Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 94

Wanafunzi Wapokea Roho Takatifu

Wanafunzi Wapokea Roho Takatifu

Siku kumi baada ya Yesu kurudi mbinguni, wanafunzi wake walipokea roho takatifu. Ilikuwa siku ya Pentekoste 33 W.K., na watu kutoka sehemu mbalimbali walikuwa wamekuja Yerusalemu kusherehekea. Kulikuwa na wanafunzi 120 hivi wa Yesu waliokuwa wamekusanyika kwenye chumba cha juu cha nyumba fulani. Ghafula, jambo la kushangaza likatokea. Kitu fulani kama moto kikatokea juu ya kichwa cha kila mwanafunzi, nao wakaanza kusema katika lugha mbalimbali. Kelele kama ya upepo wenye nguvu unaovuma ikaijaza ile nyumba.

Wageni kutoka sehemu mbalimbali waliokuja Yerusalemu walisikia kelele hizo na kwenda haraka kwenye nyumba hiyo ili kuona kilichotukia. Walishangaa waliposikia wanafunzi wakizungumza kwa lugha mbalimbali. Wakasema: ‘Lakini watu hawa ni Wagalilaya. Wanawezaje kusema katika lugha zetu?’

Kisha Petro na mitume wengine wakasimama mbele ya umati. Petro akawaeleza watu hao jinsi Yesu alivyouawa na kwamba Yehova alimfufua kutoka kwa wafu. Petro akasema: ‘Sasa Yesu yuko mbinguni kwenye mkono wa kuume wa Mungu, naye amemwaga roho takatifu kama alivyokuwa ameahidi. Ndiyo sababu mmeona na kusikia miujiza hii.’

Watu waliguswa sana na maneno ya Petro na wakauliza hivi: “Tufanye nini?” Petro akawaambia: ‘Tubuni dhambi zenu na mbatizwe katika jina la Yesu. Nanyi mtapokea zawadi ya roho takatifu.’ Siku hiyo, watu karibu 3,000 wakabatizwa. Kuanzia wakati huo na kuendelea, idadi ya wanafunzi ikaanza kuongezeka haraka jijini Yerusalemu. Kwa msaada wa roho takatifu, mitume wakaanzisha makutaniko zaidi ili waweze kuwafundisha wanafunzi mambo yote ambayo Yesu alikuwa amewaagiza.

“Ukitangaza waziwazi kwa kinywa chako kwamba Yesu ni Bwana, na kuwa na imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa.”​—Waroma 10:9