Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 1

“Yehova Mungu Wako Ndiye Unapaswa Kuabudu”

“Yehova Mungu Wako Ndiye Unapaswa Kuabudu”

MATAYO 4:10

WAZO KUBWA: Juu ya nini ibada safi inapaswa kurudishwa

1, 2. Namna gani Yesu alifikia kuwa mu jangwa la Yudea mu kipindi cha mvua ya kwanza cha mwaka wa 29 K.K.Y., na ni mambo gani ilimufikia kule? (Ona picha ku mwanzo wa habari.)

NI MWANZO wa kipindi cha mvua ya kwanza cha mwaka wa 29 K.K.Y. Yesu iko mu jangwa la Yudea, kaskazini kabisa mwa Bahari ya Chumvi. Kisha kubatizwa na kutiwa mafuta, roho takatifu ilimuongoza aende kule. Yesu amepitisha siku 40 mu eneo hili lenye kukauka la miamba na mabonde, na amekuwa na wakati mutulivu wa kufunga, kusali, na kufikiri sana. Pengine ile wakati, Yehova ameongea na Mwana wake, juu ya kumutayarisha kuhusu mambo yenye ingetokea mbele.

2 Sasa, wakati Yesu anakuwa muzaifu juu ya njaa, Shetani anamukaribia. Mambo yenye inatokea kisha inaonyesha jambo moja la maana lenye linahusu watu wote wenye wanapenda ibada safi, na wewe pia.

“Kama Wewe Uko Mwana wa Mungu . . .”

3, 4. (a) Shetani alianza majaribu mbili ya kwanza kwa kutumia maneno gani, na pengine alitaka kumufanya Yesu akuwe na mashaka juu ya nini? (b) Namna gani Shetani anatumia njia za vile leo?

3 Soma Matayo 4:1-7. Shetani alianza majaribu mbili ya kwanza kwa kutumia maneno hii ya ujanja, “Kama wewe uko mwana wa Mungu.” Je, Shetani alikuwa na mashaka kama Yesu ni Mwana wa Mungu? Hapana. Malaika huyu wa Mungu mwenye alikuwa ameharibika alijua muzuri kama Yesu ni Mwana muzaliwa wa kwanza wa Mungu. (Kol. 1:15) Tena, Shetani alijua kabisa maneno yenye Yehova alisema kutoka mbinguni wakati Yesu alibatizwa: “Huyu ni Mwana wangu, mupendwa, mwenye nimekubali.” (Mt. 3:17) Pengine Shetani alitaka kufanya Yesu aanze kujiuliza kama kweli Baba yake alikuwa mwenye kutumainika na kama alimuhangaikia kabisa. Kupitia jaribu la kwanza​—la kugeuza majiwe kuwa mikate​—ni sawa vile Shetani aliuliza: ‘Kwa kuwa uko Mwana wa Mungu, juu ya nini Baba yako hakupatie chakula mu jangwa hili lenye kukauka?’ Kupitia jaribu la pili​—la kujitupa chini kutoka ku munara wa hekalu​—ni sawa vile Shetani aliuliza: ‘Kwa kuwa uko Mwana wa Mungu, unatumaini kabisa kama Baba yako atakulinda?’

4 Shetani anatumia njia za vile leo. (2 Ko. 2:11) Ule Mujaribu anangojea mupaka wakati waabudu wa kweli wanakuwa wazaifu ao wanavunjika moyo, kisha anawashambulia, mara mingi kwa kutumia njia za ujanja. (2 Ko. 11:14) Anatafuta kutufanya tuamini kama Yehova hawezi kutupenda wala kutukubali. Ule Mujaribu anatafuta pia kutufanya tuamini kwamba Yehova hatumainike, kwamba hatatimiza mambo yenye ameahidi mu Neno lake. Lakini ile ni uongo mubaya kabisa. (Yoh. 8:44) Namna gani tunaweza kukataa ile uongo?

5. Yesu alitenda namna gani wakati alikuwa mbele ya majaribu mbili ya kwanza?

5 Fikiria namna Yesu alitenda wakati alikuwa mbele ya ile majaribu mbili. Bila shaka alijua kwamba Baba yake anamupenda, na alimutegemea kabisa Baba yake. Bila kukawia, Yesu alipinga majaribu ya Shetani kwa kutaja maandiko ya Neno la Baba yake lenye kuongozwa na roho. Jambo la kupendeza ni kwamba, Yesu alitaja maandiko yenye kuwa na jina la Mungu, Yehova. (Kum. 6:16; 8:3) Je, hauone kwamba kwa kutumia jina la Mungu​—jina la pekee lenye kuhakikisha kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote​—Mwana wa Mungu alionyesha kwamba alimutumainia Baba yake? *

6, 7. Namna gani tunaweza kupinga njia za ujanja za Shetani?

6 Tunaweza kupinga njia za ujanja za Shetani kwa kutegemea Neno la Yehova na kwa kufikiri juu ya maana ya jina la Mungu. Biblia inatuambia kwamba Yehova anapenda watumishi wake, na zaidi sana wale wenye kuvunjika moyo. Kama sisi pia tuko hakika na ile jambo, tutaweza kupinga mawazo ya uongo ya Shetani yenye kuonyesha kwamba Yehova hawezi kutupenda wala kutukubali. (Zb. 34:18; 1 Pe. 5:8) Na kama tunaweka mu akili yetu kwamba Yehova anatenda kulingana na maana ya jina lake, hatutakuwa na mashaka na kuanza kuwaza kwamba Mutimizaji wa ahadi hastahili kutumainiwa kabisa.​—Mez. 3:5, 6.

7 Lakini, ni nini Shetani anatafuta kabisa? Kwa kweli, anataka tumupatie nini? Jibu lilionekana wazi wakati Shetani alimuletea Yesu jaribu la tatu.

“Ukianguka Chini na Kunifanyia Tendo la Ibada”

8. Kupitia jaribu la tatu, namna gani Shetani alionyesha kile alikuwa anatafuta kabisa?

8 Soma Matayo 4:8-11. Kupitia jaribu la tatu, Shetani aliacha ujanja na akaonyesha waziwazi kile alikuwa anatafuta kabisa. Shetani alimuonyesha Yesu (inawezekana mu maono) “falme zote za ulimwengu na utukufu wa falme hizo”​—lakini hakuonyesha matendo ya mubaya ya zile falme. Kisha akamuambia Yesu: “Nitakupatia vitu hivi vyote ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” * Ibada​—ni ile alikuwa anatafuta! Shetani alitaka Yesu amuache Baba yake na akubali ule Mujaribu kuwa mungu wake. Mambo yenye Shetani alimuahidi Yesu inaweza kuonekana kuwa njia yenye ingemuepusha na matatizo. Shetani alitaka kuonyesha kwamba Yesu angekuwa na mamlaka na mali yote ya mataifa na hangehitaji kuteseka​—hangetiwa taji la miiba ku kichwa, hangepigwa fimbo, hangebeba muti wa mateso. Ilikuwa jaribu kabisa. Yesu hakupinga kwamba Shetani njo alikuwa anaongoza guvernema za dunia! (Yoh. 12:31; 1 Yo. 5:19) Bila shaka Shetani alikuwa tayari kutoa kitu chochote juu ya kumufanya Yesu aache ibada safi ya Baba yake.

9. (a) Ni nini kabisa Shetani anatafuta waabudu wa kweli wamupatie, na anafanya nini juu ya kutujaribu? (b) Ibada yetu inatia ndani nini? (Ona kisanduku “Ibada Ni Nini?”)

9 Leo pia, Shetani anataka kabisa tumutolee ibada​—ikuwe moja kwa moja ao kwa njia yenye haiko ya moja kwa moja. Kwa sababu yeye ni “mungu wa mupangilio huu wa mambo,” yeye njo anapokea ibada yote ya uongo yenye kutolewa na dini za Babiloni Mukubwa. (2 Ko. 4:4) Lakini kwa sababu hatosheke na ile mamilioni ya waabudu wa uongo, anataka kujaribu waabudu wa kweli kusudi watende tofauti na mapenzi ya Mungu. Anajaribu kutuchochea tutafute mali na mamlaka mu ulimwengu wake kuliko kufuatilia maisha ya Kikristo yenye inaweza kutia ndani kuteseka “kwa sababu ya haki.” (1 Pe. 3:14) Kama tunajiacha tushindwe na ile jaribu ya kuacha ibada safi na kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani, kufanya vile itakuwa kumuinamia Shetani na kumufanyia tendo la ibada, kumufanya kuwa mungu wetu. Tunaweza kufanya nini juu ya kupinga jaribu sawa ile?

10. Namna gani Yesu alitenda wakati alikuwa mbele ya jaribu la tatu, na juu ya nini?

10 Ona namna Yesu alitenda wakati alikuwa mbele ya jaribu la tatu. Juu ya kuonyesha kama alikuwa mushikamanifu kwa Yehova tu, mara moja alimufukuza ule Mujaribu, kwa kusema: “Toka mbele yangu, Shetani!” Kisha, kama vile alifanya wakati wa majaribu mbili ya kwanza, Yesu alitaja andiko moja la Kumbukumbu la Torati lenye kuwa na jina la Mungu, kwa kusema: “Imeandikwa: ‘Yehova Mungu wako ndiye unapaswa kuabudu, na yeye peke yake ndiye unapaswa kutolea utumishi mutakatifu.’” (Mt. 4:10; Kum. 6:13) Kwa kusema vile, Yesu alipinga jaribu la kupewa kazi yenye ingemufanya ajulikane sana mu dunia lakini yenye haingedumu, na alikataa maisha ya muzuri ya bila kuteseka. Alitambua kwamba Baba yake tu njo anastahili kuabudiwa na kwamba kumufanyia Shetani hata ‘tendo moja tu la ibada’ kungemaanisha kwamba anajitiisha kwake. Yesu alikataa kabisa kumufanya ule Mujaribu muovu kuwa mungu wake. Kwa sababu Yesu alikataa mambo yenye Ibilisi alisema, “Ibilisi akamuacha.” *

“TOKA MBELE YANGU, SHETANI!” (Ona fungu la 10)

11. Namna gani tunaweza kupinga Shetani na majaribu yake?

11 Tunaweza kupinga Shetani na majaribu ya ulimwengu wake muovu kwa sababu, kama Yesu, tuko na uhuru wa kuchagua. Yehova ametupatia zawadi ya maana sana: Uhuru wa kuchagua. Kwa hiyo, hakuna mutu mwenye anaweza kutukaza tuache ibada safi, hata ule Mujaribu mwenye nguvu na muovu. Wakati ‘tunamupinga [Shetani]’ kwa ushikamanifu ‘tukiwa imara katika imani,’ ni kama vile tunasema: “Toka mbele yangu, Shetani!” (1 Pe. 5:9) Kumbuka, Shetani aliondoka wakati Yesu alimupinga kabisa. Vilevile, Biblia inatuhakikishia hivi: “Mumupinge Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”​—Yak. 4:7.

Tunaweza kuchagua kupinga majaribu ya ulimwengu wa Shetani (Ona fungu la 11, 19)

Adui wa Ibada Safi

12. Mu Edeni, namna gani Shetani alionyesha kama yeye ni adui wa ibada safi?

12 Kupitia jaribu la mwisho, Shetani alihakikisha kwamba yeye njo adui wa kwanza wa ibada safi. Miaka mingi sana mbele, mu bustani ya Edeni, Shetani alionyesha kwanza namna alichukia sana ibada ya Yehova. Kwa kumushawishi Eva, mwenye alichochea Adamu asitii amri ya Yehova, Shetani alitia Adamu na Eva chini ya uongozi na utawala wake. (Soma Mwanzo 3:1-5; 2 Ko. 11:3; Ufu. 12:9) Kusema kweli, alifikia kuwa mungu wao, nao wakakuwa waabudu wake, hata kama pengine hawakujua ni nani kabisa alikuwa anawapotosha. Zaidi ya ile, kwa kuanzisha ile uasi mu Edeni, Shetani alishambulia mamlaka makubwa zaidi ya Yehova, ao haki yake ya kutawala, na pia alishambulia ibada ya kweli. Juu ya nini tunasema vile?

13. Juu ya nini tunaweza kusema kama kuko uhusiano kati ya ibada safi na ulizo kuhusu mamlaka makubwa zaidi ya Yehova?

13 Kuko uhusiano kati ya ulizo kuhusu mamlaka makubwa zaidi ya Yehova na ibada safi. Ni vile kwa sababu Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi, Mwenye ‘aliumba vitu vyote,’ yeye tu njo anastahili ibada. (Ufu. 4:11) Wakati Yehova aliumba Adamu na Eva wakiwa wakamilifu na kuwatia mu bustani ya Edeni, kusudi lake lilikuwa dunia yote ifikie kujaa wanadamu wakamilifu wenye wangemutolea ibada yao kwa kupenda​—ibada safi yenye inatoka mu mioyo safi. (Mwa. 1:28) Shetani alishambulia mamlaka makubwa zaidi ya Yehova kwa sababu alitamani kitu chenye ni mali kabisa ya Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova, ni kusema, ibada.​—Yak. 1:14, 15.

14. Je, Shetani aliweza kushambulia ibada safi? Fasiria.

14 Je, Shetani aliweza kushambulia ibada safi? Aliweza kufanya Adamu na Eva wamuache Mungu. Tangu ile wakati, Shetani amepigana vita juu ya ibada ya kweli, kusudi afanye watu wengi kadiri inawezekana wamuache Yehova Mungu. Shetani hakuacha kujaribu waabudu wa Yehova wenye waliishi mu kipindi chenye kilitangulia Ukristo. Mu karne ya kwanza (1-100) K.K.Y., alitokeza kwa uovu uasi-imani wenye ulifanya kutaniko la Kikristo liharibike, na hivyo ilionekana kama ibada safi ilikuwa imepotea. (Mt. 13:24-30, 36-43; Mdo. 20:29, 30) Kuanzia karne ya pili (101-200) K.K.Y., waabudu wa kweli waliingia mu kipindi kirefu cha utekwa wa kiroho mu Babiloni Mukubwa, ni kusema, dini zote za uongo. Lakini Shetani hajaweza kuharibu mupango wa Mungu kuhusu ibada safi. Hakuna kitu kinaweza kuzuia kusudi la Mungu lisitimie. (Isa. 46:10; 55:8-11) Jina lake linahusika, na kila mara anatenda kulingana na maana ya jina lake. Sikuzote Yehova anatimizaka kusudi lake!

Muteteaji wa Ibada Safi

15. Yehova alikamata hatua gani mu Edeni juu ya kushugulika na waasi na juu ya kuhakikisha kwamba kusudi lake litatimia?

15 Bila kukawia, Yehova alikamata hatua fulani mu Edeni juu ya kushugulika na waasi na kuhakikisha kwamba kusudi lake litatimia. (Soma Mwanzo 3:14-19.) Hata wakati Adamu na Eva walikuwa wangali mu bustani, Yehova alihukumu wale waasi tatu, na alifanya vile kulingana na namna walifuatana katika kutenda zambi​—alianza na Shetani, kisha Eva, na akamalizia na Adamu. Wakati Yehova alikuwa anazungumuza moja kwa moja na Shetani, muchocheaji wa uasi mwenye Adamu na Eva hawakukuwa wanaona, alitabiri kama kungetokea “uzao” wenye ungeondoa matokeo ya uasi. Ule “uzao” wenye uliahidiwa ungefanya kazi kubwa juu ya kutimiza kusudi la Mungu kuhusu ibada safi.

16. Kisha uasi kutokea mu Edeni, Yehova alifanya nini juu kusudi lake lisikose kutimia?

16 Kisha uasi kutokea mu Edeni, Yehova aliendelea kutumika juu kusudi lake litimie. Alikamata mipango juu wanadamu wenye hawakamilike waweze kumuabudu mu njia yenye anakubali, kama vile tutaona mu sura ya kufuata. (Ebr. 11:4–12:1) Pia, kupitia roho yake, aliongoza waandikaji fulani wa Biblia​—kama vile Isaya, Yeremia, na Ezekieli—​kusudi waandike maunabii yenye kufurahisha kuhusu kurudishwa kwa ibada safi. Kurudishwa kwa ibada safi ni habari yenye kuzungumuziwa sana mu Biblia. Hii maunabii yote ingetimizwa kupitia “uzao,” wenye sehemu yake ya kwanza ni Yesu Kristo. (Gal. 3:16) Yesu ni Muteteaji wa ibada safi, kama vile alionyesha waziwazi kupitia jibu lenye alitoa wakati alijaribiwa mara ya tatu. Ndiyo, Yesu njo Yehova amechagua juu ya kutimiza maunabii kuhusu kurudishwa kwa ibada safi. (Ufu. 19:10) Yeye njo angekomboa watu wa Mungu mu utekwa wa kiroho na kurudisha ibada safi ku fasi yake.

Utafanya Nini?

17. Juu ya nini maunabii ya Biblia kuhusu kurudishwa kwa ibada safi inagusa moyo wetu?

17 Kuchunguza maunabii ya Biblia kuhusu kurudishwa kwa ibada safi kunafurahisha sana na kunatia imani nguvu. Ile maunabii inagusa moyo wetu kwa sababu tunangojea sana wakati wenye viumbe vyote mbinguni na duniani vitaungana mu ibada safi ya Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova. Tena, ile maunabii inatupatia tumaini, kwa sababu ndani yake munapatikana mauhakikisho fulani kati ya mauhakikisho mbalimbali yenye kutia moyo sana yenye inapatikana mu Neno la Mungu. Ni nani kati yetu mwenye hangojee kwa hamu kuona utimizo wa ahadi za Mungu​—kutia ndani ufufuo wa wapendwa wetu wenye wamekufa, dunia paradiso, na maisha ya milele pamoja na afya kamilifu?​—Isa. 33:24; 35:5, 6; Ufu. 20:12, 13; 21:3, 4.

18. Tutachunguza nini mu kitabu hiki?

18 Mu kitabu hiki, tutachunguza maunabii ya kufurahisha sana yenye kupatikana mu kitabu cha Biblia cha Ezekieli. Maunabii mingi ya kitabu cha Ezekieli inahusu zaidi sana kurudishwa kwa ibada safi. Tutazungumuzia namna maunabii ya Ezekieli inapatana na maunabii ingine, namna itatimizwa kupitia Kristo, na namna inatuhusu.​—Ona kisanduku “Kifupi cha Habari Zenye Kuwa Katika Ezekieli.”

19. Unaazimia kufanya nini, na juu ya nini?

19 Tukirudia mu jangwa la Yudea mwaka wa 29 K.K.Y., tunaona kwamba Shetani alishindwa wakati alijaribu kumuchochea Yesu ageuzie mugongo ibada ya kweli. Halafu sisi? Leo, Shetani ameazimia hata zaidi kutukokota mbali na ibada safi. (Ufu. 12:12, 17) Tunataka kitabu hiki kitusaidie kutia nguvu azimio letu la kupinga ule Mujaribu muovu. Na tujikaze kuonyesha kwa maneno na matendo kwamba tunakubaliana kabisa na maneno hii, “Yehova Mungu wako ndiye unapaswa kuabudu.” Tukifanya vile, tutakuwa na tumaini la kuishi na kuona namna kusudi la muzuri sana la Yehova litafikia kutimia​—watu wote mbinguni na duniani watamutolea Yehova kwa umoja kile anastahili kabisa, ibada safi yenye inatoka mu mioyo safi!

^ fu. 5 Kulingana na watu fulani, jina Yehova linamaanisha “Yeye Anafanya Kuwa.” Ile maana inapatana kabisa na cheo cha Yehova akiwa Muumbaji na Mutimizaji wa makusudi yake.

^ fu. 8 Kuhusu maneno ya Shetani, kitabu kimoja chenye kuzungumuzia Biblia kinasema: “Kama vile katika habari ya jaribu la kwanza kabisa, lenye Adamu na Eva walishindwa . . . , ulizo linahusu kuchagua kati ya mapenzi ya Shetani ao mapenzi ya Mungu, ni kusema, kutolea mumoja ibada ao mwingine. Shetani anajiona kwa kiburi kuwa mungu pa nafasi ya ule Mungu mumoja tu.”

^ fu. 10 Injili ya Luka inapanga ile majaribu mu njia tofauti, lakini Matayo anaipanga vile ilifuatana. Kuko sababu tatu. (1) Matayo anaanza jaribu la pili kwa kutumia neno “kisha,” ile inaonyesha kama lilitokea kisha lingine. (2) Ni jambo lenye kupatana na akili kufikiri kwamba ile majaribu mbili ya ujanja​—yenye kila jaribu lilianza na maneno, “Kama wewe uko mwana wa Mungu”—​ilipaswa kufuatwa na jaribu la wazi la kuomba mutu avunje amri ya kwanza. (Kut. 20:2, 3) (3) Maneno ya Yesu “Toka mbele yangu, Shetani!” ilipaswa kusemwa tu kisha jaribu la tatu, lile la mwisho.​—Mt. 4:5, 10, 11.