Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

96

Yesu Anamuchagua Sauli

Yesu Anamuchagua Sauli

Sauli alikuwa raia wa Roma. Alizaliwa Tarso. Alikuwa Mufarisayo, na alijua sana Sheria ya Wayahudi. Alikuwa anachukia Wakristo. Alikuwa anakamata na kutosha kwa nguvu wanaume na wanamuke Wakristo mu nyumba zao na kuwatia mu gereza. Wakati watu wenye kasirani walimuua Stefano, mwanafunzi wa Yesu, kwa kumupiga majiwe, Sauli alisimama pembeni na alikuwa anaangalia.

Sauli alipenda akamate na kutesa Wakristo wa Yerusalemu na wa miji ingine. Kwa hiyo, aliomba kuhani mukubwa amutume Damasko ili akamate Wakristo wenye walikuwa kule. Wakati Sauli alikaribia ule muji, mara moja mwangaza ukamuangazia pande zote, na akaanguka chini. Akasikia sauti inasema: ‘Sauli, juu ya nini unanitesa?’ Sauli akauliza: ‘Wewe ni nani?’ Sauti ikasema: ‘Mimi ni Yesu. Uende Damasko, na kule, watakuambia mambo yenye unapaswa kufanya.’ Palepale, Sauli akakuwa kipofu. Na iliomba mutu amukamate ku mukono na kumuongoza mupaka Damasko.

Mu muji wa Damasko, mulikuwa Mukristo muaminifu mwenye aliitwa Anania. Yesu alimuambia mu maono: ‘Uende ku nyumba ya Yuda, kwenye njia yenye kuitwa Yenye Kunyooka, na utafute Sauli.’ Anania akajibu: ‘Bwana, nimesikia mambo mingi juu ya ule mutu! Ametia wanafunzi wako mu gereza!’ Lakini Yesu akamuambia: ‘Uende uonane naye. Nimemuchagua ili ahubirie mataifa mingi habari njema.’

Anania akakutana na Sauli na kumuambia: ‘Sauli, ndugu yangu, Yesu amenituma nifungue macho yako.’ Mara moja, Sauli akaanza kuona tena. Akajifunza juu ya Yesu na akakuwa mufuasi wake. Kisha kubatizwa na kuwa Mukristo, Sauli akaanza kufundisha mu masinagogi pamoja na Wakristo wenzake. Lakini, Wayahudi walishituka wakati waliona Sauli iko anafundisha watu juu ya Yesu! Walisema: ‘Haiko huyu njo mwanaume mwenye alikuwa anawinda wanafunzi wa Yesu?’

Kwa miaka tatu, Sauli alihubiria watu wa Damasko. Wayahudi walimuchukia Sauli na walipenda kumuua. Lakini ndugu walisikia ile mipango ya mubaya na wakamusaidia Sauli kukimbia. Walimutia mu kitunga na kumushusha chini kupitia tundu lenye lilikuwa ku ukuta wa muji.

Wakati Sauli alifika Yerusalemu, alijaribu kujiunga na ndugu wa kule. Lakini walimuogopa. Kwa hiyo mwanafunzi mumoja mwenye huruma mwenye aliitwa Barnaba akamupeleka kwa mitume na kuwasadikisha kama Sauli alikuwa amebadilika kabisa. Kwa hiyo, Sauli akaanza kuhubiri habari njema kwa bidii pamoja na kutaniko la Yerusalemu. Kisha, alianza kuitwa Paulo.

“Kristo Yesu alikuja katika ulimwengu ili kuokoa watenda-zambi. Kati ya hao, mimi ni wa kwanza kabisa.”​—1 Timoteo 1:15