Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

98

Ukristo Unaenea Katika Mataifa Mingi

Ukristo Unaenea Katika Mataifa Mingi

Yesu aliambia mitume wake wahubiri habari njema mu dunia yote, na ni vile walifanya. Mu mwaka wa 47, ndugu wa Antiokia walituma Paulo na Barnaba wafanye safari ya umisionere. Wale wahubiri wawili wenye bidii walisafiri mu eneo lote la Asia Ndogo, walitembelea maeneo sawa vile Derbe, Listra, na Ikoniamu.

Paulo na Barnaba walihubiria kila mutu, ikuwe tajiri ao maskini, kijana ao muzee. Watu mingi walikubali kweli kuhusu Kristo. Wakati Paulo na Barnaba walimuhubiria Sergio Paulo, gavana wa Saiprasi, mwanaume fulani mulozi alianza kuwapinga. Lakini Paulo aliambia ule mulozi: ‘Yehova atakupatia malipizi.’ Mara moja, ule mulozi akakuwa kipofu. Wakati Gavana Sergio Paulo aliona vile, akakuwa mwanafunzi wa Yesu.

Paulo na Barnaba walikuwa wanahubiri fasi yote: nyumba kwa nyumba, mu soko, mu barabara, na mu masinagogi. Wakati walipo- nyesha mwanaume mwenye alikuwa kilema kule Listra, wale wenye walijionea ule muujiza waliwaza kama Paulo na Barnaba walikuwa miungu na walijaribu kuwaabudu. Lakini Paulo na Barnaba waliwakataza kwa kusema: ‘Muabudu Mungu peke yake! Sisi ni wanadamu tu.’ Kisha, Wayahudi fulani walifika na kuchochea watu mingi wamupinge Paulo. Watu walimupiga majiwe, wakamukokota inje ya muji, na kumuacha kule kwa sababu waliwaza kama alishakufa. Lakini, alikuwa hajakufa! Mara moja, ndugu wakakuja kumubeba na kumurudisha katika muji. Kisha, Paulo akarudia Antiokia.

Mu mwaka wa 49, Paulo alifanya safari ya pili ya umisionere. Kisha kutembelea ndugu kule Asia Ndogo, alienda kuhubiri mbali sana, katika Ulaya. Alienda Atene, Efeso, Filipi, Tesalonike na sehemu zingine. Sila, Luka, na kijana mumoja mwenye kuitwa Timoteo walisafiri na Paulo. Walitumika pamoja ili kuanzisha makutaniko na kusaidia ndugu na dada wakuwe na imani ya nguvu. Paulo alibakia Korinto mwaka moja na nusu, na alikuwa anawatia moyo ndugu wenye waliishi kule. Alihubiri, alifundisha, na aliandikia makutaniko mingi barua. Ili apate mahitaji yake ya kimwili, alifanya kazi ya kutengeneza mahema. Kisha, Paulo alirudia Antiokia.

Mu mwaka wa 52, Paulo alifanya safari ya tatu ya umisionere. Alienda kwanza Asia Ndogo. Alisafiri mupaka Filipi, ngambo ya kaskazini, na kisha akashuka mupaka Korinto. Alifanya miaka mingi Efeso na iko anafundisha, anaponyesha wagonjwa na kusaidia kutaniko la Efeso. Kila siku alikuwa anatoa hotuba mu jumba la masomo fulani. Watu mingi walimusikiliza na walibadilisha tabia zao. Ku mwisho, kisha kuhubiri mu maeneo mingi, Paulo akaenda Yerusalemu.

“Kwa hiyo, muende, na mufanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”​—Matayo 28:19