Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 96

Yesu Amchagua Sauli

Yesu Amchagua Sauli

Sauli alikuwa raia wa Roma aliyezaliwa Tarso. Alikuwa Farisayo mwenye ujuzi mwingi wa Sheria ya Kiyahudi, na aliwachukia Wakristo. Aliwakokota wanaume na wanawake Wakristo kutoka nyumbani kwao na kuwatupa gerezani. Hata alisimama na kuangalia umati wenye hasira ulipompiga mawe mwanafunzi Stefano hadi akafa.

Lakini Sauli hakuridhika kuwakamata Wakristo jijini Yerusalemu pekee. Alimwomba kuhani mkuu amtume katika jiji la Damasko ili awakamate Wakristo huko. Sauli alipokaribia jiji hilo, ghafula nuru nyangavu ilimulika kumzunguka pande zote, na akaanguka chini. Akasikia sauti ikisema: ‘Sauli, kwa nini unanitesa?’ Sauli akauliza: ‘Wewe ni nani?’ Akajibiwa: ‘Mimi ni Yesu. Nenda Damasko, nawe utaambiwa jambo unalopaswa kufanya.’ Papo hapo, Sauli akawa kipofu, na akalazimika kuongozwa kwa mkono mpaka jijini.

Jijini Damasko, kulikuwa na Mkristo mwaminifu aliyeitwa Anania. Yesu alimwambia hivi katika maono: ‘Nenda kwenye nyumba ya Yuda iliyo kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na umtafute Sauli.’ Anania akasema: ‘Bwana, ninajua mambo yote kuhusu mwanamume huyu! Anawatupa wanafunzi wako gerezani!’ Lakini Yesu akamwambia: ‘Nenda kwake. Nimemchagua Sauli ahubiri habari njema kwa mataifa mengi.’

Hivyo, Anania akampata Sauli na kumwambia: ‘Sauli, ndugu, Yesu amenituma nifungue macho yako.’ Mara moja, Sauli akaanza kuona tena. Akajifunza kumhusu Yesu na kuwa mfuasi wake. Baada ya kubatizwa akiwa Mkristo, Sauli akaanza kufundisha katika masinagogi pamoja na Wakristo wenzake. Je, unaweza kuwazia jinsi Wayahudi walivyoshtuka walipomwona Sauli akifundisha watu kumhusu Yesu? Walisema: ‘Je, huyu si mwanamume aliyekuwa akiwawinda wanafunzi wa Yesu?’

Kwa miaka mitatu, Sauli aliwahubiria watu walioishi Damasko. Wayahudi walimchukia Sauli na wakafanya mpango wa kumuua. Lakini ndugu walijua njama hiyo na wakamsaidia kutoroka. Walimweka kwenye kikapu na kumshusha chini kupitia tundu lililokuwa ukutani.

Sauli alipoenda Yerusalemu, alijaribu kujiunga na akina ndugu huko. Lakini walimwogopa. Halafu mwanafunzi mwenye fadhili anayeitwa Barnaba akampeleka Sauli kwa mitume na kuwasadikisha kwamba Sauli amebadilika. Sauli akaanza kuhubiri habari njema kwa bidii pamoja na kutaniko la Yerusalemu. Baadaye, aliitwa Paulo.

“Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda dhambi. Kati yao, mimi ndiye wa kwanza kabisa.”​—1 Timotheo 1:15