Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 93

Yesu Arudi Mbinguni

Yesu Arudi Mbinguni

Alipokuwa Galilaya, Yesu alikutana na wafuasi wake. Aliwapa amri hii muhimu sana: ‘Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. Wafundisheni mambo niliyowafundisha, na mwabatize.’ Kisha akawaahidi hivi: ‘Kumbukeni, nitakuwa pamoja nanyi sikuzote.’

Katika siku 40 baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea mamia ya wanafunzi wake huko Galilaya na Yerusalemu. Aliwafundisha mambo muhimu na kufanya miujiza mingi. Kisha Yesu akakutana na mitume wake kwa mara ya mwisho kwenye Mlima wa Mizeituni. Akasema hivi: ‘Msiondoke Yerusalemu. Endeleeni kusubiri kile ambacho Baba aliwaahidi.’

Mitume wake hawakuelewa alichokuwa akimaanisha. Wakamwuliza hivi: ‘Sasa utakuwa Mfalme wa Israeli?’ Yesu akasema, ‘Wakati wa Yehova wa kuniweka niwe Mfalme haujafika. Hivi karibuni mtapokea nguvu za roho takatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu. Nendeni mkahubiri katika Yerusalemu, Yudea, Samaria, na mpaka sehemu za mbali zaidi za dunia.’

Kisha Yesu akainuliwa juu angani na wingu likamfunika. Wanafunzi wake wakaendelea kutazama angani, lakini hakuwapo tena.

Wanafunzi wakaondoka kutoka Mlima wa Mizeituni na kwenda Yerusalemu. Wakawa wakikutana pamoja katika chumba cha juu na kusali. Walikuwa wakimsubiri Yesu awape maagizo zaidi.

“Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mathayo 24:1