Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 91

Yesu Afufuliwa

Yesu Afufuliwa

Baada ya Yesu kufa, mwanamume fulani tajiri, aliyeitwa Yosefu, alimwomba Pilato amruhusu autoe mwili wa Yesu kutoka mtini. Yosefu akaufunga mwili wa Yesu kwa kitani bora na kuupaka manukato na kisha kuulaza ndani ya kaburi jipya. Pia akaviringisha jiwe kubwa kwenye mwingilio. Wakuu wa makuhani wakamwambia hivi Pilato: ‘Tunahofia kwamba baadhi ya wanafunzi wa Yesu watachukua mwili wake na baadaye watasema kwamba amefufuliwa.’ Hivyo Pilato akawaambia: ‘Funikeni mwingilio wa kaburi na mweke walinzi.’

Siku tatu baadaye, asubuhi sana, baadhi ya wanawake wakaenda kwenye kaburi na kupata kwamba jiwe lilikuwa limeondolewa. Ndani ya kaburi kulikuwa na malaika aliyewaambia hivi wanawake: ‘Msiogope. Yesu amefufuliwa. Nendeni mkawaambie wanafunzi wake wakakutane naye huko Galilaya.’

Maria Magdalene akaondoka haraka kwenda kuwatafuta Petro na Yohana. Akawaambia hivi: ‘Mtu fulani ameuchukua mwili wa Yesu!’ Petro na Yohana wakakimbia kwenda kaburini. Walipoona kuwa lilikuwa tupu, wakarudi nyumbani.

Maria aliporudi kaburini, aliona malaika wawili ndani na kuwaambia hivi: ‘Sijui walipompeleka Bwana wangu.’ Kisha akaona mwanamume fulani, na akidhania alikuwa mtunza-bustani, akasema: ‘Bwana, tafadhali niambie ulipomlaza.’ Lakini mwanamume huyo aliposema, “Maria!” akatambua kwamba alikuwa Yesu. Akalia na kusema: “Mwalimu!” na kumning’inia. Yesu akamwambia hivi: ‘Nenda kwa ndugu zangu nawe uwaambie kwamba umeniona.’ Mara moja, Maria akakimbia kwa wanafunzi wake na kuwaambia kwamba amemwona Yesu.

Baadaye siku hiyo, wanafunzi wawili walikuwa wakitembea kutoka Yerusalemu kwenda Emau. Mwanamume fulani akajiunga nao na kuwauliza walikuwa wakizungumza kuhusu nini. Wakasema: ‘Je, hujasikia? Siku tatu zilizopita wakuu wa makuhani walimwua Yesu. Sasa wanawake fulani wanasema kwamba yuko hai!’ Mwanamume huyo akauliza hivi: ‘Je, hamwaamini manabii? Walisema kwamba Kristo atakufa na kufufuliwa.’ Na akaendelea kuwaeleza maana ya Maandiko. Walipofika Emau, wanafunzi wakamwomba ajiunge nao. Wakati wa mlo wa jioni baada ya kusali kwa ajili ya mkate, wakatambua kuwa alikuwa Yesu. Kisha akatoweka.

Wanafunzi hao wawili wakafanya haraka kwenda Yerusalemu kwenye nyumba ambayo mitume walikuwa wamekutanika na wakawaambia kilichotokea. Walipokuwa kwenye nyumba hiyo, Yesu akatokea mbele yao wote. Mwanzoni, mitume hawakuamini kwamba alikuwa Yesu. Kisha akasema hivi: ‘Tazameni mikono yangu; niguseni. Iliandikwa kwamba Kristo angefufuka kutoka kwa wafu.’

“Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”​—Yohana 14:6