Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 88

Yesu Akamatwa

Yesu Akamatwa

Yesu na mitume wake walitembea katika Bonde la Kidroni wakienda kwenye Mlima wa Mizeituni. Ilikuwa ni usiku na mwezi ulikuwa mpevu kabisa. Walipofika katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwaambia hivi: “Kaeni hapa na mwendelee kukesha.” Kisha, akaenda mbele kidogo katika bustani na kupiga magoti. Akiwa na uchungu mwingi alisali hivi kwa Yehova: “Acha mapenzi yako yatendeke.” Kisha, Yehova akamtuma malaika ili amfariji. Yesu aliporudi kwa mitume, alikuta watatu kati yao wakiwa wamelala. Akawaambia hivi: ‘Amkeni! Huu si wakati wa ninyi kulala! Saa imefika ya mimi kutiwa katika mikono ya adui zangu.’

Muda mfupi baadaye, Yuda alikuja akiwa na kundi kubwa la watu wenye mapanga na marungu. Alikuwa anajua mahali ambapo Yesu anaweza kupatikana kwa sababu walizoea kuja naye katika bustani hiyo mara kwa mara. Yuda alikuwa amewaambia askari kwamba atawasaidia kuwaonyesha Yesu. Hivyo, alikwenda moja kwa moja kwa Yesu na kusema: ‘Habari, Mwalimu,’ na kisha, akambusu. Yesu akamuuliza: ‘Yuda unanisaliti kwa kunibusu?’

Yesu akasogea mbele na kuuliza umati huo hivi: “Mnamtafuta nani?” Wakasema: “Yesu Mnazareti.” Akawajibu: “Mimi ndiye,” na mara moja wanaume hao wakarudi nyuma na kuanguka chini. Kwa mara nyingine Yesu akawauliza: “Mnamtafuta nani?” Wakamjibu: “Yesu Mnazareti.” Yesu akawajibu: ‘Nimewaambia mimi ndiye. Waacheni hawa waende zao.’

Petro alipoona kile kilichokuwa kikiendelea, alichomoa upanga wake na kukata sikio la Malko, mtumishi wa kuhani mkuu. Lakini Yesu akagusa sikio la mwanaume huyo na kumponya. Kisha, akamwambia Petro hivi: ‘Rudisha upanga wako mahali pake. Ukitumia upanga, utakufa kwa upanga.’ Askari wakamkamata Yesu na kumfunga mikono, lakini mitume wakakimbia. Kisha, umati ukampeleka Yesu kwa Anasi, kuhani mkuu. Anasi alimhoji Yesu, halafu akamtuma kwa Kuhani Mkuu Kayafa. Lakini ni nini kilichotokea kwa mitume?

“Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”​—Yohana 16:33