Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Ndugu Zetu Wapendwa:

Tukiwa waabudu wa Yehova, tunalipenda Neno lake, Biblia. Tuna uhakika kwamba Biblia ina historia sahihi, mwongozo unaotegemeka kwa ajili ya maisha yetu, na uthibitisho wenye kugusa moyo kwamba Yehova anawapenda wanadamu. (Zaburi 119:105; Luka 1:3; 1 Yohana 4:19) Tunatamani sana kuwasaidia wengine wajifunze kweli hizo zenye thamani zilizo katika Neno la Mungu. Kwa sababu hiyo, tunafurahi sana kuwatolea kitabu hiki, Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia. Tafadhali acheni tuwaeleze mambo machache kuhusu kitabu hiki.

Kwa ujumla, kitabu hiki kimetayarishwa hasa kwa ajili ya watoto. Hata hivyo, kinaweza pia kutumiwa kuwasaidia watu wazima wanaotaka kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia. Na kwa sababu Biblia ni kitabu kinachowafaa watu wote, bila shaka sisi sote tutanufaika kwa kuchunguza masomo yaliyomo, ambayo yanaweza kutusaidia tupate furaha ya kweli.

Kitabu hiki kinatumia masimulizi ya Biblia kueleza hadithi kuhusu familia ya wanadamu kuanzia wakati wa uumbaji. Jitihada nyingi zimefanywa ili kuelezea masimulizi ya Biblia kwa njia rahisi na iliyo wazi. Pia, kwa kadiri iwezekanavyo, matukio hayo yamesimuliwa kwa mpangilio ambao yalitokea.

Hata hivyo, kitabu hiki hakielezi tu masimulizi ya Biblia. Maandishi na picha zimetayarishwa kwa njia ambayo masimulizi hayo ya Biblia yanaonekana kuwa halisi na kuonyesha waziwazi hisia za wahusika.

Kitabu hiki kinatusaidia kuona jinsi Biblia ilivyo kitabu kuhusu watu—watu ambao walimtii Yehova na wale ambao hawakumtii. Na kinatusaidia kujifunza mambo mbalimbali kutokana na mifano yao. (Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:6) Kitabu hiki kimegawanywa katika sehemu 14. Mwanzoni mwa kila sehemu kuna muhtasari wa baadhi ya masomo tunayoweza kujifunza.

Ikiwa wewe ni mzazi, unaweza kusoma somo moja pamoja na mtoto wako kisha mzungumzie picha zilizoonyeshwa. Kisha nyote wawili mnaweza kusoma mistari ya Biblia ambayo inategemeza somo hilo. Msaidie mtoto wako ahusianishe mambo anayosoma katika Biblia na somo hilo. Njia kama hiyo inaweza kufaa unapomsaidia mtu mzima kupata muhtasari wa mambo yanayozungumziwa katika Biblia.

Tunatumaini kwamba kitabu hiki kitawasaidia watu wote wenye mioyo minyoofu—vijana kwa wazee—wajifunze kutoka kwa Neno la Mungu na kutumia masomo wanayojifunza maishani mwao. Wanapofanya hivyo wao pia watamwabudu Mungu wakiwa sehemu ya familia yake.

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova