Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

“Yehova Mungu Wako Ndiye Unayepaswa Kumwabudu”

“Yehova Mungu Wako Ndiye Unayepaswa Kumwabudu”

MATHAYO 4:10

WAZO KUU: Kwa nini ibada safi inahitaji kurudishwa?

1, 2. Kwa nini Yesu alienda katika nyika ya Yudea majira ya vuli ya mwaka wa 29 W.K., na nini kilichompata huko? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

NI MWANZO wa majira ya vuli ya mwaka wa 29 W.K., na Yesu yuko katika nyika ya Yudea kaskazini ya Bahari ya Chumvi. Baada ya kubatizwa na kutiwa mafuta, aliongozwa na roho takatifu kwenda kwenye eneo hilo. Akiwa huko, katikati ya eneo lenye ukame, miamba na mabonde, Yesu ametumia siku 40 akifunga, kusali, na kutafakari akiwa peke yake. Labda wakati huo, Yehova amewasiliana na Mwana wake na kumtayarisha kwa ajili ya kazi iliyo mbele yake.

2 Sasa, Yesu akiwa amedhoofika kwa sababu ya njaa, Shetani anamwendea. Jambo linalotokea linafunua suala muhimu sana ambalo linawahusu watu wote wanaoipenda ibada safi, kutia ndani wewe.

“Ikiwa Wewe ni Mwana wa Mungu . . .”

3, 4. (a) Shetani alianza majaribu mawili ya kwanza kwa maneno gani, na huenda alikuwa akijaribu kumfanya Yesu awe na shaka kuhusu nini? (b) Shetani anatumiaje mbinu kama hizo leo?

3 Soma Mathayo 4:1-7. Shetani anaanza majaribu yake ya kwanza mawili kwa maneno haya ya ujanja, “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu.” Je, Shetani alikuwa na shaka kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu? Hapana. Malaika huyo mwasi aliyekuwa mwana wa Mungu alijua vizuri kwamba Yesu ni Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu. (Kol. 1:15) Bila shaka, Shetani pia aliyajua maneno haya ambayo Yehova alisema kutoka mbinguni wakati wa ubatizo wa Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:17) Labda Shetani alitaka Yesu afikiri kwamba Baba yake hakuwa mwaminifu na kwamba hakumjali. Katika jaribu la kwanza​—alilotaka abadili mawe yawe mikate—​ni kama Shetani aliuliza hivi: ‘Kwa kuwa wewe ni Mwana wa Mungu, kwa nini Baba yako hakupi chakula hapa nyikani?’ Katika jaribu la pili​—alilotaka aruke kutoka kwenye mnara wa hekalu—​tunaweza kusema Shetani aliuliza hivi: ‘Kwa kuwa wewe ni Mwana wa Mungu, je, unaamini kabisa kwamba Baba yako atakulinda?’

4 Shetani anatumia mbinu hizohizo leo. (2 Kor. 2:11) Mjaribu huyo anasubiri hadi wakati ambapo waabudu wa kweli wamedhoofika au kuvunjika moyo, kisha anawashambulia na mara nyingi anatumia ujanja. (2 Kor. 11:14) Anajaribu kutudanganya tuamini kwamba Yehova hawezi kamwe kutupenda wala kutukubali. Pia, Mjaribu huyo anajaribu kutufanya tuamini kwamba Yehova si mwaminifu, na hatatimiza ahadi zilizo katika Neno lake. Lakini huo ni uwongo mbaya sana. (Yoh. 8:44) Tunawezaje kuupinga uwongo huo?

5. Yesu alijibuje majaribu mawili ya kwanza?

5 Fikiria jinsi Yesu alivyojibu majaribu hayo mawili ya kwanza. Hakushuku kamwe kwamba Baba yake anampenda, naye alimtumaini kabisa Baba yake. Bila kusita, Yesu alimpinga Shetani kwa kunukuu Neno la Baba yake lililoongozwa na roho. Kwa kufaa, Yesu alinukuu maandiko yaliyo na jina la Mungu, Yehova. (Kum. 6:16; 8:3) Mwana wa Mungu alitumia njia bora sana kuonyesha kwamba alimtumaini Baba yake, alitumia jina Lake​—jina pekee ambalo linatoa uhakikisho kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote. *

6, 7. Tunawezaje kupinga mashambulizi ya Shetani ya ujanja?

6 Tunaweza kupinga mashambulizi ya kijanja ya Shetani kwa kulitegemea Neno la Yehova na kutafakari kuhusu maana ya jina la Mungu. Tukiamini mambo ambayo Maandiko yanasema kuhusu upendo wa Yehova na jinsi anavyowahangaikia waabudu wake, hata wale waliovunjika moyo, tunaweza kupinga uwongo wa Shetani kwamba Yehova hatupendi wala kutukubali. (Zab. 34:18; 1 Pet. 5:8) Na tukikumbuka kwamba sikuzote Yehova hutenda kulingana na maana ya jina lake, tutamtegemea kabisa Mtimizaji wa ahadi bila kuwa na shaka.—Met. 3:5, 6.

7 Hata hivyo, lengo kuu la Shetani ni nini? Anataka nini hasa kutoka kwetu? Tunapata jibu kutokana jaribu la tatu la Shetani kwa Yesu.

‘Anguka Chini Unifanyie Tendo la Ibada’

8. Shetani alifunuaje suala hususa katika jaribu la tatu?

8 Soma Mathayo 4:8-11. Katika jaribu la tatu, Shetani anaziacha mbinu zake za ujanja na kufunua lengo lake. Shetani alimwonyesha Yesu (labda kupitia maono) “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo”—lakini hakumwonyesha uovu wa falme hizo. Kisha akamwambia Yesu: “Nitakupa vitu hivi vyote ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” * Ibada​—ndiyo iliyokuwa kusudi lake kuu! Shetani alitaka Yesu amkatae Baba yake na kumkubali Mjaribu huyo kuwa ndiye mungu wake. Shetani alimshawishi Yesu kwa jambo ambalo lilionekana kuwa rahisi. Alimaanisha kwamba Yesu angekuwa na nguvu zote na utajiri wote wa mataifa na hangeteseka kwa kuvishwa taji la miiba, kupigwa mijeledi, au kutundikwa kwenye mti wa mateso. Jaribu hilo lilikuwa halisi. Yesu hakupinga mamlaka ya Shetani juu ya serikali za ulimwengu! (Yoh. 12:31; 1 Yoh. 5:19) Kwa kweli, Shetani angetoa chochote ili kumpotosha Yesu aache ibada safi ya Baba yake.

9. (a) Shetani anataka nini hasa kutoka kwa waabudu wa kweli, naye anajaribuje kutushawishi? (b) Ibada yetu inahusisha nini? (Tazama sanduku “Ibada Ni Nini?”)

9 Leo pia, Shetani anataka sana tumwabudu yeye​—moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Akiwa “mungu wa mfumo huu wa mambo,” anaabudiwa katika ibada zote za uwongo zinazofanywa na dini za Babiloni Mkubwa. (2 Kor. 4:4) Hata hivyo, hajatosheka na mabilioni ya waabudu wa uwongo, anawashawishi waabudu wa kweli watende kinyume na mapenzi ya Mungu. Anajaribu kutushawishi tufuatilie utajiri na umashuhuri katika ulimwengu wake badala ya kufuatilia mwendo wa Kikristo ambao unahusisha kuteseka “kwa ajili ya uadilifu.” (1 Pet. 3:14) Tukijiruhusu tushawishiwe kuacha ibada safi na kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani, tutakuwa tukimpigia magoti Shetani na kumfanyia tendo la ibada, na hivyo kumfanya awe mungu wetu. Tunawezaje kupinga kishawishi hicho?

10. Yesu alijibuje jaribu la tatu, na kwa nini?

10 Ona jinsi Yesu alivyojibu jaribu la tatu. Akionyesha ushikamanifu wake usioyumbayumba kwa Yehova, alimpinga haraka Mjaribu huyo, akisema: “Nenda zako, Shetani!” Kama alivyofanya katika majaribu mawili ya kwanza, Yesu ananukuu andiko. Ananukuu kitabu cha Kumbukumbu la Torati ambacho kina jina la Mungu: “Imeandikwa: ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Mt. 4:10; Kum. 6:13) Kwa hiyo, Yesu alipinga kishawishi cha kupata umaarufu wa muda mfupi katika ulimwengu na kuishi maisha ya starehe bila kuteseka. Alitambua kwamba Baba yake peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa na kwamba kumfanyia Shetani “tendo [moja] la ibada” kungemaanisha kumtii. Yesu alikataa kabisa Mjaribu huyo mwovu awe mungu wake. Alipokataa, “Ibilisi akamwacha.” *

“NENDA ZAKO, SHETANI!” (Tazama fungu la 10)

11. Tunawezaje kumpinga Shetani na majaribu yake?

11 Tunaweza kumpinga Shetani na vishawishi vya ulimwengu wake mwovu, kwa sababu kama Yesu tunaweza kufanya uamuzi. Yehova ametupatia zawadi yenye thamani sana ya uhuru wa kuchagua. Hivyo, hakuna mtu yeyote​—hata yule Mjaribu mwovu mwenye nguvu—​anayeweza kutulazimisha tuiache ibada safi. Tunapokuwa washikamanifu na kuchukua “msimamo dhidi [ya Shetani, tukiwa] imara katika imani,” tutakuwa tukisema: “Nenda zako, Shetani!” (1 Pet. 5:9) Kumbuka kwamba Shetani aliondoka baada ya Yesu kumpinga kwa uthabiti. Pia, Biblia inatuambia hivi: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—​Yak. 4:7.

Tunaweza kupinga vishawishi vya ulimwengu wa Shetani (Tazama fungu la 11, 19)

Adui wa Ibada Safi

12. Katika Edeni, Shetani alifunuaje kwamba yeye ni adui wa ibada safi?

12 Katika jaribu la mwisho, Shetani alithibitisha kwamba yeye ndiye adui mkuu wa ibada safi. Maelfu ya miaka mapema, katika bustani ya Edeni, Shetani alifunua kwa mara ya kwanza chuki yake dhidi ya ibada ya Yehova. Kwa kumdanganya Hawa, ambaye pia alimshawishi Adamu asitii amri ya Yehova, Shetani aliwafanya wawe chini ya uongozi na utawala wake. (Soma Mwanzo 3:1-5; 2 Kor. 11:3; Ufu. 12:9) Kihalisi akawa mungu wao, nao wakawa waabudu wake, hata kama huenda hawakujua ni nani hasa aliyekuwa akiwapotosha. Pia, kwa kuanzisha uasi huo katika bustani ya Edeni, Shetani hakupinga tu enzi kuu ya Yehova, au haki ya kutawala, bali pia alishambulia ibada safi. Jinsi gani?

13. Ibada safi inahusikaje katika suala la enzi kuu?

13 Suala la enzi kuu linahusu ibada safi. Mwenye Enzi kuu wa kweli, Yule ‘aliyeumba vitu vyote’ ndiye anayestahili kuabudiwa peke yake. (Ufu. 4:11) Yehova alipowaumba Adamu na Hawa wakiwa wakamilifu aliwaweka katika bustani ya Edeni. Alikusudia kwamba mwishowe dunia yote ingejaa wanadamu wakamilifu ambao wangemwabudu kwa hiari—ibada safi kutoka kwa mioyo safi. (Mwa. 1:28) Shetani alitilia shaka enzi kuu ya Yehova kwa sababu alitamani ibada ambayo ni haki ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova peke yake.—​Yak. 1:14, 15.

14. Je, Shetani alifaulu aliposhambulia ibada safi? Eleza.

14 Je, Shetani alifaulu katika shambulizi lake dhidi ya ibada safi? Alifaulu kuwapotosha Adamu na Hawa wamwache Mungu. Tangu wakati huo, Shetani amekuwa akipigana vita dhidi ya ibada safi, akitaka kuwapotosha wengi kadiri awezavyo wamwache Yehova Mungu. Shetani hakulegeza jitihada zake za kuwashawishi waabudu wa Yehova kabla ya Ukristo. Katika karne ya kwanza W.K., mwovu huyo alichochea uasi imani ambao ulichafua kutaniko la Kikristo, na mwishowe ikaonekana kana kwamba ibada safi imepotea. (Mt. 13:24-30, 36-43; Mdo. 20:29, 30) Kuanzia karne ya pili W.K., waabudu wa kweli waliingia katika kipindi kirefu cha utekwa wa kiroho katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Hata hivyo, Shetani hajafanikiwa kukomesha kusudi la Mungu kuhusu ibada safi. Hakuna kinachoweza kumzuia Mungu kutimiza kusudi lake. (Isa. 46:10; 55:8-11) Jina lake linahusika, na sikuzote yeye hutenda kulingana na jina lake. Yehova ni Mtimizaji asiyeshindwa wa kusudi lake!

Mteteaji Hodari wa Ibada Safi

15. Yehova alichukua hatua gani katika Edeni ili kuwaadhibu waasi na kuhakikisha kwamba kusudi lake lingefanikiwa?

15 Katika bustani ya Edeni, Yehova aliwachukulia hatua mara moja wale waasi na kuhakikisha kwamba kusudi lake litatimia. (Soma Mwanzo 3:14-19.) Adamu na Hawa wakiwa bado katika bustani, Yehova aliwahukumu wale waasi watatu, na alifanya hivyo kulingana na jinsi walivyokuwa wametenda dhambi—alianza na Shetani, kisha Hawa, na mwishowe Adamu. Katika maneno yake kwa Shetani, ambaye alianzisha uasi, Yehova alitabiri “uzao” ambao ungeondoa matokeo ya uasi. “Uzao” huo ulioahidiwa ungetimiza jukumu muhimu katika kutimiza kusudi la Yehova kuhusiana na ibada safi.

16. Baada ya uasi katika Edeni, Yehova alihakikishaje kwamba kusudi lake linaendelea kutimizwa?

16 Baada ya uasi katika Edeni, Yehova ameendelea kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimia. Alifanya mipango ili wanadamu ambao hawajakamilika wamwabudu kwa njia inayokubalika, kama tutakavyoona katika sura inayofuata. (Ebr. 11:4–12:1) Pia, aliwaongoza waandikaji wengi wa Biblia—​kutia ndani Isaya, Yeremia, Ezekieli—​waandike unabii wenye kusisimua kuhusu kurudishwa kwa ibada safi. Kurudishwa kwa ibada safi ni ujumbe muhimu katika Biblia. Unabii huo wote ungetimizwa na “uzao” ulioahidiwa, ambao ulithibitika hasa kuwa Yesu Kristo. (Gal. 3:16) Yesu ni Mteteaji Hodari wa ibada safi, kama alivyoonyesha waziwazi katika jibu lake kwa jaribu la tatu. Naam, Yesu ndiye aliyechaguliwa na Yehova ili atimize unabii wa kurudishwa kwa ibada safi. (Ufu. 19:10) Angewakomboa watu wa Mungu kutoka katika utekwa wa kiroho na kuirudisha ibada safi mahali pake.

Utafanya Nini?

17. Kwa nini unabii wa Biblia kuhusu kurudishwa kwa ibada safi unagusa mioyo yetu?

17 Kuchunguza unabii wa Biblia unaohusu kurudishwa kwa ibada safi kunasisimua na kuimarisha imani. Tunaupenda unabii huo kwa sababu tunatazamia kwa hamu wakati viumbe wote mbinguni na duniani watakapoungana katika ibada safi ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Pia, unabii huo utatupatia tumaini, kwa kuwa umejaa uhakikisho wenye kutia moyo unaopatikana katika Neno la Mungu. Ni nani kati yetu ambaye hatamani kuona ahadi za Yehova zikitimia—kutia ndani kufufuliwa kwa wapendwa wetu waliokufa, dunia paradiso, na maisha yasiyo na mwisho tukiwa na afya bora?—Isa. 33:24; 35:5, 6; Ufu. 20:12, 13; 21:3, 4.

18. Tutachunguza nini katika kitabu hiki?

18 Katika kitabu hiki, tutachunguza unabii wenye kusisimua katika kitabu cha Biblia cha Ezekieli. Mwingi kati ya unabii huo unakazia kurudishwa kwa ibada safi. Tutazungumzia jinsi unabii wa Ezekieli unavyohusiana na unabii mwingine, jinsi utakavyotimizwa kupitia Kristo, na jinsi tunavyohusika.​—Tazama sanduku “Muhtasari wa Ezekieli.”

19. Umeazimia kufanya nini, na kwa nini?

19 Katika nyika ya Yudea mwaka wa 29 W.K., Shetani alishindwa katika jaribio lake la kumshawishi Yesu aache ibada safi. Namna gani sisi? Kuliko wakati mwingine wowote, Shetani ameazimia kutuondoa katika ibada safi. (Ufu. 12:12, 17) Kitabu hiki na kitusaidie kuimarisha azimio letu la kumpinga Mjaribu huyo mwovu. Pia, na tuonyeshe kwa maneno na matendo kwamba tunakubaliana kabisa na maneno haya: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu.” Kisha tutakuwa na tumaini la kuishi na hatimaye kuona kusudi la Yehova lenye utukufu likitimizwa—wote mbinguni na duniani wakiungana kumpa Yehova kile anachostahili kabisa, yaani, ibada safi kutoka katika mioyo safi!

^ fu. 5 Baadhi ya watu wanaamini kwamba jina Yehova linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Ufafanuzi huo unafaana vizuri na jukumu la Yehova akiwa Muumba na Mtimizaji wa makusudi yake.

^ fu. 8 Kuhusu maneno ya Shetani, kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema hivi: “Katika simulizi la kwanza la kujaribiwa, ambalo Adamu na Hawa walianguka . . . , suala linahusu kuchagua kati ya mapenzi ya Shetani na mapenzi ya Mungu, jambo ambalo linamaanisha kumtolea kikamili ibada mmoja kati ya hao wawili. Kwa kweli, Shetani anajifanya kuwa mungu katika cheo cha Mungu wa pekee.”

^ fu. 10 Injili ya Luka inaorodhesha majaribu hayo kwa mpangilio tofauti, lakini inaonekana simulizi la Mathayo linataja jinsi matukio hayo yalivyofuatana. Chunguza sababu tatu. (1) Mathayo anaanza kutaja jaribu la pili kwa neno “ndipo,” kuonyesha kwamba ndilo tukio lililofuata. (2) Inapatana na akili kuamini kwamba majaribu mawili yaliyotungwa kwa ujanja—kila moja likianza kwa maneno, “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu”—yangefuatwa na jaribu la waziwazi la kuvunja amri ya kwanza. (Kut. 20:2, 3) (3) Maneno ya Yesu “Nenda zako, Shetani!” kwa kweli yangefuata jaribu la tatu na la mwisho.—Mt. 4:5, 10, 11.