Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 97

Kornelio Apokea Roho Takatifu

Kornelio Apokea Roho Takatifu

Katika jiji la Kaisaria, kulikuwa na ofisa wa cheo cha juu aliyeitwa Kornelio. Ingawa hakuwa Myahudi, Wayahudi walimheshimu. Aliwasaidia kwa ukarimu maskini na watu wenye uhitaji. Kornelio alimwamini Yehova na alisali kwake kwa ukawaida. Siku moja, malaika alimtokea Kornelio na kusema hivi: ‘Mungu amesikia sala zako. Sasa, watume wanaume katika jiji la Yopa, ambako Petro anaishi, na umwombe aje kwako.’ Mara moja, Kornelio akawatuma wanaume watatu kwenda Yopa, jiji ambalo lilikuwa kilomita thelathini hivi upande wa kusini.

Wakati huohuo, jijini Yopa, Petro akapata maono. Aliona wanyama ambao wayahudi hawakuruhusiwa kula, na alisikia sauti ikimwambia ale. Petro alikataa akisema hivi: ‘Lakini sijawahi kamwe kula mnyama aliye najisi.’ Sauti hiyo ikamwambia tena hivi: ‘Usiwaite wanyama hawa najisi. Mungu amewatakasa.’ Petro aliambiwa hivi pia: ‘Kuna wanaume watatu mlangoni pako. Enda pamoja nao.’ Petro akaenda mlangoni na kuwauliza wanaume hao walitaka nini. Walijibu hivi: ‘Tumetumwa na Kornelio, ofisa jeshi Mroma. Unahitaji kwenda nyumbani kwake jijini Kaisaria.’ Petro akawakaribisha wanaume hao wawe wageni wake usiku huo. Siku iliyofuata, alienda nao jijini Kaisaria, pamoja na baadhi ya ndugu kutoka Yopa.

Hatimaye Kornelio alipomwona Petro, alipiga magoti. Lakini Petro akamwambia hivi: ‘Simama! Mimi ni mwanadamu kama wewe tu. Mungu aliniambia nije nyumbani kwako, ingawa Wayahudi hawaingii ndani ya nyumba za watu wa Mataifa. Tafadhali sasa, niambie kwa nini ulituma watu waniite.’

Kornelio akamwambia Petro hivi: ‘Siku nne zilizopita nilikuwa nikisali kwa Mungu, na malaika fulani akaniambia nitume watu wakuite. Tafadhali, tufundishe maneno ya Yehova.’ Petro akasema hivi: ‘Nimejifunza kwamba Mungu hana ubaguzi. Anamkubali mtu yeyote ambaye anataka kumwabudu.’ Petro aliwafundisha mambo mengi kumhusu Yesu. Kisha roho takatifu ikaja juu ya Kornelio na wote waliokuwa pamoja naye, na wote wakabatizwa.

“Katika kila taifa mtu anayemwogopa [Mungu] na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​—Matendo 10:35