, inawakilisha damu yangu, ambayo nitaitoa ili msamehewe dhambi zenu. Ninawaahidi kwamba mtakuwa wafalme pamoja nami mbinguni. Kila mwaka, fanyeni hivi ili kunikumbuka.’ Wafuasi wa Yesu hukutana jioni ya Nisani 14 kila mwaka. Mkutano huo unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.

Baada ya mlo huo, mitume wakaanza kubishana kuhusu ni nani aliye mkubwa kati yao. Lakini Yesu akawaambia: ‘Yule aliye mkubwa kati yenu ni yule ambaye anajiona kuwa mdogo zaidi.

‘Ninyi ni rafiki zangu. Ninawaambia kila kitu ambacho Baba anataka niwaambie. Muda si mrefu nitaenda kwa Baba yangu aliye mbinguni. Nitawaacha ninyi, na watu watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu mkiwa na upendo kati yenu wenyewe. Mnapaswa kupendana kama vile mimi nilivyowapenda.’

Mwishowe, Yesu alisali kumwomba Yehova awalinde wanafunzi wake wote. Alimwomba Yehova awasaidie wanafunzi wake wafanye kazi kwa amani. Alisali ili jina la Yehova litakaswe. Kisha, Yesu na mitume wake waliimba nyimbo za kumsifu Yehova na kuondoka. Wakati wa Yesu kukamatwa ulikuwa umekaribia.

“Msiogope, ninyi kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa Ufalme.”​—Luka 12:32