Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 101

Paulo Apelekwa Roma

Paulo Apelekwa Roma

Safari ya tatu ya kuhubiri ya Paulo iliishia kule Yerusalemu. Akiwa huko, alikamatwa na kutupwa gerezani. Wakati wa usiku, Yesu alimwambia hivi katika maono: ‘Utaenda Roma na kuhubiri huko.’ Paulo alichukuliwa kutoka Yerusalemu na kupelekwa Kaisaria ambako alifungwa kwa miaka miwili gerezani. Alipokuwa akishtakiwa mbele ya Gavana Festo, Paulo alisema hivi: ‘Acha nihukumiwe na Kaisari, huko Roma.’ Festo akamwambia: “Umekata rufani kwa Kaisari; utaenda kwa Kaisari.” Paulo alisafirishwa kwa meli kwenda Roma. Ndugu wawili Wakristo, Luka na Aristarko, walienda pamoja naye.

Baharini, walipatwa na dhoruba ambayo ilivuma kwa siku nyingi. Kila mtu aliyekuwa ndani ya meli hiyo alifikiri kwamba angekufa. Lakini Paulo akawaambia: ‘Wanaume, malaika ameniambia hivi katika ndoto: “Usiogope, Paulo. Utafika Roma, na wale wote wanaosafiri pamoja nawe watakuwa salama.” Changamkeni! Hatutakufa.’

Dhoruba hiyo ilivuma kwa siku 14. Mwishowe, wakaona nchi kavu. Kilikuwa kisiwa cha Malta. Meli hiyo ikagonga mwamba na kuvunjika vipande-vipande, lakini watu wote 276 waliokuwa ndani ya meli hiyo, wakafika salama kwenye nchi kavu. Baadhi yao waliogelea na wengine walishikilia vipande vya meli hiyo na kuelea hadi pwani. Watu wa Malta wakawasaidia na hata waliwasha moto ili wapate joto.

Miezi mitatu baadaye, askari-jeshi wakampeleka Paulo hadi Roma kwa kutumia meli nyingine. Alipofika, akina ndugu walikuja kumpokea. Alipowaona, Paulo akamshukuru Yehova na kujipa nguvu. Ingawa Paulo alikuwa mfungwa, aliruhusiwa kuishi katika nyumba ya kukodiwa huku akilindwa na askari-jeshi. Aliishi pale kwa miaka miwili. Watu walikuja kumtembelea na akawahubiria kuhusu Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kumhusu Yesu. Pia, Paulo aliyaandikia barua makutaniko kule Asia Ndogo na Yudea. Kwa kweli, Yehova alimtumia Paulo kueneza habari njema kwa mataifa.

“Katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu, kwa kuvumilia mengi, kwa dhiki, kwa nyakati za uhitaji, kwa shida.”​—2 Wakorintho 6:4