Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

“Nikaanza Kuona Maono ya Mungu”

“Nikaanza Kuona Maono ya Mungu”

EZEKIELI 1:1

WAZO KUU: Muhtasari wa maono ya Ezekieli kuhusu gari la kimbingu

1-3. (a) Eleza mambo ambayo Ezekieli anaona na kusikia. (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Ni nguvu gani iliyomwezesha Ezekieli kuona maono hayo, nayo ilimchocheaje?

EZEKIELI anakaza macho kule mbali, akitazama nchi pana na tambarare yenye mchanga. Anatazama kwa makini, kisha anafungua macho kwa mshangao. Haamini anachoona. Anaona dhoruba ikija kwa mbali. Lakini si dhoruba ya kawaida. Upepo mkali kutoka kaskazini unapuliza nywele zake na nguo zake, anaona wingu zito na kubwa. Wingu hilo lina mwangaza wa moto unaomulika, na mwanga wake unamkumbusha chuma cha thamani kilichoyeyushwa. * Wingu hilo linapozidi kumkaribia Ezekieli, anasikia sauti inayozidi kuongezeka—ikinguruma kama jeshi kubwa lililo mwendoni.​—Eze. 1:4, 24.

2 Akiwa na umri wa karibu miaka 30, mwanamume huyo kijana anaona jambo la kwanza kati ya mfululizo wa mambo mengi yasiyosahaulika. Anahisi “mkono wa Yehova” ukiwa juu yake, yaani, nguvu zisizozuilika za roho takatifu ya Yehova. Roho hiyo itamsaidia kuona na kusikia mambo ya pekee sana, na yanayostaajabisha kuliko sinema yoyote iliyotengenezwa na watengeneza filamu wa leo. Maono ambayo Ezekieli anaona yanamfanya aanguke kifudifudi akiwa amelemewa kabisa.​—Eze. 1:3, 28.

3 Hata hivyo, kusudi la Yehova si kumstaajabisha tu Ezekieli. Maono ya kwanza ya Ezekieli—kama maono mengine yaliyoandikwa katika kitabu hicho cha kinabii chenye kusisimua—yana maana kubwa, kwake na kwa watumishi waaminifu wa Yehova leo. Basi, acheni tuchunguze kwa undani mambo ambayo Ezekieli anaona na kusikia.

Muktadha

4, 5. Ezekieli alipata maono hayo akiwa wapi?

4 Soma Ezekieli 1:1-3. Kwanza, acheni tujikumbushe muktadha. Ulikuwa mwaka wa 613 K.W.K. Kama tulivyojifunza katika sura iliyotangulia, Ezekieli alikuwa Babiloni, akiishi na wahamishwa wenzake kando ya mto Kebari—inaonekana ni mfereji au mto ambao vyombo vya majini vingeweza kupita uliochimbwa kutoka kwenye mto Efrati na kisha kuungana tena na mto huo.

Ezekieli aliishi pamoja na wahamishwa wenzake karibu na mto Kebari (Tazama fungu la 4)

5 Yerusalemu, jiji la nyumbani la wahamishwa hao, lilikuwa umbali wa kilomita 800 hivi. * Hekalu ambalo baba ya Ezekieli alitumikia akiwa kuhani lilikuwa limezama katika upotovu na ibada ya sanamu. Kiti cha ufalme kilichokuwa Yerusalemu, ambapo Daudi na Sulemani walikalia kwa utukufu, sasa kilidharaulika. Yehoyakini, mfalme asiye na imani alikuwa huko Babiloni pamoja na wahamishwa. Sedekia, mfalme aliyetawala baada yake, alikuwa kibaraka tu na mtu mwovu.​—2 Fal. 24:8-12, 17, 19.

6, 7. Kwa nini huenda Ezekieli alihisi kwamba aliishi wakati wenye kukatisha tamaa?

6 Kwa mtu mwenye imani kama Ezekieli, lazima huo ulikuwa wakati mgumu sana maishani mwake. Huenda baadhi ya wahamishwa wenzake walijiuliza: ‘Je, Yehova ametuacha milele? Je, utawala mwovu wa Babiloni na miungu yake mingi ya uwongo utakomesha kabisa ibada safi na kuondoa utawala wa Yehova duniani?’

7 Ukiwa na habari hizo akilini, kwa nini usianze funzo lako la kibinafsi kuhusu habari hii kwa kusoma ufafanuzi wa maono ya kwanza ya Ezekieli? (Eze. 1:4-28) Unapofanya hivyo, jaribu kujiwazia ukiwa katika hali ya Ezekieli, ukiona mambo aliyoona na kusikia mambo aliyosikia.

Mto Efrati katika eneo lililo karibu na Karkemishi (Tazama fungu la 5 hadi 7)

Gari la Kustaajabisha

8. Ezekieli aliona nini katika maono, na mambo aliyoona yanawakilisha nini?

8 Ezekieli aliona nini kwa ujumla? Aliona gari kubwa lenye kustaajabisha. Lilikuwa na magurudumu manne makubwa na viumbe wanne wa kiroho wasio wa kawaida, ambao baadaye wanatajwa kuwa makerubi. (Eze. 10:1) Juu yao kulikuwa na jukwaa kubwa au anga lililo kama barafu, na juu ya anga hilo kulikuwa na kiti chenye utukufu cha ufalme cha Mungu, na Yehova akiwa amekaa juu yake! Hata hivyo, gari hilo lilimaanisha nini? Kwa kweli, maono ya Ezekieli yanamaanisha jambo moja tu: sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova lenye utukufu la ulimwengu mzima. Kwa nini tunasema hivyo? Hebu tuchunguze sababu tatu zinazofanya tuamini hivyo.

9. Uhusiano kati ya Yehova na viumbe wake wa mbinguni unafananaje na gari?

9 Uhusiano wa Yehova na viumbe wake wa mbinguni. Kumbuka kwamba katika maono haya, kiti cha ufalme cha Yehova kimewekwa juu ya makerubi. Katika sehemu nyingine za Neno la Mungu, Yehova anafafanuliwa au kuonyeshwa akiwa ameketi juu au katikati ya makerubi wake. (Soma 2 Wafalme 19:15; Kut. 25:22; Zab. 80:1) Kama vile ambavyo hahitaji kuendesha gari halisi, bila shaka, haketi kihalisi juu ya makerubi wake​—kana kwamba anahitaji kubebwa na viumbe hao wa roho wenye nguvu. Lakini makerubi wanaunga mkono enzi yake kuu, naye anaweza kuwatuma mahali popote ulimwenguni kutimiza mapenzi ya enzi yake kuu. Kama ilivyo kwa malaika wote watakatifu wa Mungu, wao pia wanatekeleza maamuzi ya Yehova wakiwa wahudumu au wawakilishi wake. (Zab. 104:4) Kwa hiyo, Yehova ‘anawaongoza’ wote, akiwaelekeza akiwa mtawala wao, kana kwamba ni gari moja kubwa lililounganishwa.

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba ni zaidi ya makerubi wanne wanaohusika katika gari la kimbingu?

10 Gari hilo haliwakilishi makerubi peke yao. Makerubi ambao Ezekieli aliona walikuwa wanne. Mara nyingi namba hiyo hutumiwa katika Biblia kumaanisha usawa au ukamili—​inahusisha ulimwengu mzima. Hivyo, inaonekana kwamba makerubi hao wanne wanawakilisha wana wote wa kiroho wa Yehova walio washikamanifu. Pia, kumbuka kwamba magurudumu na makerubi wamejaa macho, kuonyesha kwamba zaidi ya viumbe hao wanne, kuna viumbe wengine wengi wa kiroho ambao wako macho. Ufafanuzi wa Ezekieli unaonyesha kwamba gari hilo ni kubwa, hivi kwamba makerubi hao wenye kuvutia wanaonekana kuwa wadogo. (Eze. 1:18, 22; 10:12) Vivyo hivyo, sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova ni kubwa sana, inahusisha mengi zaidi ya wale makerubi wanne.

Ezekieli alistaajabishwa na maono aliyoona ya gari la kimbingu la Yehova (Tazama fungu la 8-10)

11. Danieli alipata maono gani yanayofanana na ya Ezekieli, na yanatusaidia kufikia mkataa gani?

11 Danieli pia aliona maono kama hayo ya mbinguni. Nabii Danieli aliishi miaka mingi uhamishoni katika jiji la Babiloni, yeye pia alipokea maono ya mbinguni. Jambo la kupendeza ni kwamba katika maono hayo pia, kiti cha ufalme cha Yehova kilikuwa na magurudumu. Maono ya Danieli yalikazia ukubwa wa familia ya kiroho ya Yehova huko mbinguni. Danieli aliona “elfu kwa maelfu . . . na elfu kumi mara elfu kumi” ya wana wa kiroho wa Mungu wakiwa wamesimama mbele za Yehova. Waliketi wakiwa Mahakama ya kimbingu, bila shaka kila mmoja mahali pake. (Dan. 7:9, 10, 13-18) Basi ni sawa kukata shauri kwamba maono ya Ezekieli yanawakilisha mkusanyiko huo mtakatifu wa viumbe wa roho, sivyo?

12. Kujifunza kuhusu maono ya Ezekieli ya gari la kimbingu kunatulinda jinsi gani?

12 Yehova anajua kwamba ni ulinzi kwa wanadamu kukazia fikira mambo halisi ya kiroho​—“vitu visivyoonekana,” kama mtume Paulo anavyosema. Kwa nini? Tukiwa viumbe wa nyama na damu, tunakazia sana “vitu vinavyoonekana,” mahitaji yetu ya kimwili, ambayo ni ya muda mfupi tu. (Soma 2 Wakorintho 4:18.) Mara nyingi Shetani anatumia hali hiyo na kutuchochea tufikirie zaidi vitu vya kimwili. Ili tuweze kupinga mwelekeo huo, kwa upendo Yehova anatuandalia ujumbe kama huu wa unabii wa Ezekieli, akitupatia vikumbusho vyenye kusisimua kuhusu ukuu wenye kustaajabisha wa familia ya Yehova ya mbinguni!

“Magurudumu Yanayozunguka!”

13, 14. (a) Ezekieli alifafanuaje magurudumu aliyoona? (b) Kwa nini gari la Yehova lina magurudumu?

13 Mwanzoni, Ezekieli aliwakazia fikira makerubi wanne, na katika Sura ya 4 ya kitabu hiki, tutaona mambo tunayojifunza kumhusu Yehova kutokana na viumbe hao na mwonekano wao wenye kushangaza. Hata hivyo, Ezekieli aliona magurudumu manne kando ya makerubi hao, na bila shaka yalikuwa katika pembe nne, na kufanyiza umbo kubwa la mraba. (Soma Ezekieli 1:16-18.) Yalionekana kama yalitengenezwa kwa krisolito, jiwe la thamani jangavu lenye rangi ya manjano au manjano iliyochanganyika na kijani. Kitu hicho maridadi kiling’aa.

14 Maono ya Ezekieli yalikazia sana magurudumu ya gari. Aliona jambo ambalo si la kawaida. Kiti cha ufalme chenye magurudumu! Huenda tukawazia kiti cha ufalme kikiwa kimewekwa sehemu moja tu na kwa kawaida hivyo ndivyo ilivyo, kwa kuwa eneo la watawala wa dunia lina mipaka. Lakini enzi kuu ya Yehova ni tofauti kabisa na utawala wowote wa mwanadamu. Kama Ezekieli alivyoona, mamlaka ya enzi kuu ya Yehova haina mipaka. (Neh. 9:6) Kihalisi, Mwenye Enzi Kuu anaweza kutumia mamlaka yake mahali popote!

15. Magurudumu ambayo Ezekieli aliona yalikuwa na ukubwa na muundo gani?

15 Ezekieli alishangazwa na ukubwa wa magurudumu hayo. Aliandika hivi: “Mizingo yake ilikuwa juu sana hivi kwamba iliogopesha.” Tunaweza kuwazia Ezekieli akiinua kichwa chake kuangalia mizingo hiyo mikubwa inayong’aa na jinsi ilivyonyooka kuelekea mbinguni. Naye aliongezea maelezo haya yenye kustaajabisha: “Mizingo ya magurudumu yote manne ilikuwa imejaa macho kuizunguka.” Labda jambo la kushangaza zaidi lilikuwa umbo lisilo la kawaida la magurudumu hayo. Alieleza hivi: “Mwonekano wake na muundo wake ni kama gurudumu lililokuwa ndani ya gurudumu.” Hilo lilimaanisha nini?

16, 17. (a) Gari hilo lilikuwaje na magurudumu yaliyokuwa ndani ya magurudumu? (b) Magurudumu hayo yanaonyesha nini kuhusu uwezo wa kusonga wa gari la Yehova?

16 Inaonekana kila gurudumu aliloona Ezekieli, lilikuwa na magurudumu mawili yaliyounganishwa, kila gurudumu liliunganishwa na gurudumu lingine kwenye mhimili mmoja katika pembe mraba. Jambo hilo linaonyesha kwa nini magurudumu hayo yalienda kama Ezekieli alivyoeleza: “Yaliposonga, yangeweza kwenda upande wowote kati ya zile pande nne bila kugeuka yalipokuwa yakienda.” Magurudumu hayo yanaonyesha nini kuhusu gari la kimbingu ambalo Ezekieli aliona?

17 Magurudumu yenye kimo kirefu hivyo yangeweza kukanyaga eneo kubwa sana hata kwa mzunguko mmoja tu. Kwa kweli, maono hayo yanaonyesha kwamba gari hilo lilisonga kwa mwendo kama radi! (Eze. 1:14) Zaidi ya hayo, wahandisi hawawezi kutengeneza magurudumu yenye uwezo kama huo wa kwenda pande zote nne. Gari hilo linaweza kwenda upande wowote bila kugeuka wala kupunguza mwendo! Hata hivyo, halifanyi hivyo bila kuona. Ni wazi kwamba macho yaliyojaa kuzunguka mizingo ya magurudumu yanaonyesha kwamba gari hilo linaona kila kitu pande zote.

Magurudumu yalikuwa na ukubwa wa ajabu, na yalisonga kwa kasi sana (Tazama fungu la 17)

18. Tunajifunza nini kutokana na ukubwa wa magurudumu na macho yaliyojaa kwenye magurudumu hayo?

18 Sasa, Yehova alikuwa akimfundisha nini Ezekieli—na watu wote waaminifu—kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo Lake? Fikiria mambo ambayo tayari tumechunguza. Ni lenye utukufu na lenye kuogopesha, kama mng’ao wa magurudumu na ukubwa wake unavyoonyesha. Linaona kila kitu, kama inavyoonyeshwa na wingi wa macho kwenye magurudumu. Macho ya Yehova yanaona kila kitu. (Met. 15:3; Yer. 23:24) Pia, ana mamilioni ya watumishi wake wa kimalaika ambao anaweza kuwatuma sehemu yoyote ya ulimwengu mzima, nao wanaweza kuchunguza mambo kwa makini na kurudisha ripoti kwa mtawala wao Mwenye Enzi Kuu.​—Soma Waebrania 1:13, 14.

Muundo wa magurudumu unaonyesha uwezo wa kusonga kwa ukamilifu (Tazama fungu la 17 na 19)

19. Tunajifunza nini kumhusu Yehova na sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake kutokana na kasi ya gari la kimbingu na uwezo wake wa kubadili mwelekeo?

19 Zaidi ya hayo, tunaona kwamba gari linasonga kwa kasi sana kuelekea upande wowote. Hebu wazia tofauti iliyopo kati ya sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova na taasisi, mashirika, na serikali za wanadamu! Haziwezi kuona mambo yajayo, na hivyo hazifanyi mabadiliko hadi zinapopatwa na matatizo au kupitwa na wakati. Lakini gari la Yehova linafunua kikamilifu usawaziko wa Mungu anayeliendesha, ambaye hubadilika kulingana na hali. Kama tu jina lake linavyomaanisha, anaweza kuwa kitu chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. (Kut. 3:13, 14) Kwa mfano, anaweza kubadilika haraka na kuwa Shujaa anayewapigania watu wake, lakini ghafla anaweza kubadilika tena na kuwa mwenye rehema na kusamehe dhambi, akiwasaidia na kuwaimarisha hata watenda dhambi wanaotubu waliovunjika moyo kabisa.​—Zab. 30:5; Isa. 66:13.

20. Kwa nini tunapaswa kustaajabishwa na gari la Yehova?

20 Kufikia hapa, maono ya Ezekieli yanaweza kutuchochea tujiulize, ‘Je, kweli ninastaajabishwa na gari la Yehova?’ Tunapaswa kukumbuka kwamba gari hilo linasonga. Tusifikiri kamwe kwamba Yehova na Mwana wake, na malaika wote hawaoni baadhi ya matatizo yanayotuvunja moyo. Wala hatupaswi kuhofu kwamba Mungu wetu atakawia kututimizia mahitaji yetu au kwamba tengenezo lake litashindwa kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu usiotegemeka. Tunapaswa kukumbuka kwamba tengenezo la Yehova linatenda, sikuzote linasonga. Hata Ezekieli alisikia sauti kutoka mbinguni ikisema hivi “Magurudumu yanayozunguka!”—inaonekana magurudumu yalikuwa yakiamriwa yaanze kusonga. (Eze. 10:13) Je, hustaajabu unapotafakari jinsi Yehova anavyoliendesha tengenezo lake? Hata hivyo, Yehova ndiye tunayepaswa kumstaajabia zaidi.

Yule Anayeliendesha

21, 22. Ni nini kinachounganisha sehemu mbalimbali za gari hilo?

21 Ezekieli aliacha kukazia fikira magurudumu akaangalia juu, ambako aliona “mfano wa anga lililometameta kama barafu inayotisha.” (Eze. 1:22) Juu ya vichwa vya makerubi, anga hilo lilitanda, likimetameta katika mng’ao wa utukufu. Mpaka hapo, msomaji anayejua jinsi mashine zinavyofanya kazi lazima ajiulize maswali mengi kuhusu gari hilo. Kwa mfano, wengine wanaweza kujiuliza: ‘Ni nini kinachoshikilia jukwaa lililo juu ya magurudumu? Na magurudumu yanawezaje kufanya kazi bila kuunganishwa?’ Kumbuka kwamba gari hili haliathiriwi na sheria za asili, kwa sababu ni mfano, picha halisi ya makao ya kiroho. Kumbuka pia maneno haya muhimu: “Roho iliyokuwa ikitenda katika wale viumbe hai ilikuwa pia katika yale magurudumu.” (Eze. 1:20, 21) Ni roho gani iliyokuwa ikitenda katika wale makerubi na magurudumu hayo?

22 Bila shaka, ilikuwa roho takatifu ya Yehova, nguvu kuu zaidi katika ulimwengu wote mzima. Nguvu hiyo ya utendaji inaliunganisha gari hilo pamoja, inalipatia nguvu, na kuliongoza kikamili kwa mwendo wenye upatano. Tukiwa na hilo akilini, acheni tufuatane na Ezekieli anapomtazama Yule anayeliendesha gari hilo.

Ilikuwa vigumu kwa Ezekieli kufafanua maono yenye kustaajabisha

23. Ezekieli anatumia maneno gani kujaribu kumfafanua Yehova na kwa nini?

23 Soma Ezekieli 1:26-28. Katika maelezo yake yote kuhusu maono, mara nyingi Ezekieli anatumia maneno kama vile “-onekana,” “-onekana kama,” “-fanana,” na “kitu kama.” Hata hivyo, katika mistari hii, anayatumia mara nyingi zaidi. Inaonekana maono hayo yalikuwa ya kustaajabisha sana hivi kwamba ilikuwa vigumu kwake kuyafafanua. Aliona “kitu kilichoonekana kama jiwe la yakuti, na kilifanana na kiti cha ufalme.” Hebu wazia kiti cha ufalme kilichotengenezwa kutokana na jiwe kubwa la yakuti la rangi ya bluu? Na aliyeketi juu yake alikuwa mtu Mkuu. ‘Mwonekano wake ulikuwa kama mwanadamu.’

24, 25. (a) Upinde wa mvua unaozunguka kiti cha ufalme cha Yehova unatukumbusha nini? (b) Maono kama hayo yanawachocheaje watu wenye imani?

24 Kwa ujumla aliona umbo lenye utukufu, kwa kuwa Yehova alitoa mwangaza wa utukufu kuanzia kiunoni kushuka chini na kuanzia kiunoni kwenda juu. Tunaweza kuwazia jinsi nabii huyo alivyohitaji kuyakinga macho yake alipokuwa akitazama utukufu huo. Mwishowe, Ezekieli aliona jambo la ajabu: “Kulikuwa na mwangaza mkali kumzunguka pande zote kama wa upinde wa mvua katika mawingu siku ya mvua.” Je, umewahi kusisimka ulipoona upinde wa mvua? Hilo ni jambo zuri sana linalotukumbusha utukufu wa Muumba wetu! Upinde huo maridadi wa angani pia unatukumbusha kuhusu agano la Yehova la amani baada ya Gharika. (Mwa. 9:11-16) Ingawa ni mwenye nguvu sana, Mungu Mweza Yote ni mwenye amani. (Ebr. 13:20) Amani inatawala katika moyo wake na kusambaa kwa wote wanaomwabudu kwa uaminifu.

Upinde wa mvua wenye utukufu unaozunguka kiti cha ufalme cha Yehova unatukumbusha kwamba tunamtumikia Mungu mwenye amani (Tazama fungu la 24)

25 Ezekieli alitendaje baada ya kuona utukufu wa Yehova Mungu? Aliandika jambo lililotokea: “Nilipouona, nikaanguka chini kifudifudi.” Akiwa amelemewa na hofu na kumwogopa Mungu, Ezekieli alianguka chini. Manabii wengine walifanya vivyo hivyo walipopata maono kutoka kwa Yehova; jambo hilo ni lenye kunyenyekeza, hata kuogopesha. (Isa. 6:1-5; Dan. 10:8, 9; Ufu. 1:12-17) Hata hivyo, wanaume hao waliimarishwa sana na mambo ambayo Yehova aliwafunulia. Ezekieli aliimarishwa sana. Kwa hiyo, masimulizi kama hayo ya Biblia yanapaswa kutuchocheaje tunapoyasoma?

26. Ezekieli aliimarishwaje na maono hayo?

26 Ikiwa Ezekieli alikuwa na shaka au maoni yasiyofaa kuhusiana na hali ya watu wa Mungu huko Babiloni, lazima aliimarishwa na maono hayo. Kwa kweli, watu waaminifu wa Mungu wangeweza kufikiwa na gari kubwa la Yehova mahali popote walipokuwa. Iwe ni Yerusalemu, Babiloni, au kwingineko! Ni nguvu gani ya Shetani ambayo inaweza kushindana na Mungu ambaye analiongoza tengenezo hilo la kimbingu lenye utukufu? (Soma Zaburi 118:6.) Pia, Ezekieli aliona kwamba gari la kimbingu halikuwa mbali na wanadamu. Naam, magurudumu yake yalifika duniani! (Eze. 1:19) Hivyo, Yehova alipendezwa sana na watu wake waaminifu waliokuwa uhamishoni. Sikuzote wangekuwa chini ya utunzaji wenye upendo wa Baba yao!

Jinsi Gari Hilo Linavyokuhusu

27. Maono ya Ezekieli yana maana gani kwetu leo?

27 Je, maono ya Ezekieli yana maana kwetu leo? Bila shaka! Kumbuka kwamba Shetani anapanga mashambulizi makubwa zaidi dhidi ya ibada safi ya Yehova. Angependa kufanya tufikiri kwamba tuko peke yetu, tumetengwa, na kwamba Baba yetu wa mbinguni na tengenezo lake wako mbali nasi. Usiruhusu kamwe akili na moyo wako udanganywe na uwongo huo! (Zab. 139:7-12) Kama Ezekieli, tuna kila sababu ya kujawa na hofu. Huenda tusianguke kifudifudi kama alivyofanya. Je, hatustaajabishwi na nguvu, mwendo, uwezo wa kusonga, kubadilikana, na utukufu wa sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova la ulimwengu wote mzima?

28, 29. Ni nini kinachoonyesha kwamba gari la Yehova limekuwa likisonga katika karne iliyopita?

28 Pia, kumbuka kwamba tengenezo la Yehova lina sehemu ya kidunia. Hata hivyo, sehemu ya kidunia inafanyizwa na wanadamu wasio wakamilifu. Lakini fikiria mambo ambayo Yehova ametimiza hapa duniani! Ulimwenguni kote Yehova amewasaidia wanadamu wa kawaida kufanya mambo ambayo hawangeweza kufanya kwa uwezo wao wenyewe. (Yoh. 14:12) Unapochunguza kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala! utaona jinsi kazi kubwa ya kuhubiri ilivyofanywa kwa kasi katika karne iliyopita. Tunaweza pia kufikiria mambo ambayo tengenezo la Yehova limefanya katika kuwaelimisha Wakristo wa kweli, kushinda kesi mahakamani, na hata kutumia teknolojia ya karibuni ili kutimiza mapenzi ya Mungu!

29 Tunapochunguza mambo yote ambayo yamefanywa ili kurudisha ibada safi katika kipindi hiki cha siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo, ni wazi kwamba gari la Yehova linasonga. Tuna pendeleo kubwa sana la kushirikiana na tengenezo hilo na kumtumikia Mwenye Enzi Kuu!​—Zab. 84:10.

Sikuzote, sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova inasonga (Tazama fungu la 28 na 29)

30. Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

30 Hata hivyo, tunajifunza mengi zaidi kutokana na maono ya Ezekieli. Katika sura inayofuata, tutawachunguza kwa undani wale ‘viumbe hai’ au makerubi. Wanatufundisha nini kumhusu Mungu wetu Mwenye Enzi Kuu, Yehova?

^ fu. 1 Ezekieli alitaja kihususa mchanganyiko wa dhahabu na fedha.

^ fu. 5 Huo ni umbali wa njia ya moja kwa moja, lakini inawezekana kwamba watu waliohamishwa walipitia njia iliyokuwa ndefu mara mbili ya umbali huo.