Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 7

Mataifa Yatalazimika “Kujua Kwamba Mimi Ni Yehova”

Mataifa Yatalazimika “Kujua Kwamba Mimi Ni Yehova”

EZEKIELI 25:17

WAZO KUU: Mambo tunayojifunza kutokana na uhusiano wa Israeli na mataifa yaliyolichafua jina la Yehova

1, 2. (a) Taifa la Israeli lilikuwaje kama kondoo aliyezungukwa na kundi la mbwamwitu? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.) (b) Waisraeli na wafalme wao waliruhusu jambo gani liwapate?

KWA mamia ya miaka, taifa la Israeli lilikuwa kama kondoo aliyezungukwa na kundi la mbwamwitu. Waamoni, Wamoabu, na Waedomu, walikuwa tishio kwenye mpaka wa mashariki wa Israeli. Wafilisti wenye nguvu sana na maadui wa muda mrefu wa Israeli, walikuwa upande wa magharibi. Jiji la Tiro lenye utajiri mwingi lililokuwa kitovu cha milki kubwa ya kibiashara, lilikuwa upande wa kaskazini. Upande wa kusini kulikuwa na taifa la kale la Misri, lililotawaliwa na Farao ambaye alionwa kuwa mungu.

2 Waisraeli walipomtegemea Yehova, aliwalinda kutokana na maadui wao. Hata hivyo, watu wake pamoja na wafalme wao waliruhusu mataifa yaliyowazunguka yawapotoshe tena na tena. Kwa mfano, Mfalme Ahabu ni mojawapo ya watawala waliopotoshwa. Aliishi kipindi kimoja na Mfalme Yehoshafati wa Yuda, naye alitawala ufalme wa Israeli wenye makabila kumi. Alimwoa binti ya mfalme wa Sidoni aliyetawala jiji lenye ufanisi la Tiro. Mwanamke huyo aliyeitwa Yezebeli, aliendeleza sana ibada ya Baali katika Israeli na akamshawishi mume wake aichafue ibada safi kwa kiwango kikubwa sana.—1 Fal. 16:30-33; 18:4, 19.

3, 4. (a) Sasa Ezekieli anakazia nani fikira? (b) Tutazungumzia maswali gani?

3 Yehova alikuwa amewaonya watu wake kuhusu matokeo mabaya ya kutokuwa washikamanifu kwake. Sasa subira yake ilikuwa imefikia mwisho. (Yer. 21:7, 10; Eze. 5:7-9) Mwaka wa 609 K.W.K., jeshi la Babiloni lilirudi katika Nchi ya Ahadi kwa mara ya tatu. Miaka kumi ilikuwa imepita tangu walipovamia nchi hiyo. Wakati huu walibomoa kuta za Yerusalemu na kuwaangamiza wale waliomwasi Nebukadneza. Jiji hilo lilipoanza kuzingirwa, na unabii wa Ezekieli ulioongozwa na roho ulipotimizwa kikamili, nabii huyo alikazia fikira mambo ambayo yangeyapata mataifa yaliyozunguka Nchi ya Ahadi.

Mataifa yaliyolichafua jina la Yehova hayangeepuka matokeo mabaya ya matendo yao

4 Yehova alimfunulia Ezekieli kwamba maadui wa Yuda wangeshangilia uharibifu wa Yerusalemu na wangewatesa watu walioponyoka. Hata hivyo, mataifa yaliyolichafua jina la Yehova na kuwatesa au kuwapotosha watu wake, hayangeepuka matokeo mabaya ya matendo yao. Tunajifunza mambo gani kutokana na uhusiano wa Israeli na mataifa hayo? Na unabii wa Ezekieli kuhusu mataifa hayo unatupatia tumaini gani leo?

Watu wa Ukoo Waliowatendea Waisraeli kwa “Dharau Kubwa”

5, 6. Waamoni na Waisraeli walikuwa na uhusiano gani?

5 Kwa njia fulani, Waamoni, Wamoabu, na Waedomu walikuwa na ukoo mmoja na Israeli. Licha ya kuwa na ukoo mmoja na historia moja, mataifa hayo yaliwachukia watu wa Mungu kwa muda mrefu na kuwatendea kwa “dharau kubwa.”—Eze. 25:6.

6 Fikiria Waamoni. Walikuwa wazao wa mpwa wa Abrahamu, Loti, kupitia binti yake mdogo. (Mwa. 19:38) Lugha yao ilifanana sana na Kiebrania na inaelekea watu wa Mungu waliielewa. Kwa sababu ya uhusiano huo wa kifamilia, Yehova aliwaambia Waisraeli wasianzishe vita dhidi ya Waamoni. (Kum. 2:19) Hata hivyo, katika siku za Waamuzi, Waamoni waliungana na Mfalme Egloni wa Moabu kuwatesa Waisraeli. (Amu. 3:12-15, 27-30) Baadaye, Sauli alipowekwa kuwa mfalme, Waamoni walishambulia Israeli. (1 Sam. 11:1-4) Katika siku za Mfalme Yehoshafati, majeshi ya Waamoni yaliungana tena na ya Moabu ili kushambulia Nchi ya Ahadi.—2 Nya. 20:1, 2.

7. Wamoabu waliwatendeaje binamu zao, wazao wa Israeli?

7 Wamoabu pia walikuwa wazao wa Loti, lakini kupitia binti yake mkubwa. (Mwa. 19:36, 37) Yehova aliwaambia Waisraeli wasipigane na Wamoabu. (Kum. 2:9) Lakini Wamoabu hawakuwa na fadhili. Badala ya kuwasaidia binamu zao waliokuwa wakitoroka utumwa huko Misri, walijaribu kuwazuia wasiingie katika Nchi ya Ahadi. Mfalme Balaki wa Moabu alimlipa Balaamu ili awalaani Waisraeli, naye Balaamu akamfundisha Balaki jinsi ya kuwashawishi wanaume Waisraeli wafanye uasherati na kuabudu sanamu. (Hes. 22:1-8; 25:1-9; Ufu. 2:14) Kwa karne nyingi Wamoabu waliendelea kuwakandamiza watu wao wa ukoo, hadi kufikia siku za Ezekieli.—2 Fal. 24:1, 2.

8. Kwa nini Yehova alisema kwamba Edomu alikuwa ndugu ya Israeli, hata hivyo Waedomu walitendaje?

8 Waedomu walikuwa wazao wa Esau, aliyekuwa ndugu pacha wa Yakobo. Uhusiano wao wa kifamilia na Israeli ulikuwa wa karibu sana hivi kwamba Yehova aliwaita Waedomu na Waisraeli ndugu. (Kum. 2:1-5; 23:7, 8) Hata hivyo, Waedomu waliwapinga Waisraeli tangu walipotoka Misri hadi Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. (Hes. 20:14, 18; Eze. 25:12) Wakati huo, Waedomu walishangilia Waisraeli walipokuwa wakiteseka, na waliwahimiza Wababiloni waliharibu Yerusalemu, isitoshe, waliwazuia Waisraeli waliokuwa wakitoroka na wakawakabidhi kwa Wababiloni.—Zab. 137:7; Oba. 11, 14.

9, 10. (a) Ni nini kilichoyapata mataifa ya Amoni, Moabu na Edomu? (b) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba si watu wote katika mataifa hayo waliokuwa maadui wa Israeli?

9 Yehova aliyahukumu mataifa hayo kwa sababu ya kuwatendea watu Wake vibaya. Alisema: ‘Nitawatoa Waamoni kuwa mali ya watu wa Mashariki, ili Waamoni wasikumbukwe kati ya mataifa.’ Pia alisema: “Nitatekeleza hukumu katika Moabu, nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 25:10, 11) Miaka mitano baada ya Yerusalemu kuharibiwa, unabii huo ulianza kutimia Wababiloni waliposhinda Amoni na Moabu. Kuhusu Edomu, Yehova alisema kwamba ‘angewaangamiza wanadamu na wanyama waliomo,’ na ‘kuifanya kuwa ukiwa.’ (Eze. 25:13) Kama ilivyotabiriwa, hatimaye mataifa ya Amoni, Moabu, na Edomu yaliangamizwa.—Yer. 9:25, 26; 48:42; 49:17, 18.

10 Hata hivyo, si watu wote katika mataifa hayo waliokuwa maadui wa watu wa Mungu. Kwa mfano, Seleki Mwamoni na Ithma Mmoabu wanatajwa kati ya mashujaa wenye nguvu wa Daudi. (1 Nya. 11:26, 39, 46; 12:1) Naye Ruthu Mmoabu alikuwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova.—Rut. 1:4, 16, 17.

Usilegeze msimamo wako hata katika mambo madogo

11. Tunajifunza nini kutokana na uhusiano wa Israeli na mataifa ya Amoni, Moabu, na Edomu?

11 Tunajifunza masomo gani kutokana na jinsi Waisraeli walivyoshughulika na mataifa hayo? Kwanza, Waisraeli walipowaruhusu watu wao wa ukoo wawashawishi, walianza kuabudu miungu kama vile Baali wa Peori wa Wamoabu na mungu wa Waamoni, Moleki. (Hes. 25:1-3; 1 Fal. 11:7) Sisi pia tunaweza kupatwa na jambo kama hilo. Watu wa ukoo wasioamini wanaweza kutushinikiza tulegeze msimamo wetu. Kwa mfano, huenda wasielewe kwa nini hatusherehekei Ista, hatupeani zawadi za Krismasi, au kushiriki katika desturi nyingine zinazopendwa na watu wengi ambazo zinahusianishwa na mafundisho ya dini ya uwongo. Hata ingawa hawana nia mbaya wanaweza kutushawishi tulegeze viwango vyetu angalau kidogo tu. Lakini ni muhimu sana tusishindwe na kishawishi hicho! Kama historia ya Israeli inavyoonyesha tukilegeza msimamo hata katika mambo madogo, uhusiano wetu na Yehova unaweza kuharibika.

12, 13. Huenda tukakabili upinzani gani, na ni nini kinachoweza kutokea tukibaki washikamanifu?

12 Tunajifunza somo lingine kutokana na uhusiano kati ya Israeli na Amoni, Moabu, na Edomu. Tunaweza kupingwa sana na watu wa familia yetu ambao si waamini. Yesu alionya kwamba nyakati nyingine, ujumbe tunaohubiri ungeleta “mgawanyiko, mtu dhidi ya baba yake, [na] binti dhidi ya mama yake.” (Mt. 10:35, 36) Yehova aliwaambia Waisraeli wasianzishe ugomvi na watu wao wa ukoo, sisi pia hatutaki kubishana na watu wa familia yetu wasioamini. Hata hivyo, hatupaswi kushangaa tunapopingwa.—2 Tim. 3:12.

13 Hata ikiwa watu wetu wa ukoo hawatupingi moja kwa moja tunapomwabudu Yehova, hatupaswi kuwaruhusu wawe na nguvu juu yetu kuliko Yehova. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anastahili kuchukua nafasi ya kwanza katika moyo wetu. (Soma Mathayo 10:37.) Isitoshe, tukiendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova, baadhi ya watu wetu wa ukoo wanaweza kuwa kama Seleki, Ithma, na Ruthu na kujiunga nasi katika ibada safi. (1 Tim. 4:16) Kisha wao pia watapata shangwe ya kumtumikia Mungu wa pekee wa kweli na kufurahia upendo na ulinzi wake.

Maadui wa Yehova Walipata “Adhabu Kali”

14, 15. Wafilisti waliwatendeaje Waisraeli?

14 Wafilisti walikuwa wametoka kisiwa cha Krete na kuhamia nchi ambayo baadaye Yehova aliahidi kumpa Abrahamu na wazao wake. Abrahamu na Isaka walishirikiana na watu hao. (Mwa. 21:29-32; 26:1) Kufikia wakati ambapo Waisraeli waliingia katika Nchi ya Ahadi, tayari Wafilisti walikuwa taifa lenye nguvu na lenye jeshi imara. Waliabudu miungu ya uwongo kama vile Baal-zebubu na Dagoni. (1 Sam. 5:1-4; 2 Fal. 1:2, 3) Wakati mwingine, Waisraeli pia waliiabudu miungu hiyo.—Amu. 10:6.

15 Kwa sababu Waisraeli walikosa kuwa washikamanifu, Yehova aliruhusu Wafilisti wawakandamize watu wake kwa miaka mingi. (Amu. 10:7, 8; Eze. 25:15) Waliwawekea Waisraeli masharti mengi * na kuwaua Waisraeli wengi. (1 Sam. 4:10) Hata hivyo, Waisraeli walipotubu na kumrudia Yehova, aliwakomboa. Aliwachagua wanaume kama vile Samsoni, Sauli, na Daudi ili wawakomboe watu Wake. (Amu. 13:5, 24; 1 Sam. 9:15-17; 18:6, 7) Na kama Ezekieli alivyotabiri, Wafilisti walipata “adhabu kali” nchi yao iliposhambuliwa na Wababiloni na baadaye Wagiriki.—Eze. 25:15-17.

16, 17. Tunajifunza masomo gani kutokana na uhusiano wa Israeli na Wafilisti?

16 Tunajifunza masomo gani kutokana na jinsi Waisraeli walivyoshughulika na Wafilisti? Leo, watu wa Yehova wamepingwa na baadhi ya mataifa yenye nguvu zaidi ambayo yamewahi kuwatawala wanadamu. Tofauti na Israeli, tumejitahidi kudumisha ushikamanifu wetu kwa Yehova. Hata hivyo, nyakati nyingine, huenda ikaonekana kwamba maadui wa ibada safi wanashinda. Kwa mfano, mwanzoni mwa karne ya 20, serikali ya Marekani ilijaribu kusimamisha kazi ya watu wa Yehova kwa kuwahukumu kifungo cha muda mrefu gerezani wale waliokuwa wakiliongoza tengenezo. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, chama cha Nazi cha Ujerumani kilijaribu kuwaangamiza watu wa Mungu, kwa kuwafunga maelfu gerezani na kuwaua mamia. Baada ya vita hivyo, Muungano wa Sovieti ulianzisha kampeni ya miaka mingi dhidi ya Mashahidi wa Yehova, kwa kuwapeleka ndugu zetu kwenye kambi za kazi ngumu au kuwahamishia maeneo ya mbali sana.

17 Huenda serikali zikaendelea kupiga marufuku kazi ya kuhubiri, kuwafunga gerezani watu wa Mungu, na hata kuwaua baadhi yetu. Je, matukio hayo yanapaswa kutufanya tushindwe na woga au kukosa imani? Hapana! Yehova atawalinda watu wake washikamanifu. (Soma Mathayo 10:28-31.) Tumeona serikali zenye nguvu na zinazokandamiza zikitoweka, lakini watu wa Yehova wameendelea kunawiri. Hivi karibuni, serikali zote za wanadamu zitapatwa na jambo lililowapata Wafilisti—zitalazimika kumjua Yehova. Na kama ilivyokuwa kwa Wafilisti, zitaangamizwa!

‘Utajiri Mwingi’ Haukuleta Ulinzi wa Kudumu

18. Tiro ilidhibiti milki ya aina gani?

18 Jiji la kale la Tiro * lilikuwa katikati ya mojawapo ya milki kuu za kibiashara za ulimwengu wa kale. Jiji hilo lilikuwa na njia nyingi za kibiashara upande wa magharibi, kuvuka Bahari ya Mediterania. Upande wa mashariki, njia za kibiashara za Tiro zilipita kwenye nchi kavu na zililiunganisha jiji hilo na milki za mbali. Kwa karne nyingi, Tiro lilijikusanyia utajiri mwingi kwa bidhaa zilizotoka maeneo hayo ya mbali. Wafanyabiashara wake walikuwa na utajiri mwingi hivi kwamba walijiona kuwa wakuu.—Isa. 23:8.

19, 20. Kuna tofauti gani kati ya wakaaji wa Tiro na wakaaji wa Gibeoni?

19 Chini ya utawala wa Mfalme Daudi na Sulemani, taifa la Israeli lilifanya biashara na wakaaji wa Tiro, ambao walileta vifaa vya ujenzi na mafundi ili kusaidia katika ujenzi wa jumba la kifalme la Daudi na baadaye hekalu la Sulemani. (2 Nya. 2:1, 3, 7-16) Tiro iliona taifa la Israeli likiwa katika hali bora kabisa. (1 Fal. 3:10-12; 10:4-9) Hebu fikiria fursa ambayo maelfu ya Watiro walikuwa nayo ya kujifunza kuhusu ibada safi, kumjua Yehova, na kujionea moja kwa moja faida za kumtumikia Mungu wa kweli!

20 Licha ya fursa hiyo, wakaaji wa Tiro waliendelea kukazia mambo ya kimwili maishani mwao. Hawakufuata mfano wa jiji la Kanaani lenye nguvu la Gibeoni, ambalo wakaaji wake walisikia tu kuhusu kazi kuu za Yehova nao wakachochewa kuwa watumishi wake. (Yos. 9:2, 3, 22–10:2) Hatimaye, wakaaji wa Tiro waliwapinga watu wa Mungu na hata kuwauza baadhi yao utumwani.—Zab. 83:2, 7; Yoe. 3:4, 6; Amo. 1:9.

Hatungependa kamwe kuviona vitu vya kimwili kuwa ukuta wa ulinzi

21, 22. Ni nini kilicholipata jiji la Tiro, na kwa nini?

21 Kupitia Ezekieli, Yehova aliwaambia hivi wapinzani hao: “Niko dhidi yako, Ee Tiro, nami nitayainua mataifa mengi dhidi yako, kama vile bahari inavyoinua mawimbi yake. Wataziharibu kuta za Tiro na kuibomoa minara yake, nami nitakwangua udongo na kumfanya awe mwamba ulio wazi, unaong’aa.” (Eze. 26:1-5) Wakaaji wa Tiro walitegemea utajiri wao na walitumaini ungewalinda, pia walihisi wakiwa salama kwa sababu kisiwa hicho kilizingirwa na kuta zenye urefu wa mita 46. Walipaswa kukazia fikira onyo hili la Sulemani: “Mali ya tajiri ni jiji lake lenye ngome; ni kama ukuta wa ulinzi katika mawazo yake.”—Met. 18:11.

22 Wababiloni na Wagiriki walipoutimiza unabii wa Ezekieli, wakaaji wa Tiro walitambua kwamba usalama uliotokana na utajiri wa jiji hilo na kuta zake, ulikuwa wa kuwaziwa tu. Baada ya kuliharibu Yerusalemu, Wababiloni walianzisha vita dhidi ya Tiro kwa miaka 13. (Eze. 29:17, 18) Kisha katika mwaka wa 332 K.W.K., Aleksanda Mkuu alitimiza sehemu muhimu ya unabii uliotolewa na Ezekieli. * Jeshi lake lilikusanya magofu ya jiji la nchi kavu la Tiro na wakatupa mawe, mbao, na mchanga huo ndani ya maji na hivyo wakatengeneza njia ya kufika kwenye jiji lililo kisiwani. (Eze. 26:4, 12) Aleksanda alitoboa kuta za jiji hilo, akalipora, akawaua maelfu ya wanajeshi na raia, na kuwauza makumi ya maelfu utumwani. Wakaaji wa Tiro walilazimika kumjua Yehova walipojifunza kwamba ‘utajiri mwingi’ si ulinzi wa kudumu.—Eze. 27:33, 34.

Ingawa jiji la Tiro lilionekana kuwa salama kabisa, liliangamizwa, kama Ezekieli alivyokuwa ametabiri (Tazama fungu la 22)

23. Tunajifunza somo gani kutokana na wakaaji wa Tiro?

23 Tunajifunza somo gani kutokana na wakaaji wa Tiro? Hatungependa kamwe kuruhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri” zitufanye tutegemee vitu vya kimwili na kuviona kuwa ukuta wa ulinzi. (Mt. 13:22) Hatuwezi “kutumikia Mungu na Utajiri.” (Soma Mathayo 6:24.) Wale tu wanaomtumikia Yehova kwa moyo wote ndio walio na usalama wa kweli. (Mt. 6:31-33; Yoh. 10:27-29) Unabii kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo utatimizwa kikamili kama tu unabii kuhusu Tiro ulivyotimizwa. Wakati huo, wale wanaotegemea utajiri watalazimika kumjua Yehova atakapoharibu mfumo wa kibiashara wa ulimwengu huu uliojaa pupa na ubinafsi.

Serikali Iliyokuwa Kama “Utete”

24-26. (a) Kwa nini Yehova aliliita taifa la Misri “utete”? (b) Mfalme Sedekia alipuuzaje maagizo ya Yehova, naye alipata matokeo gani?

24 Kabla ya siku za Yosefu hadi Wababiloni waliposhambulia Yerusalemu, taifa la Misri lilikuwa na uvutano mkubwa wa kisiasa katika eneo la Nchi ya Ahadi. Kwa sababu taifa la Misri lilikuwepo kwa muda mrefu, lilionekana kuwa imara, kama mti mkubwa wa muda mrefu. Lakini taifa hilo lilipolinganishwa na Yehova, lilikuwa dhaifu—kama “utete” tu.—Eze. 29:6.

25 Sedekia, mfalme aliyeasi, hakutambua jambo hilo kuhusu Misri. Kupitia nabii Yeremia, Yehova alimhimiza Sedekia ajitiishe kwa mfalme wa Babiloni. (Yer. 27:12) Sedekia hata aliapa katika jina la Yehova kwamba hatamwasi Nebukadneza. Hata hivyo, alipuuza maagizo ya Yehova, akavunja kiapo chake kwa Nebukadneza, na akaomba Misri imsaidie kupigana na Wababiloni. (2 Nya. 36:13; Eze. 17:12-20) Hata hivyo, Waisraeli waliotegemea nguvu za kisiasa za Misri walijiumiza kwa njia kubwa. (Eze. 29:7) Huenda Misri ilionekana kuwa yenye nguvu kama “mnyama mkubwa sana wa baharini.” (Eze. 29:3, 4) Lakini Yehova alisema atamshughulikia kama wawindaji wanavyowakamata mamba wa Mto Nile—angemtia kulabu katika mataya yake na kumvuta aangamizwe. Alifanya hivyo alipowatuma Wababiloni wakalishambulie taifa hilo la kale.—Eze. 29:9-12, 19.

26 Ni nini kilichompata Sedekia aliyekosa uaminifu? Kwa sababu alimwasi Yehova, Ezekieli alitabiri kwamba ‘mkuu huyo mwovu’ angepoteza taji lake na utawala wake ungeharibiwa. Hata hivyo, Ezekieli alitangaza pia ujumbe wa tumaini. (Eze. 21:25-27) Yehova alimwongoza Ezekieli kutabiri kwamba kungetokea mfalme katika ukoo wa kifalme ambaye angekuwa na “haki ya kisheria,” naye angerithi kiti cha ufalme. Katika sura inayofuata ya kitabu hiki tutaona mfalme huyo alikuwa nani.

27. Tunajifunza somo gani kutokana na uhusiano wa Israeli na Misri?

27 Tunajifunza somo gani kutokana na uhusiano wa Israeli na Misri? Leo, watu wa Yehova wanapaswa kuepuka kutegemea serikali za wanadamu wakifikiri kwamba zitawaletea usalama wa kudumu. Hata katika mawazo yetu, hatupaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 15:19; Yak. 4:4) Huenda mfumo wa kisiasa ukaonekana kuwa imara, lakini kama taifa la kale la Misri, mfumo huo ni dhaifu kama utete. Kwa kweli si jambo la hekima kuwategemea wanadamu ambao hufa, badala yake tunapaswa kumtegemea Mungu Mweza-Yote, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote!—Soma Zaburi 146:3-6.

Hata faraghani, tunapaswa kuepuka kuunga mkono upande fulani katika siasa za ulimwengu huu (Tazama fungu la 27)

Mataifa Yatalazimika “Kujua”

28-30. Kuna tofauti gani kati ya jinsi mataifa yatakavyolazimika “kumjua” Yehova na jinsi sisi tunavyomjua Yehova?

28 Katika kitabu cha Ezekieli, Yehova amesema mara nyingi mataifa yatalazimika “kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Eze. 25:17) Nyakati za kale, maneno hayo yalitimia Yehova alipotekeleza hukumu dhidi ya maadui wa watu wake. Lakini yatatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu. Yatatimizwaje?

29 Kama ilivyokuwa kwa watu wa Mungu nyakati za kale, tumezungukwa na mataifa ambayo yanatuona kama kondoo aliye peke yake ambaye hana ulinzi. (Eze. 38:10-13) Kama tutakavyoona katika Sura ya 17 na 18 ya kitabu hiki, hivi karibuni mataifa yatawashambulia vikali watu wa Mungu. Lakini watakapofanya hivyo, watamjua yule aliye na nguvu zote. Watalazimika kumjua Yehova—kutambua enzi yake kuu—atakapowaangamiza katika vita vya Har–Magedoni.—Ufu. 16:16; 19:17-21.

30 Hata hivyo, Yehova atatulinda na kutubariki. Kwa nini? Kwa sababu tumetumia fursa tuliyo nayo sasa kuthibitisha kwamba tunamjua Yehova kwa kumtegemea, kwa kumtii, na kwa kumpa ibada safi ambayo anastahili.—Soma Ezekieli 28:26.

^ fu. 15 Kwa mfano, Wafilisti hawakumruhusu mtu yeyote afanye kazi ya kufua vyuma katika Israeli. Waisraeli walilazimika kwenda kwa Wafilisti kunoa vifaa vyao vya kilimo na malipo waliyotozwa kwa kazi hiyo yalikuwa sawa na mshahara wa siku kadhaa.—1 Sam. 13:19-22.

^ fu. 18 Inaelekea mwanzoni jiji la Tiro lilijengwa kwenye mwamba uliokuwa baharini ambao haukuwa mbali sana na ufuo, karibu kilomita 50 mashariki ya Mlima Karmeli. Baadaye, jiji hilo lilipanuliwa kwa kujengwa kwenye nchi kavu. Jina la Kisemiti la jiji hilo, Sur, linamaanisha “Mwamba.”

^ fu. 22 Isaya, Yeremia, Yoeli, Amosi, na Zekaria pia walitoa unabii kuhusu Tiro, na unabii huo ulitimizwa kikamili.—Isa. 23:1-8; Yer. 25:15, 22, 27; Yoe. 3:4; Amo. 1:10; Zek. 9:3, 4.