Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

“Nitamweka Mchungaji Mmoja”

“Nitamweka Mchungaji Mmoja”

EZEKIELI 34:23

WAZO KUU: Kristo atimiza unabii mbalimbali kumhusu Masihi

1-3. Kwa nini moyo wa Ezekieli umelemewa, na sasa anaongozwa kuandika nini?

NI MWAKA wa sita tangu Ezekieli alipopelekwa uhamishoni. * Moyo wa nabii huyo umelemewa anapotafakari hali yenye kusikitisha ya utawala huko Yuda, nchi alikozaliwa iliyo umbali wa mamia ya kilomita. Amejionea watawala kadhaa wakitawala na kuondoka.

2 Ezekieli alizaliwa katikati ya utawala wa Mfalme Yosia aliyekuwa mwaminifu. Bila shaka, Ezekieli alifurahi sana alipojua kuhusu kampeni ambayo Yosia alikuwa amefanya ya kuharibu sanamu za kuchongwa na kurudisha ibada safi huko Yuda. (2 Nya. 34:1-8) Lakini jitihada za Yosia hazikuleta mabadiliko ya kudumu kwa sababu wafalme wengi waliotawala baada yake waliendeleza ibada ya sanamu. Haishangazi kwamba, chini ya watawala hao wabaya taifa limezama hata zaidi katika upotovu wa kiroho na kiadili. Je, kuna tumaini? Ndiyo!

3 Yehova anamwongoza nabii wake mwaminifu kuandika unabii—wa kwanza kati ya unabii mwingi—kuhusu Masihi, Mtawala na Mchungaji wa wakati ujao atakayerudisha ibada safi milele na kuwatunza kwa wororo kondoo wa Yehova. Ni vizuri tuchunguze unabii huo kwa makini kwa sababu kutimizwa kwake kunahusiana na wakati wetu ujao wa milele. Acheni sasa tuchunguze unabii mbalimbali katika kitabu cha Ezekieli kumhusu Masihi.

“Chipukizi Changa” Linakuwa “Mwerezi Mkubwa”

4. Ezekieli alitoa unabii gani, na Yehova alianzaje unabii huo?

4 Karibu mwaka wa 612 K.W.K., “neno la Yehova” lilimjia Ezekieli naye akatoa unabii unaoonyesha jinsi utawala wa Masihi utakavyokuwa, na pia umuhimu wa kutegemea Ufalme wake. Yehova alianza unabii huo kwa kumwongoza Ezekieli awasimulie wahamishwa wenzake fumbo la kinabii lililoonyesha ukosefu wa imani wa watawala wa Yuda na umuhimu wa kuwa na Mtawala mwadilifu wa Kimasihi.—Eze. 17:1, 2.

5. Fumbo hilo linahusisha nini?

5 Soma Ezekieli 17:3-10. Ufuatao ni muhtasari wa fumbo hilo: “Tai mkubwa” anachukua chipukizi lililo juu zaidi la mwerezi na kuliweka katika “jiji la wafanyabiashara.” Kisha tai huyo anachukua “baadhi ya mbegu za nchi hiyo” na kuzipanda katika shamba lenye rutuba “kando ya maji mengi.” Mbegu hiyo inasitawi na kuwa ‘mzabibu unaotambaa.’ Kisha “tai mwingine mkubwa” anatokea. Mizizi ya ule mzabibu inasambaa “kwa bidii kuelekea” yule tai wa pili ikitaka kupandwa tena katika eneo lingine lenye maji. Yehova anashutumu matendo ya mzabibu huo, na kuonyesha kwamba mizizi yake itang’olewa nao ‘utakauka kabisa.’

Tai mkubwa wa kwanza aliwakilisha Mfalme Nebukadneza wa Babiloni (Tazama fungu la 6)

6. Fafanua maana ya fumbo hilo.

6 Fumbo hilo lilimaanisha nini? (Soma Ezekieli 17:11-15.) Mwaka wa 617 K.W.K., Mfalme Nebukadneza wa Babiloni (“tai mkubwa” wa kwanza) alizingira Yerusalemu. Alimchukua Mfalme Yehoyakini wa Yuda (“chipukizi lililo juu zaidi”) kutoka kwenye kiti chake cha Ufalme na kumpeleka Babiloni (“jiji la wafanyabiashara”). Nebukadneza alimweka Sedekia (mmoja wa “mbegu za nchi” wa familia ya kifalme) awe mtawala huko Yerusalemu. Mfalme mpya wa Yuda aliapishwa katika jina la Mungu, na hivyo kuwajibika kuwa mshikamanifu akiwa mfalme kibaraka. (2 Nya. 36:13) Lakini Sedekia alipuuza kiapo chake; akaasi dhidi ya Babiloni na kugeukia Farao wa Misri (yule “tai mkubwa” wa pili) ili kupata msaada wa kijeshi lakini hakufanikiwa. Yehova alishutumu matendo yasiyo ya uaminifu ya Sedekia aliyevunja kiapo. (Eze. 17:16-21) Mwishowe, Sedekia aling’olewa mamlakani, na kufa gerezani huko Babiloni.—Yer. 52:6-11.

7. Tunajifunza nini kutokana na fumbo hilo la kinabii?

7 Tunajifunza somo gani kutokana na fumbo hilo la kinabii? Kwanza, tukiwa waabudu wa kweli tunapaswa kutimiza ahadi zetu. Yesu alisema: “Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo.” (Mt. 5:37) Tunapoombwa kuapa mbele za Mungu kwamba tutasema ukweli—kwa mfano tunapotoa ushahidi mahakamani—tunachukua kiapo hicho kwa uzito. Pili, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu watu tunaowategemea. Biblia inatuonya hivi: “Msiwatumaini wakuu wala mwanadamu, ambaye hawezi kuleta wokovu.”—Zab. 146:3.

8-10. Yehova alimfafanuaje Mtawala wa Kimasihi wa wakati ujao, na unabii huo unatimizwaje? (Tazama pia sanduku “Unabii Kuhusu Masihi—Mwerezi Mkubwa.”)

8 Hata hivyo, kuna mtawala ambaye tunapaswa kumwamini na kumtegemea kabisa. Baada ya kutoa fumbo la kinabii kuhusu chipukizi lililohamishwa, Yehova alitumia mfano huohuo wa kinabii kufafanua Mtawala wa Kimasihi wa wakati ujao.

9 Unabii huo unasema nini? (Soma Ezekieli 17:22-24.) Sasa Yehova ndiye atakayechukua hatua bali si tai wakubwa. Atachukua chipukizi changa “kutoka katika kilele cha mwerezi mkubwa na kulipanda . . . juu ya mlima mrefu na ulio juu sana.” Chipukizi hilo litasitawi na kuwa “mwerezi mkubwa” na kuandaa makao kwa ajili ya “ndege wa kila aina.” Kisha “miti yote ya shambani” itajua kwamba Yehova ndiye aliyeufanya mti huo mkubwa usitawi.

10 Jinsi unabii huo unavyotimizwa. Yehova alimchukua mwana wake, Yesu Kristo kutoka kwenye ukoo wa kifalme wa Daudi (“mwerezi mkubwa”) na kumpanda juu ya Mlima Sayuni ulio mbinguni (“mlima mrefu na ulio juu sana”). (Zab. 2:6; Yer. 23:5; Ufu. 14:1) Kwa hiyo, Yehova alimchukua Mwana wake, ambaye alionwa na adui zake kuwa “mwanadamu wa hali ya chini zaidi” na kumkweza kwa kumpa “kiti cha ufalme cha Daudi baba yake.” (Dan. 4:17; Luka 1:32, 33) Kama mwerezi mkubwa, Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo atatawala dunia nzima na kuwaletea raia zake wote baraka. Kwa kweli, huyo ndiye Mtawala tunayepaswa kumtegemea. Chini ya kivuli cha utawala wa Ufalme wa Yesu, wanadamu waaminifu duniani kote ‘wataishi kwa usalama bila kuhangaishwa na woga wa msiba.’—Met. 1:33.

11. Tunajifunza somo gani muhimu kutokana na unabii kuhusu “chipukizi changa” linalokuwa “mwerezi mkubwa”?

11 Tunajifunza nini kutokana na unabii huo? Unabii wenye kusisimua kuhusu “chipukizi changa” linalokuwa “mwerezi mkubwa” unatusaidia kujibu swali muhimu sana: Tunapaswa kumtegemea nani? Ni upumbavu kutegemea serikali za wanadamu na majeshi yake. Ili kupata usalama wa kweli, ni jambo la hekima kumtumaini na kumtegemea kabisa Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo. Serikali ya mbinguni iliyo katika mikono yake yenye uwezo ndio tumaini pekee la wanadamu.—Ufu. 11:15.

“Yule Aliye na Haki ya Kisheria”

12. Yehova alionyeshaje wazi kwamba hakuwa amesahau agano alilofanya pamoja na Daudi?

12 Kutokana na ufafanuzi wa Mungu kuhusu fumbo la kinabii la tai wawili, Ezekieli alielewa kwamba Sedekia, mfalme asiye mwaminifu wa ukoo wa Daudi, angeng’olewa mamlakani na kupelekwa utekwani Babiloni. Labda nabii huyo alijiuliza, ‘Namna gani kuhusu agano la Mungu pamoja na Daudi, aliloahidi kwamba mfalme kutoka katika familia ya Daudi angetawala milele?’ (2 Sam. 7:12, 16) Ikiwa Ezekieli alijiuliza swali hilo, hangesubiri muda mrefu kabla ya kupata jibu. Karibu mwaka wa 611 K.W.K., katika mwaka wa saba wa uhamisho, Sedekia akiwa bado anatawala Yuda, ‘neno la Yehova lilimjia’ Ezekieli. (Eze. 20:2) Yehova alimwongoza kutoa unabii mwingine wa Kimasihi, ulioonyesha wazi kwamba Mungu hakuwa amesahau agano lake pamoja na Daudi. Badala yake, unabii huo ulionyesha kwamba Mtawala wa Kimasihi wa wakati ujao angekuwa na haki ya kisheria ya kutawala akiwa mrithi wa Daudi.

13, 14. Unabii ulioandikwa kwenye Ezekieli 21:25-27 unahusisha nini, na unabii huo unatimizwaje?

13 Unabii huo unasema nini? (Soma Ezekieli 21:25-27.) Akitaja mambo waziwazi, Yehova kupitia Ezekieli anazungumza na “mkuu mwovu wa Israeli,” ambaye wakati wake wa kuadhibiwa umefika. Yehova anamwambia mtawala huyo mwovu kwamba angenyang’anywa “kilemba” chake na “taji” lake (ishara za mamlaka ya kifalme). Kisha, serikali zilizokuwa “chini” zingeinuliwa, na zile zilizokuwa “juu” zingeshushwa. Serikali zilizoinuliwa zingeendelea kutawala, lakini mpaka “yule aliye na haki ya kisheria atakapokuja,” kisha Yehova ampe Ufalme.

14 Jinsi unabii huo unavyotimizwa. Mwaka wa 607 K.W.K., Yerusalemu lilipoharibiwa, ufalme wa Yuda uliokuwa “juu” ambao makao yake yalikuwa Yerusalemu ulishushwa Wababiloni walipoharibu jiji hilo, wakamng’oa mamlakani Mfalme Sedekia, na kumchukua mateka. Kisha, Yerusalemu likiwa bila mfalme wa ukoo wa kifalme wa Daudi, serikali za watu wa mataifa zilizo “chini” ziliinuliwa, zikaanza kuitawala dunia—lakini kwa kipindi kifupi tu. Nyakati za Mataifa, au “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilikwisha mwaka wa 1914 Yehova alipomfanya Yesu kuwa mfalme. (Luka 21:24) Akiwa mzao wa Mfalme Daudi, kwa kweli Yesu alikuwa na “haki ya kisheria” ya kukabidhiwa Ufalme wa Kimasihi. * (Mwa. 49:10) Hivyo, kupitia Yesu, Yehova alitimiza ahadi aliyompa Daudi ya kuwa na mrithi wa kudumu wa Ufalme wa milele.—Luka 1:32, 33.

Yesu akiwa na haki ya kisheria ya kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu (Tazama fungu la 15)

15. Kwa nini tunaweza kumtegemea kabisa Mfalme, Yesu Kristo?

15 Tunajifunza nini kutokana na unabii huo? Tunaweza kumtegemea kabisa Mfalme, Yesu Kristo. Kwa nini? Kwa sababu tofauti na watawala wa ulimwengu ambao huenda wakachaguliwa na wanadamu au kupindua mamlaka zinazotawala, Yesu alichaguliwa na Yehova na ‘kupewa ufalme’ ambao ana haki ya kifalme ya kuupata. (Dan. 7:13, 14) Kwa kweli, tunapaswa kumtegemea kabisa Mfalme ambaye amechaguliwa na Yehova mwenyewe!

“Mtumishi Wangu Daudi” Atakuwa “Mchungaji Wao”

16. Yehova anahisije kuhusu kondoo wake, na “wachungaji wa Israeli” katika siku za Ezekieli walilitendeaje kundi?

16 Yehova, Mchungaji Mkuu Zaidi, anawajali sana kondoo wake, yaani, waabudu wake walio duniani. (Zab. 100:3) Anapowakabidhi wachungaji wadogo wa kibinadamu—wale walio na mamlaka—jukumu la kuwatunza kondoo wake, anaangalia kwa makini jinsi wanavyowatendea kondoo wake. Basi, wazia jinsi Yehova alivyohisi kuhusu “wachungaji wa Israeli” katika siku za Ezekieli. Watawala hao walitawala “kwa ukali na kwa uonevu” bila aibu. Matokeo ni kwamba, kondoo waliteseka, na wengi wakaacha ibada safi.—Eze. 34:1-6.

17. Yehova aliwaokoaje kondoo wake?

17 Yehova angefanya nini? Aliwaambia hivi watawala wakali Waisraeli: “Nitafanya wawajibike.” Kisha akaahidi hivi: “Nitawaokoa kondoo wangu.” (Eze. 34:10) Sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake. (Yos. 21:45) Mwaka wa 607 K.W.K., aliwaokoa kondoo wake alipotumia Wababiloni kuwashambulia na kuwanyang’anya utawala wachungaji hao wenye ubinafsi. Miaka sabini baadaye, aliwakomboa kutoka Babiloni waabudu wake walio kama kondoo na kuwarudisha katika nchi yao ili warudishe ibada ya kweli huko. Lakini bado kondoo wa Yehova wangeweza kushambuliwa, kwa sababu wangeendelea kuwa chini ya utawala wa serikali za ulimwengu. “Nyakati zilizowekwa za mataifa” zingeendelea kwa karne nyingi.—Luka 21:24.

18, 19. Ezekieli alitoa unabii gani mwaka wa 606 K.W.K.? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

18 Mwaka wa 606 K.W.K., karibu mwaka mmoja baada ya Yerusalemu kuharibiwa na miaka mingi kabla ya Waisraeli kukombolewa kutoka uhamishoni Babiloni, Yehova alimwongoza Ezekieli kutoa unabii unaoonyesha jinsi Mchungaji Mkuu Zaidi anavyowajali sana kondoo wake kwa umilele. Unabii huo unafafanua jinsi Mtawala wa Kimasihi atakavyowachunga kondoo wa Yehova.

19 Unabii huo unasema nini? (Soma Ezekieli 34:22-24.) Mungu atamweka “mchungaji mmoja,” ambaye anamwita “mtumishi wangu Daudi.” Maneno “mchungaji mmoja” pamoja na neno “mtumishi” yanamaanisha kwamba Mtawala huyo hangeanzisha nasaba ya wafalme katika ukoo wa Daudi bali angekuwa mrithi pekee wa kudumu wa Daudi. Mtawala huyo aliye Mchungaji atawalisha kondoo wa Mungu na kuwa “kiongozi wao.” Yehova atafanya “agano la amani” pamoja na kondoo wake. “Baraka zitamwagika [juu yao] kama mvua,” nao watafurahia hali yenye kupendeza ya usalama, ufanisi, na kunawiri. Naam, kutakuwa na amani kati ya wanadamu na pia kati ya wanadamu na wanyama!—Eze. 34:25-28.

20, 21. (a) Unabii kuhusu “mtumishi wangu Daudi” unatimizwaje? (b) Maneno ya Ezekieli kuhusu “agano la amani” yatakuwa na maana gani wakati ujao?

20 Jinsi unabii huo unavyotimizwa. Kwa kumwita Mtawala huyo “mtumishi wangu Daudi,” Mungu alitoa unabii kumhusu Yesu, mzao wa Daudi aliye na haki ya kisheria ya kutawala. (Zab. 89:35, 36) Alipokuwa duniani, Yesu alithibitika kuwa “mchungaji mwema,” kwa kutoa uhai wake “kwa ajili ya kondoo.” (Yoh. 10:14, 15) Lakini sasa ni Mchungaji aliye mbinguni. (Ebr. 13:20) Mwaka wa 1914, Mungu alimweka Yesu kuwa Mfalme na akamkabidhi jukumu la kuwachunga na kuwalisha kondoo wa Mungu walio duniani. Muda mfupi baadaye, mwaka wa 1919, Mfalme mpya aliyetawazwa alimchagua “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” awalishe ‘watumishi wa nyumbani’—watumishi washikamanifu wa Mungu walio na tumaini la kuishi mbinguni au duniani. (Mt. 24:45-47) Chini ya mwongozo wa Kristo, mtumwa mwaminifu ameendelea kuwalisha vizuri kondoo wa Mungu chakula cha kiroho. Chakula hicho kimewasaidia kudumisha amani na usalama katika paradiso ya sasa ya kiroho.

21 Maneno ya Ezekieli kuhusu “agano la amani” na mvua ya baraka yatakuwa na maana gani wakati ujao? Katika ulimwengu mpya unaokuja, waabudu wa kweli wa Yehova duniani watafurahia kikamili baraka za “agano la amani.” Katika paradiso halisi duniani kote, wanadamu waaminifu hawataogopa tena vita, uhalifu, njaa, magonjwa, au wanyama wa mwituni. (Isa. 11:6-9; 35:5, 6; 65:21-23) Je, huchochewi na tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani ambako kondoo wa Mungu “wataishi kwa usalama, na hakuna mtu atakayewaogopesha”?—Eze. 34:28.

Akiwa Mchungaji aliye mbinguni, Yesu anatazama jinsi kondoo wa Mungu wanavyotendewa (Tazama fungu la 22)

22. Yesu anahisije kuhusu kondoo, na wale wanaotumikia wakiwa wachungaji wadogo wanawezaje kuonyesha kwamba wanawajali?

22 Tunajifunza nini kutokana na unabii huo? Kama Baba yake, Yesu anawajali sana kondoo. Mtawala aliye Mchungaji anahakikisha kwamba kondoo wa Baba yake wanalishwa vizuri kiroho na wanafurahia amani na usalama katika paradiso ya kiroho. Inapendeza sana kutunzwa na Mtawala huyo! Wale wanaotumikia wakiwa wachungaji wadogo wanapaswa kuiga jinsi Yesu anavyowahangaikia kondoo. Wazee wanapaswa kulichunga kundi “kwa kupenda” na kwa “hamu” na kuweka mfano ambao kondoo wanaweza kuiga. (1 Pet. 5:2, 3) Mzee hapaswi kamwe kumtendea vibaya kondoo yeyote wa Yehova! Kumbuka maneno ya Yehova kwa wachungaji wa kale wa Israeli waliokuwa wakali katika siku za Ezekieli: “Nitafanya wawajibike.” (Eze. 34:10) Yehova Mchungaji Mkuu Zaidi, na Mwana wake, wanatazama kwa makini jinsi kondoo wa Yehova wanavyotendewa.

“Mtumishi Wangu Daudi Atakuwa Kiongozi Wao Milele”

23. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu kuunganisha taifa la Israeli, naye alitimizaje ahadi hiyo?

23 Yehova anataka waabudu wake wamtumikie pamoja kwa umoja. Katika unabii kuhusu kurudishwa, Mungu aliahidi kwamba angewakusanya watu wake—watu wa ufalme wa Yuda wenye makabila mawili na wa ufalme wa Israeli wenye makabila kumi—na kuwaunganisha kuwa “taifa moja,” kana kwamba anafanya “vijiti” viwili viwe “kijiti kimoja” mkononi mwake. (Eze. 37:15-23) Unabii huo ulitimizwa Mungu aliporudisha taifa lililoungana la Israeli katika Nchi ya Ahadi mwaka wa 537 K.W.K. * Lakini umoja huo ulikuwa kionjo tu cha umoja mkubwa zaidi wa kudumu utakaokuja. Baada ya kuahidi kuunganisha Israeli, Yehova alimpa Ezekieli unabii kuhusu jinsi Mtawala wa wakati ujao atakavyowaunganisha waabudu wa kweli duniani kote katika muungano wa umoja ambao utadumu milele.

24. Yehova anamfafanuaje Mtawala wa Kimasihi, na utawala wa Mfalme huyo utakuwaje?

24 Unabii huo unasema nini? (Soma Ezekieli 37:24-28.) Kwa mara nyingine tena Yehova anamwita Mtawala wa Kimasihi “mtumishi wangu Daudi,” “mchungaji mmoja,” na “kiongozi.” Lakini pia, sasa Yehova anamwita Yule Aliyeahidiwa, “mfalme.” (Eze. 37:22) Utawala wa Mfalme huyo utakuwaje? Utawala wake utakuwa wa kudumu. Neno “milele” linaonyesha kwamba hakutakuwa na mwisho wa baraka za utawala wa Mfalme huyo. * Kutakuwa na umoja chini ya utawala wake. Chini ya “mfalme mmoja” raia washikamanifu watafuata “sheria,” na “wataishi [pamoja] katika nchi.” Utawala wake utafanya raia wa Mfalme wamkaribie zaidi Yehova Mungu. Yehova atafanya “agano la amani” pamoja na raia hao. Yehova atakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wake. Na mahali pake patakatifu patakuwa “kati yao milele.”

25. Unabii kuhusu Mfalme wa Kimasihi unatimizwaje?

25 Unabii huo unatimizwaje? Mwaka wa 1919, watiwa mafuta waaminifu waliunganishwa chini ya “mchungaji mmoja,” Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo. Baadaye, “umati mkubwa” kutoka “mataifa yote na makabila na jamii na lugha” uliungana na waamini wenzao waliotiwa mafuta. (Ufu. 7:9) Pamoja, wamekuwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja.” (Yoh. 10:16) Iwe wana tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, wote wanatii sheria za Yehova. Matokeo ni kwamba wanakaa pamoja katika paradiso ya kiroho wakiwa undugu wenye umoja wa ulimwenguni pote. Yehova amewabariki kwa kuwapa amani, na mahali pake patakatifu, panapowakilisha ibada yake safi pako kati yao. Yehova ndiye Mungu wao, nao wanajivunia kuwa waabudu wake, sasa na milele!

26. Tunawezaje kuchangia umoja wa paradiso ya kiroho?

26 Tunajifunza nini kutokana na unabii huo? Tuna pendeleo la kuunganishwa katika undugu wa ulimwenguni pote unaomtolea Yehova ibada safi. Lakini pendeleo hilo linatokeza wajibu, tunapaswa kuendeleza umoja. Hivyo, sisi sote tunapaswa kutimiza sehemu yetu ili kudumisha umoja wa imani na matendo. (1 Kor. 1:10) Ili kufanya hivyo, tunajitahidi kula chakula kilekile cha kiroho, tunafuata viwango vilevile vya mwenendo, na tunashiriki katika kazi ileile muhimu ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Hata hivyo, siri ya umoja wetu ni upendo. Tunapojitahidi kuonyesha upendo kwa njia mbalimbali—kutia ndani hisia-mwenzi, huruma, na kusamehe—tunachangia umoja. Biblia inasema: “Upendo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:12-14; 1 Kor. 13:4-7.

Yehova anawabariki waabudu wake walio katika undugu wa ulimwenguni pote wenye upendo (Tazama fungu la 26)

27. (a) Unahisije kuhusu unabii kumhusu Masihi ulio katika kitabu cha Ezekieli? (b) Tutachunguza nini katika sura zinazofuata?

27 Tunashukuru sana kwa sababu ya unabii kuhusu Masihi ulio katika kitabu cha Ezekieli! Kusoma na kutafakari unabii huo kunatufundisha kwamba tunapaswa kumtegemea Mfalme wetu mpendwa, Yesu Kristo, aliye na haki ya kisheria ya kutawala, ambaye anatuchunga kwa wororo, na atakayetusaidia kuwa na umoja utakaodumu milele. Tuna pendeleo kubwa la kuwa raia wa Mfalme wa Kimasihi! Acheni tukumbuke kwamba unabii huu kuhusu Masihi ni sehemu ya ujumbe mkuu wa kurudishwa kwa ibada ambao unazungumziwa katika kitabu cha Biblia cha Ezekieli. Kupitia Yesu, Yehova anakusanya watu Wake na kurudisha ibada safi kati yao. (Eze. 20:41) Katika sura zinazofuata za kitabu hiki, tutachunguza ujumbe huo wenye kusisimua wa kurudishwa na jinsi unavyofafanuliwa katika kitabu cha Ezekieli.

^ fu. 1 Mwaka wa kwanza wa uhamisho ulianza 617 K.W.K., mateka wa kwanza Wayahudi walipopelekwa Babiloni. Hivyo, mwaka wa sita ulianza 612 K.W.K.

^ fu. 14 Ukoo wa Yesu kutokana na Daudi umeorodheshwa vizuri katika vitabu vya Injili vilivyoongozwa na roho.—Mt. 1:1-16; Luka 3:23-31.

^ fu. 23 Unabii wa Ezekieli kuhusu vijiti viwili na jinsi ulivyotimizwa utazungumziwa katika Sura ya 12 ya kitabu hiki.

^ fu. 24 Kuhusu neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “milele,” kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Mbali na kuonyesha muda, neno hilo lina maana ya kudumu, kuendelea, kutoharibika, kutobadilika, na kutoweza kung’olewa.”