Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 2

“Mungu Alikubali” Zawadi Zao

“Mungu Alikubali” Zawadi Zao

WAEBRANIA 11:4

WAZO KUU: Historia ya mpango wa Yehova wa ibada safi

1-3. (a) Tutachunguza maswali gani? (b) Tutazungumzia mambo gani manne muhimu kuhusu ibada safi? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

ABELI anakagua mifugo yake kwa makini. Amefuga wanyama hao kwa upendo tangu walipozaliwa. Sasa anawachagua baadhi yao, anawachinja, na kuwatoa wakiwa zawadi kwa Mungu. Je, Yehova atakubali tendo hilo la ibada linalofanywa na mwanadamu asiye mkamilifu?

2 Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi kumhusu Abeli: “Mungu alikubali zawadi zake.” Hata hivyo, Yehova aliikataa dhabihu ya Kaini. (Soma Waebrania 11:4) Hilo linatokeza maswali ambayo tunapaswa kuyachunguza. Kwa nini Yehova alikubali ibada ya Abeli na si ya Kaini? Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya Kaini na Abeli na watu wengine wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11? Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuelewa vizuri mambo yanayohusika katika ibada safi.

3 Tunapozungumzia muhtasari wa matukio kuanzia kipindi cha Abeli hadi siku za Ezekieli, ona mambo haya manne muhimu ambayo kwa pamoja yanafanya ibada ikubalike kwa Mungu: Yehova ndiye anayepaswa kupokea ibada, inapaswa kuwa bora kabisa, inapaswa kutolewa kwa njia inayokubaliwa na Mungu, na yule anayemwabudu anapaswa kuwa na nia safi.

Kwa Nini Ibada ya Kaini Ilikataliwa?

4, 5. Ni nini kilichomfanya Kaini aamini kwamba Yehova ndiye angepokea zawadi yake?

4 Soma Mwanzo 4:2-5. Kaini alijua kwamba Yehova ndiye angepokea zawadi yake. Kaini alikuwa na muda na nafasi nyingi za kujifunza kumhusu Yehova. Huenda yeye na ndugu yake Abeli walikuwa na umri wa miaka 100 hivi walipomtolea Mungu zawadi zao. * Wavulana wote wawili walijua kuhusu bustani ya Edeni tangu utotoni, labda hata waliiona bustani hiyo maridadi kwa mbali. Bila shaka, waliwaona makerubi wakilinda mwingilio wa bustani hiyo. (Mwa. 3:24) Kwa hakika, wazazi wa wavulana hao waliwaambia kwamba Yehova aliumba kila kitu kilicho hai na kwamba kusudi lake la mwanzoni kwa ajili ya wanadamu ni tofauti na jinsi hali ilivyokuwa​—kuzeeka hatua kwa hatua na mwishowe kufa. (Mwa. 1:24-28) Huenda kujua mambo hayo kulimfanya Kaini afikiri kwamba anapaswa kumtolea Mungu zawadi yake.

5 Ni nini kingine ambacho huenda kilimchochea Kaini atoe dhabihu yake? Yehova alikuwa ametabiri kwamba “uzao” ungetokea, yaani, mtu ambaye angemponda kichwa “nyoka” aliyemdanganya Hawa afanye uamuzi mbaya. (Mwa. 3:4-6, 14, 15) Labda, Kaini akiwa mzaliwa wa kwanza, alifikiri kwamba yeye ndiye “uzao” huo uliotabiriwa. (Mwa. 4:1) Isitoshe, Yehova hakuwa amekatisha kabisa mawasiliano na wanadamu wenye dhambi; hata baada ya Adamu kufanya dhambi, inaelekea Mungu alizungumza naye kupitia malaika. (Mwa. 3:8-10) Na Yehova alizungumza na Kaini baada ya kutoa dhabihu yake. (Mwa. 4:6) Bila shaka, Kaini alijua kwamba Yehova ndiye anayestahili kuabudiwa.

6, 7. Je, Kaini alitoa dhabihu yake kwa njia isiyofaa au labda haikuwa bora? Eleza.

6 Basi, kwa nini Yehova hakuikubali dhabihu ya Kaini? Je, zawadi hiyo haikuwa bora? Biblia haitoi jibu. Kwa ufupi, inasema kwamba Kaini alileta “mazao ya shambani.” Baadaye, katika Sheria aliyompa Musa, Yehova alionyesha kuwa dhabihu kama hizo zinakubalika. (Hes. 15:8, 9) Pia, fikiria hali zilizokuwapo. Kipindi hicho, wanadamu walikula mimea peke yake. (Mwa. 1:29) Na kwa kuwa eneo lililokuwa nje ya Edeni lililaaniwa na Mungu, Kaini alikuwa amefanya kazi ngumu ili kupata mazao yake. (Mwa. 3:17-19) Alitoa chakula kinachoendeleza uhai, ambacho alikipata kwa jasho! Hata hivyo, Yehova hakuikubali dhabihu ya Kaini.

7 Au je, njia ambayo zawadi hiyo ilitolewa ilikuwa na kasoro? Je, Kaini alikosa kuitoa kwa njia inayofaa? Huenda isiwe hivyo. Kwa nini? Kwa sababu Yehova alipoikataa dhabihu ya Kaini, hakushutumu njia ambayo ilitolewa. Kwa kweli, Biblia haitaji njia ambayo Kaini na Abeli walitoa dhabihu zao. Basi, tatizo lilikuwa nini?

Kaini hakuwa na nia nzuri (Tazama fungu la 8, 9)

8, 9. (a) Kwa nini Yehova hakumkubali Kaini na dhabihu yake? (b) Unavutiwa na nini kuhusu habari zinazopatikana katika Biblia kumhusu Kaini na Abeli?

8 Maneno ya Paulo kwa Waebrania yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaonyesha kwamba Kaini hakutoa dhabihu hiyo akiwa na nia nzuri. Kaini hakuwa na imani. (Ebr. 11:4; 1 Yoh. 3:11, 12) Hiyo ndiyo sababu Yehova hakupendezwa hata kidogo na Kaini​—Kaini mwenyewe—​si dhabihu yake tu. (Mwa. 4:5-8) Yehova ni baba mwenye upendo, basi alijaribu kumrekebisha mwana wake kwa fadhili. Lakini Kaini, alikataa msaada wa Yehova. Moyo wa mfano wa Kaini ulijaa matendo ya mwili wenye dhambi​—“chuki, mizozo, wivu.” (Gal. 5:19, 20) Moyo mbaya wa Kaini ulifanya mambo mengine mazuri kuhusu ibada yake yasiwe na thamani yoyote. Mfano wake unatufundisha kwamba ibada safi inahitaji mengi kuliko kujionyesha tu kwa nje kwamba tunamwabudu Yehova.

9 Biblia inatuambia mengi kumhusu Kaini​—tunamsikia Yehova akizungumza naye, tunasoma Kaini anavyojibu, na hata tunasoma kuhusu majina ya watoto wake na kuhusu mambo waliyofanya. (Mwa. 4:17-24) Kuhusu Abeli, Biblia haitaji kwamba alikuwa na watoto na hakuna hata neno moja alilosema ambalo limeandikwa. Hata hivyo, bado matendo ya Abeli yanazungumza nasi leo. Jinsi gani?

Abeli Alituwekea Mfano Kuhusu Ibada Safi

10. Abeli alituwekeaje mfano mzuri kuhusu ibada safi?

10 Abeli alimtolea Yehova dhabihu yake, akijua kwamba Yehova peke yake ndiye anayestahili kuipokea. Alitoa dhabihu bora​—Abeli alichagua “baadhi ya wazaliwa wa kwanza wa mifugo yake.” Ingawa Biblia haisemi kama alitoa dhabihu yake kwenye madhabahu, ni wazi kwamba njia aliyotumia ilikubalika. Lakini jambo muhimu kuhusu zawadi ya Abeli ni nia yake ya kutoa, mfano ambao karibu miaka 6,000 baadaye bado tunapaswa kuuiga. Abeli alichochewa na imani yake katika Mungu na upendo wake kwa viwango vya uadilifu vya Yehova. Tunajuaje?

Abeli alitimiza mambo manne muhimu yanayohitajiwa katika ibada safi (Tazama fungu la 10)

11. Kwa nini Yesu alisema kwamba Abeli alikuwa mwadilifu?

11 Kwanza, fikiria jambo ambalo Yesu alisema kumhusu Abeli. Yesu alimfahamu vizuri. Yesu alikuwa mbinguni Abeli alipokuwa hai. Yesu alimpenda sana mwana huyo wa Adamu. (Met. 8:22, 30, 31; Yoh. 8:58; Kol. 1:15, 16) Basi, Yesu alikuwa akitoa ushahidi aliojionea aliposema kwamba Abeli alikuwa mwadilifu. (Mt. 23:35) Mtu mwadilifu anakubali kwamba Yehova ndiye anayepaswa kuweka viwango vya mema na mabaya. Lakini anafanya mengi zaidi—anaonyesha kwa maneno na matendo kwamba anakubaliana na viwango hivyo. (Linganisha Luka 1:5, 6.) Muda unahitajiwa ili mtu ajulikane kuwa mwadilifu. Hata kabla hajamtolea Mungu zawadi, Abeli alijulikana kuwa mtu aliyeishi kulingana na viwango vya Yehova. Haikuwa rahisi kwake kuwa mwadilifu. Inawezekana kwamba ndugu yake mkubwa hakumsaidia kwa kuwa moyo wa Kaini ulikuwa mwovu. (1 Yoh. 3:12) Mama yake Abeli alikosa kutii amri ya Mungu, na baba yake alikuwa amemwasi Yehova, akitaka kujiamulia mema na mabaya. (Mwa. 2:16, 17; 3:6) Abeli alionyesha ujasiri mkubwa kwa kuishi kwa njia tofauti na familia yake!

12. Kulikuwa na tofauti gani kubwa kati ya Kaini na Abeli?

12 Kisha, fikiria jinsi mtume Paulo anavyohusianisha sifa ya imani na uadilifu. Aliandika hivi: “Kwa imani, Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko ile ya Kaini, na kupitia imani hiyo alitolewa ushahidi kwamba alikuwa mwadilifu.” (Ebr. 11:4) Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba tofauti na Kaini, Abeli alichochewa na imani thabiti katika Yehova na njia yake ya kufanya mambo.

13. Mfano wa Abeli unatufundisha nini?

13 Mfano wa Abeli unatufundisha kwamba ibada safi inatoka tu katika moyo wenye nia nzuri​—moyo uliojaa imani katika Yehova na unaokubaliana kabisa na viwango vyake vya uadilifu. Isitoshe, tunajifunza kwamba ibada safi haihusishi tendo moja tu la ibada. Inahusisha maisha yetu yote, mwenendo wetu wote.

Wazee wa Ukoo Walifuata Mfano Huo

14. Kwa nini Yehova alikubali zawadi zilizotolewa na Noa, Abrahamu, na Yakobo?

14 Abeli alikuwa mtu wa kwanza asiye mkamilifu ambaye alimtolea Yehova ibada safi, lakini hakuwa wa mwisho. Mtume Paulo anawataja watu wengine waliomwabudu Yehova kwa njia inayokubalika—kama vile Noa, Abrahamu, na Yakobo. (Soma Waebrania 11:7, 8, 17-21.) Katika kipindi fulani maishani mwao, kila mmoja kati ya wazee hao alimtolea Yehova dhabihu, na Mungu aliikubali. Kwa nini? Kwa sababu wanaume hao hawakutoa tu ibada ya kidesturi—kila mmoja wao pia alitimiza matakwa yote muhimu kuhusiana na ibada safi. Fikiria mifano yao.

Dhabihu za Noa zilitoa ujumbe ulio wazi (Tazama fungu la 15, 16)

15, 16. Noa alitimizaje mambo manne muhimu yanayohitajika katika ibada safi?

15 Noa alizaliwa miaka 126 tu baada ya Adamu kufa; hata hivyo, alilelewa katika ulimwengu uliojaa ibada ya uwongo. * (Mwa. 6:11) Kati ya familia zote duniani muda mfupi kabla ya Gharika, ni Noa tu na familia yake waliomtumikia Yehova kwa njia inayokubalika. (2 Pet. 2:5) Baada ya kuokoka Gharika, Noa alichochewa kujenga madhabahu, madhabahu ya kwanza inayotajwa kihususa katika Biblia, kisha akamtolea Yehova dhabihu. Kupitia tendo hilo lililotoka moyoni, Noa aliionyesha waziwazi familia yake na wanadamu wengine wote ambao wangetokana naye jambo hili​—Yehova peke yake ndiye anayestahili kupokea ibada. Ingawa kulikuwa na wanyama wengi ambao angeweza kuwatoa kuwa dhabihu, Noa alichagua “baadhi ya wanyama walio safi na baadhi ya viumbe wanaoruka walio safi.” (Mwa. 8:20) Hizo zilikuwa dhabihu bora kwa sababu Yehova ndiye aliyewatangaza wanyama hao kuwa safi.​—Mwa. 7:2.

16 Noa alitoa dhabihu hizo za kuteketezwa kwenye madhabahu aliyotengeneza. Je, njia yake ya kuabudu ilikubaliwa? Ndiyo. Simulizi hilo linasema kwamba Yehova alipendezwa na harufu ya dhabihu hizo kisha akambariki Noa na wanawe. (Mwa. 8:21; 9:1) Hata hivyo, Yehova alizikubali dhabihu hizo hasa kwa sababu ya nia iliyomchochea Noa kuzitoa. Dhabihu hizo zilionyesha tena kwamba Noa alikuwa na imani thabiti katika Yehova na njia yake ya kufanya mambo. Kwa kuwa Noa alimtii Yehova kwa kuendelea kufuata viwango vyake, Biblia inasema kwamba “alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” Matokeo ni kwamba Noa alijulikana kuwa mtu mwadilifu.​—Mwa. 6:9; Eze. 14:14; Ebr. 11:7.

17, 18. Abrahamu alitimizaje mambo manne muhimu yanayohitajika katika ibada safi?

17 Abrahamu alizungukwa na ibada ya uwongo. Jiji la Uru, ambako Abrahamu aliishi, lilikuwa na hekalu la mungu mwezi aliyeitwa Nanna. * Wakati fulani hata baba ya Abrahamu aliabudu miungu ya uwongo. (Yos. 24:2) Hata hivyo, Abrahamu aliamua kumwabudu Yehova. Inawezekana kwamba alijifunza kumhusu Mungu wa kweli kupitia Shemu, babu yake, mmoja wa wana wa Noa. Waliishi wakati mmoja kwa kipindi cha miaka 150.

18 Katika maisha yake marefu, Abrahamu alitoa dhabihu nyingi. Lakini sikuzote alielekeza matendo hayo yanayokubalika ya ibada kwa yule tu aliyestahili kuyapokea, Yehova. (Mwa. 12:8; 13:18; 15:8-10) Je, Abrahamu alikuwa tayari kumtolea Yehova dhabihu bora kabisa? Swali hilo lilijibiwa kikamili Abrahamu alipokuwa tayari kumdhabihu Isaka, mwanawe mpendwa. Pindi hiyo, Yehova alitaja kihususa njia ambayo Abrahamu alipaswa kutoa dhabihu hiyo. (Mwa. 22:1, 2) Na Abrahamu alikuwa tayari kufuata maagizo hayo kikamili. Yehova ndiye aliyemzuia Abrahamu asimuue mwanawe. (Mwa. 22:9-12) Yehova alikubali ibada ya Abrahamu kwa sababu alikuwa na nia nzuri. Paulo aliandika hivi: “Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa uadilifu.”​—Rom. 4:3.

Yakobo aliiwekea familia yake mfano mzuri (Tazama fungu la 19, 20)

19, 20. Yakobo alitimizaje mambo manne muhimu yanayohitajika katika ibada safi?

19 Yakobo aliishi Kanaani kwa miaka mingi, nchi ambayo Yehova alikuwa ameahidi kumpa Abrahamu na wazao wake. (Mwa. 17:1, 8) Watu wa nchi hiyo walijihusisha sana na ibada iliyopotoka hivi kwamba Yehova akasema nchi hiyo ‘ingewatapika wakaaji wake.’ (Law. 18:24, 25) Yakobo alipokuwa na umri wa miaka 77, aliondoka Kanaani, akaoa, na baadaye akarudi akiwa na familia kubwa. (Mwa. 28:1, 2; 33:18) Lakini baadhi ya watu wa familia yake walishiriki katika ibada ya uwongo. Hata hivyo, Yehova alipomwambia Yakobo aende Betheli na kujenga madhabahu, Yakobo alitenda bila kusita. Kwanza aliiambia familia yake hivi: “Ondoeni kabisa miungu ya kigeni iliyo kati yenu, na mjisafishe.” Kisha akafuata kwa makini maagizo aliyopewa.—Mwa. 35:1-7.

20 Yakobo alijenga madhabahu kadhaa katika nchi ya ahadi, lakini sikuzote Yehova ndiye aliyepokea ibada hiyo. (Mwa. 35:14; 46:1) Dhabihu zake bora, njia aliyotumia kumwabudu Mungu, na nia yake ya kufanya hivyo inafanya aitwe “mtu asiye na lawama” katika Biblia. Maneno hayo yanawafafanua watu ambao wamekubaliwa na Mungu. (Mwa. 25:27) Kupitia maisha yake yote, Yakobo aliliwekea mfano bora taifa la Israeli, ambalo lingetokana naye.​—Mwa. 35:9-12.

21. Tunajifunza nini kuhusu ibada safi kutokana na mifano iliyowekwa na wazee wa ukoo?

21 Tunaweza kujifunza nini kuhusu ibada safi kutokana na mifano iliyowekwa na wazee wa ukoo? Kama wao, tunazungukwa na watu, labda hata watu wa familia ambao wanaweza kutukengeusha tusimwabudu Yehova peke yake. Ili kuepuka kushawishiwa, tunapaswa kusitawisha imani yenye nguvu katika Yehova na tuamini kabisa kwamba viwango vyake vya uadilifu ni bora. Tunaonyesha imani hiyo kwa kumtii Yehova na kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kumtumikia. (Mt. 22:37-40; 1 Kor. 10:31) Inatia moyo kujua kwamba tunapomwabudu Yehova kwa uwezo wetu wote, katika njia anayotaka, na tukiwa na nia nzuri, anatuona kuwa waadilifu!​—Soma Yakobo 2:18-24.

Taifa Lililokuwa na Bidii Katika Ibada Safi

22-24. Sheria ilikaziaje umuhimu wa yule aliyepaswa kupokea ibada, ubora wa dhabihu, na njia ambayo Waisraeli walitoa dhabihu?

22 Yehova aliwapa Sheria wazao wa Yakobo, na hivyo akawaonyesha kikamili mambo aliyotaka wafanye. Kama wangemtii Yehova, wangekuwa ‘mali yake ya pekee’ na “taifa takatifu.” (Kut. 19:5, 6) Ona jinsi Sheria ilivyokazia yale mambo manne muhimu kuhusu ibada safi.

23 Yehova alionyesha waziwazi yule aliyepaswa kupokea ibada ya Waisraeli. Yehova alisema: “Usiwe na miungu mingine yoyote ila mimi.” (Kut. 20:3-5) Walipaswa kumtolea dhabihu bora kabisa. Kwa mfano, walipaswa kutoa dhabihu za wanyama wasio vilema na wasio na kasoro. (Law. 1:3; Kum. 15:21; linganisha na Malaki 1:6-8.) Walawi walifaidika kutokana na zawadi ambazo Yehova alipewa, lakini wao pia walitoa dhabihu za kibinafsi. Walipaswa kutoa kutoka ‘katika zawadi bora zaidi walizopokea.’ (Hes. 18:29) Kuhusu njia ambayo waliabudu, Waisraeli walipewa maagizo hususa kuhusu aina ya dhabihu, mahali, na jinsi ilivyopaswa kutolewa kwa Yehova. Kwa ujumla, walipewa zaidi ya sheria 600 ili kuongoza matendo yao, nao wakaambiwa: “Mnapaswa kuwa waangalifu kufanya kama Yehova Mungu wenu alivyowaamuru. Msigeuke kwenda kulia wala kushoto.”​—Kum. 5:32.

24 Je, Waisraeli walipaswa kutoa dhabihu zao mahali fulani hususa? Ndiyo. Yehova aliwaagiza watu wake wajenge hema la ibada, nalo likawa kituo cha ibada safi. (Kut. 40:1-3, 29, 34) Wakati huo, ili dhabihu za Waisraeli zikubaliwe na Mungu, walipaswa kuzileta kwenye hema la ibada. *​—Kum. 12:17, 18.

25. Ni jambo gani lililokuwa muhimu zaidi kuhusu kutoa dhabihu? Eleza.

25 Hata hivyo, jambo lililokuwa muhimu zaidi ni nia ya Mwisraeli ya kutoa zawadi! Alipaswa kuchochewa kutoka moyoni kumpenda Yehova na viwango vyake. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:4-6.) Waisraeli waliposhiriki katika ibada safi kidesturi, Yehova alikataa dhabihu zao. (Isa. 1:10-13) Kupitia nabii Isaya, Yehova alifunua kwamba hawezi kudanganywa na ibada ya kinafiki, aliposema: “Watu hawa . . . huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali sana nami.​—Isa. 29:13.

Ibada Katika Hekalu

26. Mwanzoni, hekalu lililojengwa na Sulemani lilitimiza jambo gani katika ibada safi?

26 Karne nyingi baada ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Mfalme Sulemani alijenga kituo cha ibada kilichokuwa kikubwa zaidi kuliko hema la ibada. (1 Fal. 7:51; 2 Nya. 3:1, 6, 7) Mwanzoni, Yehova ndiye aliyepokea dhabihu zilizotolewa hekaluni. Sulemani na raia wake walitoa idadi kubwa ya dhabihu bora kwa njia iliyofafanuliwa katika Sheria ya Mungu. (1 Fal. 8:63) Hata hivyo, Yehova hakukubali ibada iliyofanywa katika hekalu kwa sababu tu ya gharama ya jengo hilo na idadi ya dhabihu zilizotolewa. Jambo muhimu lilikuwa nia ya wale waliotoa zawadi. Sulemani alikazia jambo hilo hekalu lilipokuwa likiwekwa wakfu. Alisema: “Acheni mioyo yenu iwe kamili kwa Yehova Mungu wetu kwa kufuata masharti yake na kushika amri zake kama ilivyo leo.”​—1 Fal. 8:57-61.

27. Wafalme wa Israeli na raia wao walifanya nini, na Yehova alitendaje?

27 Inasikitisha kwamba Waisraeli hawakuendelea kufuata ushauri wenye hekima wa mfalme. Walikosa kutimiza jambo moja au zaidi kati ya mambo muhimu kuhusu ibada safi. Wafalme wa Israeli na raia wao waliruhusu mioyo yao ipotoshwe, wakaacha kumwamini Yehova, na wakaacha kufuata viwango vyake vya uadilifu. Kwa upendo, Yehova aliwatuma tena na tena manabii wawarekebishe na kuwaonya kuhusu matokeo ya matendo yao. (Yer. 7:13-15, 23-26) Mmoja kati ya manabii hao ni mwanamume mwaminifu Ezekieli. Aliishi katika kipindi hatari cha historia ya ibada safi.

Ezekieli Aliona Ibada Safi Ikipotoshwa

28, 29. Tunajua nini kumhusu Ezekieli? (Tazama sanduku “Ezekieli​—Maisha na Nyakati Zake.”)

28 Ezekieli alifahamu vizuri ibada iliyofanywa katika hekalu lililojengwa na Sulemani. Baba yake alikuwa kuhani na inawezekana alifanya utumishi hekaluni kwa zamu. (Eze. 1:3) Huenda miaka ya utotoni ya Ezekieli ilikuwa yenye furaha. Bila shaka, baba yake alimfundisha kumhusu Yehova na Sheria yake. Karibu na kipindi ambacho Ezekieli alizaliwa “kitabu cha Sheria” kilipatikana hekaluni. * Mfalme mzuri Yosia aliyekuwa akitawala alichochewa sana na mambo aliyosikia hivi kwamba akazidisha jitihada zake za kuendeleza ibada safi.​—2 Fal. 22:8-13.

Bila shaka, baba ya Ezekieli alimfundisha kumhusu Yehova na Sheria (Tazama fungu la 28)

29 Kama wanaume waaminifu walioishi kabla yake, Ezekieli alitimiza yale matakwa manne kuhusu ibada safi. Kama kitabu cha Ezekieli kinavyoonyesha, alimtumikia Yehova peke yake, akajitahidi kutoa utumishi bora kwa kuendelea, na akatii kwa kufanya mambo ambayo Yehova alimwagiza na katika njia ambayo Yehova alitaka. Ezekieli alifanya mambo hayo yote kwa sababu alichochewa na moyo wenye imani. Haiwezi kusemwa hivyo kuhusu watu wengi walioishi kipindi hicho. Tangu utotoni Ezekieli alisikiliza unabii wa Yeremia, aliyeanza kazi yake mwaka wa 647 K.W.K., na ambaye alitoa onyo kwa bidii kuhusu hukumu ya Yehova iliyokuwa ikija.

30. (a) Unabii ulioandikwa na Ezekieli unafunua nini? (b) Unabii ni nini, na tunapaswa kuuelewaje unabii uliotolewa na Ezekieli? (Tazama sanduku “Kuuelewa Unabii wa Ezekieli.”)

30 Maneno ya Ezekieli yaliyoongozwa na roho yanaonyesha jinsi ambavyo watu wa Mungu walikuwa wameacha kumtumikia. (Soma Ezekieli 8:6.) Yehova alipoanza kutia nidhamu Yuda, Ezekieli alikuwa kati ya watu waliopelekwa utekwani huko Babiloni. (2 Fal. 24:11-17) Ingawa alikuwa mfungwa, Ezekieli hakuwa akiadhibiwa. Yehova alitaka afanye kazi fulani kati ya watu wake waliopelekwa uhamishoni. Maono yenye kustaajabisha na unabii ulioandikwa na Ezekieli yanaonyesha jinsi ambavyo ibada safi ingerudishwa huko Yerusalemu. Lakini tunajifunza mengi zaidi​—tunaona jinsi ambavyo mwishowe ibada safi itarudishwa kikamili kwa wote wanaompenda Yehova.

31. Kitabu hiki kitatusaidiaje?

31 Katika sehemu zinazofuata za kitabu hiki, tutaona makao ya mbinguni anakoishi Yehova, tutaona jinsi ambavyo ibada safi ilikuwa imechafuliwa, tutajifunza jinsi Yehova anavyowarudisha na kuwalinda watu wake, na tutachunguza wakati ujao ambapo kila mwanadamu aliye hai atamwabudu Yehova. Katika sura inayofuata, tutachunguza maono ya kwanza ambayo Ezekieli aliandika. Yanakazia katika akili zetu picha au taswira ya Yehova na sehemu ya mbinguni ya tengenezo lake, na kukazia kwa nini yeye peke yake ndiye anayepaswa kupokea ibada safi.

^ fu. 4 Inaelekea Abeli alizaliwa muda mfupi baada ya Adamu na Hawa kufukuzwa kutoka Edeni (Mwa. 4:1, 2) Mwanzo 4:25 inasema Mungu alimchagua Sethi ‘achukue mahali pa Abeli.’ Adamu alikuwa na umri wa miaka 130 alipomzaa Sethi, baada ya Abeli kuuawa kikatili. (Mwa. 5:3) Basi, huenda Abeli alikuwa na umri wa miaka 100 Kaini alipomuua.

^ fu. 15 Andiko la Mwanzo 4:26 linasema kwamba wakati wa Enoshi, mjukuu wa Adamu, “watu walianza kuliitia jina la Yehova.” Hata hivyo, ni wazi kwamba walikuwa wakifanya hivyo kwa dharau, labda wakilihusianisha jina la Yehova na sanamu.

^ fu. 17 Mungu wa kiume Nanna alijulikana pia kwa jina Sin. Ingawa wakaaji wa Uru waliabudu miungu mingi, mahekalu na madhabahu katika jiji hilo yaliwekwa wakfu kwake.

^ fu. 24 Baada ya Sanduku takatifu kuondolewa katika hema la ibada, inaonekana kwamba Yehova aliruhusu dhabihu zitolewe mahali pengine mbali na hema la ibada.​—1 Sam. 4:3, 11; 7:7-9; 10:8; 11:14, 15; 16:4, 5; 1 Nya. 21:26-30.

^ fu. 28 Inaonekana Ezekieli alianza kutoa unabii alipokuwa na umri wa miaka 30, mwaka wa 613 K.W.K. Kwa hiyo inaonekana alizaliwa karibu mwaka wa 643 K.W.K. (Eze. 1:1) Yosia alianza kutawala mwaka wa 659 K.W.K., na kitabu cha Sheria, labda nakala ya awali, ilipatikana karibu na mwaka wa 18 wa utawala wake, au karibu mwaka wa 642-641 K.W.K.