Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 13

“Waeleze . . . Kuhusu Hekalu”

“Waeleze . . . Kuhusu Hekalu”

EZEKIELI 43:10

WAZO KUU: Maana ya maono yenye utukufu ya hekalu la Ezekieli

1-3. (a) Kwa nini huenda Ezekieli alifarijiwa na maono ya majengo makubwa ya hekalu? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.) (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?

MWAZIE Ezekieli akiwa na umri wa miaka 50. Ameishi uhamishoni kwa miaka 25. Kwa kipindi hicho hekalu lililo Yerusalemu limekuwa magofu. Ikiwa Ezekieli alitazamia kwamba angetumikia akiwa kuhani huko Yerusalemu, matumaini hayo yamepotea. Kipindi cha kuwa uhamishoni kitakwisha baada ya miaka 56 hivi, basi Ezekieli anajua haiwezekani kwamba ataishi kufikia kipindi ambacho watu wa Mungu watarudishwa kwenye nchi yao, na kujenga upya hekalu. (Yer. 25:11) Je, anahuzunishwa na mawazo hayo?

2 Kwa fadhili, katika kipindi hiki Yehova anampa Ezekieli maono yenye kina, ambayo yatamfariji sana na kumpa tumaini mwanamume huyu mwaminifu! Kupitia maono hayo, nabii huyo anasafirishwa hadi nchi ya kwao na kuwekwa juu ya mlima mrefu sana. Akiwa mahali hapo palipoinuka, anakutana na “mtu fulani ambaye [anaonekana] kama shaba.” Malaika huyo anamtembeza na kumwonyesha kila mahali katika hekalu kubwa sana. (Soma Ezekieli 40:1-4.) Maono hayo yanaonekana kuwa halisi kabisa! Ezekieli anaimarishwa imani, anastaajabishwa, na labda hata anashangazwa na maono hayo. Ingawa hekalu analoona lina vitu vingi anavyovifahamu, linatofautiana sana na hekalu alilofahamu huko Yerusalemu.

3 Maono hayo yenye kusisimua yameandikwa katika sura tisa za mwisho za kitabu cha Ezekieli. Acheni sasa tuzungumzie mtazamo tunaopaswa kuwa nao tunapochunguza maono hayo na kujaribu kuyaelewa. Kisha tutazungumzia ikiwa hekalu aliloona Ezekieli lilikuwa hekalu kubwa la kiroho ambalo Paulo alilizungumzia kwa kina karne nyingi baadaye. Mwishowe tutachunguza maana ya maono hayo kwa Ezekieli na wahamishwa wenzake.

Kwa Nini Tunahitaji Mtazamo Tofauti?

4. Maono ya hekalu yalifafanuliwaje wakati uliopita, lakini sasa yanafafanuliwaje?

4 Zamani, machapisho yetu yalisema kwamba Ezekieli aliona hekalu kubwa la kiroho la Yehova, ambalo mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika kulihusu katika barua yake kwa Waebrania. * Kwa kutegemea maoni hayo, ilionekana inapatana na akili kuamini kwamba kwa msingi wa maelezo ya Paulo kuhusu hema la ibada mambo mengi katika hekalu aliloona Ezekieli yalikuwa mifano au yaliwakilisha mambo fulani. Hata hivyo, baada ya kusali na kutafakari zaidi imeonekana kwamba tunahitaji kufafanua kwa njia rahisi zaidi hekalu aliloona Ezekieli.

5, 6. (a) Mtume Paulo alionyeshaje unyenyekevu alipozungumzia hema la ibada? (b) Paulo alisema nini kuhusu baadhi ya vitu vilivyokuwa katika hema la ibada, na tunawezaje kutumia kanuni hiyo ili kuelewa maono ya hekalu aliloona Ezekieli?

5 Ni jambo la hekima kwamba hatutafuti maana ya kinabii au mfano katika kila jambo kwenye hekalu aliloona Ezekieli. Kwa nini? Fikiria mfano wenye kupendeza. Paulo alipozungumzia hema la ibada na hekalu la kiroho, alitaja mambo mbalimbali kuhusu hema la ibada, kama vile chetezo cha dhahabu, kifuniko cha sanduku la agano, na mtungi wa dhahabu uliokuwa na mana. Je, alisema kwamba vitu hivyo vilikuwa na maana ya kinabii? Inaonekana roho takatifu haikumwongoza kusema hivyo. Badala yake, Paulo aliandika hivi: “Sasa si wakati wa kuzungumzia mambo hayo kirefu.” (Ebr. 9:4, 5) Paulo alikuwa tayari kufuata mwongozo wa roho takatifu na kumsubiri Yehova kwa unyenyekevu.—Ebr. 9:8.

6 Tunaweza kusema hivyo pia kuhusu hekalu aliloona Ezekieli. Hekalu hilo pia lina vitu vingi. Ni jambo la busara kumsubiri Yehova afafanue mambo, ikiwa ufafanuzi zaidi unahitajika. (Soma Mika 7:7.) Hata hivyo, je, inamaanisha kwamba roho ya Yehova haijafunua wazi zaidi maana ya maono hayo? La hasha!

Je, Ezekieli Aliona Hekalu Kubwa la Kiroho?

7, 8. (a) Ni uelewaji gani ambao sasa umerekebishwa? (b) Hekalu aliloona Ezekieli linatofautianaje na hekalu la kiroho ambalo Paulo alilifafanua?

7 Kama ilivyotajwa, kwa miaka mingi machapisho yetu yamefafanua kwamba Ezekieli aliona hekalu kubwa la kiroho la Yehova, ambalo Paulo aliongozwa na roho kuandika katika barua yake kwa Waebrania. Hata hivyo, baada ya kuchunguza zaidi tumeona kwamba Ezekieli hakuona hekalu kubwa la kiroho. Kwa nini?

8 Kwanza, hekalu ambalo Ezekieli aliona linatofautiana na ufafanuzi wa Paulo ulioongozwa na roho. Fikiria jambo hili: Mtume Paulo alisema wazi kwamba hema la ibada la siku za Musa lilikuwa kivuli na mfano wa jambo kubwa zaidi. Kama hekalu la Sulemani na hekalu la Zerubabeli, yaliyokuwa na muundo uleule, hema la ibada lilikuwa na sehemu iliyoitwa “Patakatifu Zaidi.” Paulo aliita sehemu hiyo “mahali patakatifu palipotengenezwa kwa mikono,” na kueleza kwamba palikuwa “mfano wa uhalisi,” na si uhalisi wenyewe. Uhalisi ulikuwa nini? Paulo alieleza hivi: “Mbinguni kwenyewe.” (Ebr. 9:3, 24) Je, Ezekieli aliona mambo yaliyo mbinguni? Hapana. Maono ya Ezekieli hayaonyeshi kwamba alikuwa akiona vitu vilivyo mbinguni.—Linganisha na Danieli 7:9, 10, 13, 14.

9, 10. Inapohusu dhabihu, hekalu aliloona Ezekieli linatofautianaje na hekalu kubwa la kiroho ambalo Paulo alilifafanua?

9 Tofauti kubwa zaidi kati ya maono ya Ezekieli na maelezo ya Paulo inahusu dhabihu. Ezekieli alisikia maagizo mengi kuhusu kutoa dhabihu yakitolewa kwa watu, wakuu, na makuhani. Walipaswa kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe. Pia walipaswa kutoa dhabihu za ushirika, ambazo wangekula pamoja katika vyumba vya kulia chakula hekaluni. (Eze. 43:18, 19; 44:11, 15, 27; 45:15-20, 22-25) Je, katika hekalu kubwa la kiroho kuna dhabihu kama hizo zinazotolewa tena na tena?

Hekalu ambalo Ezekieli aliona si hekalu kubwa la kiroho

10 Jibu ni wazi na linaeleweka. Paulo alifafanua hivi: “Kristo alipokuja akiwa kuhani mkuu wa mambo mema ambayo tayari yamefanyika, aliingia katika hema kubwa na kamilifu zaidi ambalo halikutengenezwa kwa mikono, yaani, si la uumbaji huu. Aliingia mahali patakatifu, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote, na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu.” (Ebr. 9:11, 12) Basi katika hekalu kubwa la kiroho, ni dhabihu moja tu inayotolewa—kwa wakati wote. Ni dhabihu ya fidia, nayo inatolewa na Kuhani Mkuu Zaidi mwenyewe, Yesu Kristo. Ni wazi kwamba hekalu ambalo Ezekieli aliona lililokuwa na dhabihu nyingi za mbuzi na ng’ombe dume, halikuwa hekalu kubwa la kiroho.

11. Katika siku za Ezekieli, kwa nini muda haukuwa umefika wa Mungu kufunua ukweli kuhusu hekalu kubwa la kiroho?

11 Sasa tutazungumzia sababu ya pili inayoonyesha kwamba Ezekieli hakuona hekalu kubwa la kiroho: Muda wa Mungu wa kufunua kweli hizo haukuwa umefika. Kumbuka kwamba maono ya Ezekieli yaliwahusu hasa Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni. Walikuwa chini ya Sheria ya Musa. Baada ya kipindi cha kuwa uhamishoni kwisha, wangerudi Yerusalemu na kufuata Sheria katika ibada safi nao wangejenga hekalu pamoja na madhabahu yake. Kisha wangeendelea kutoa dhabihu humo, na walifanya hivyo kwa karibu karne sita. Wayahudi wangetendaje ikiwa maono ya Ezekieli yangewaonyesha hekalu la kiroho—hekalu ambamo kuhani mkuu alitoa uhai wake mwenyewe kuwa dhabihu, kisha dhabihu nyingine zote ziondolewe? Je, wangeelewa maono hayo? Je, hilo halingefanya wapuuze Sheria ya Musa? Kama kawaida, Yehova hufunua kweli hasa wakati unaofaa na watu wake wanapokuwa tayari.

12-14. Kuna uhusiano gani kati ya hekalu ambalo Ezekieli aliona na maelezo ya Paulo kuhusu hekalu la kiroho? (Tazama sanduku “Mahekalu Tofauti, Masomo Tofauti.”)

12 Basi, kuna uhusiano gani kati ya hekalu aliloona Ezekieli na maelezo ya Paulo kuhusu hekalu la kiroho? Kumbuka kwamba mazungumzo ya Paulo hayakutegemea hekalu aliloona Ezekieli; badala yake yalitegemea hema la ibada la siku za Musa. Ni kweli kwamba Paulo alitaja baadhi ya vitu vilivyokuwa pia katika hekalu la Sulemani na la Zerubabeli na ambavyo pia vilitajwa katika hekalu aliloona Ezekieli. Lakini kwa ujumla Ezekieli na Paulo walikazia mambo tofauti katika maandishi yao. * Hawakufafanua jambo lilelile, hata hivyo maandishi yao yanakamilishana. Jinsi gani?

13 Tunaweza kufikiria uhusiano kati ya masimulizi hayo mawili ya Biblia kwa njia hii: Kutokana na Paulo, tunajifunza mpango wa Yehova kuhusu ibada, lakini kutokana na Ezekieli, tunajifunza viwango vya Yehova kuhusu ibada. Paulo anatufundisha kuhusu mpango wa Yehova wa ibada safi, kwa kufafanua maana ya mambo mbalimbali ya hekalu la kiroho kama vile kuhani mkuu, dhabihu, madhabahu, na Patakatifu Zaidi. Lakini hekalu aliloona Ezekieli linakazia viwango vya juu vya Yehova kuhusu ibada safi, kwa kutupatia habari nyingi zinazokazia katika akili na mioyo yetu masomo mengi kuhusu viwango vya Yehova.

14 Basi, sasa tuna uelewaji gani uliorekebishwa? Haimaanishi kamwe kwamba maono ya Ezekieli hayatuhusu sana leo. Ili kuona jinsi tunavyofaidika kutokana na maono hayo, acheni tuchunguze kwa makini jinsi Wayahudi waaminifu walivyofaidika kutokana na maono hayo katika siku za Ezekieli na baadaye.

Maono Hayo Yalikuwa na Maana Gani kwa Wayahudi Waliohamishwa?

15. (a) Kwa ujumla, maono ya Ezekieli yalikuwa na ujumbe gani? (b) Kuna tofauti gani kati ya Ezekieli sura ya 8 na Ezekieli sura ya 40 hadi 48?

15 Ili kupata jibu la Biblia kuhusu swali hilo, acheni tuchunguze maswali kadhaa yanayohusiana ambayo yatatusaidia kuelewa jambo hilo kikamili. Kwanza, unabii huo ulikuwa na ujumbe gani kwa ujumla? Kwa ufupi, ujumbe ulikuwa kwamba ibada safi ingerudishwa! Ni kweli kwamba Ezekieli alielewa jambo hilo. Alikuwa tayari ameandika sura ya 8 ya Ezekieli, ambapo Yehova alikuwa amemwonyesha hali yenye kuchukiza ya hekalu huko Yerusalemu. Ezekieli alifurahia sana kuandika kwa undani kuhusu jambo tofauti, katika sura ya 40 hadi 48. Hapa hatuoni ibada iliyopotoka, bali ibada safi kama ilivyopaswa kuwa—mfano mkamilifu wa kumwabudu Yehova kulingana na Sheria ya Musa.

16. Hekalu aliloona Ezekieli linathibitishaje jambo ambalo Isaya alikuwa ametabiri karne moja mapema?

16 Ili kurudisha ibada ya Yehova mahali pake, ilihitaji kuinuliwa. Zaidi ya karne moja mapema nabii Isaya aliongozwa na roho kuandika hivi: “Katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya Yehova utaimarishwa kabisa juu ya vilele vya milima, nao utainuliwa juu ya vilima.” (Isa. 2:2) Isaya aliona wazi kimbele kwamba ibada safi ingerudishwa na kuinuliwa, kana kwamba imewekwa juu ya mlima mrefu zaidi. Sasa, Ezekieli alikuwa wapi alipopata maono haya kutoka kwa Mungu? Alikuwa “juu ya mlima mrefu sana,” akitazama nyumba ya Yehova! (Eze. 40:2) Kwa hiyo, maono ya Ezekieli yanathibitisha kwamba ibada safi ingerudishwa.

Hekalu aliloona Ezekieli lilikuwa mahali palipo juu, palipoinuliwa sana (Tazama fungu la 16)

17. Eleza muhtasari wa Ezekieli sura ya 40 hadi 48.

17 Fikiria muhtasari wa mambo ambayo Ezekieli aliona na kusikia, kama ilivyoandikwa kwenye Ezekieli sura ya 40 hadi 48. Alimtazama malaika akipima malango, ukuta, nyua, na patakatifu pa hekalu. (Eze. 40-42) Kisha jambo lenye kusisimua linatokea: Utukufu wa Yehova unawasili hekaluni! Yehova aliwapa ushauri watu wake waliopotoka, makuhani, na wakuu. (Eze. 43:1-12; 44:10-31; 45:9-12) Ezekieli aliona mto ukitiririka kutoka patakatifu, na kuleta uhai na baraka ulipokuwa ukiingia katika Bahari ya Chumvi. (Eze. 47:1-12) Naye aliona nchi ikiwa imegawanywa katika vipande hususa, huku ibada safi ikiendelea karibu na katikati ya nchi hiyo. (Eze. 45:1-8; 47:13–48:35) Kwa ujumla, alitangaza ujumbe gani? Yehova alikuwa akiwahikikishia waziwazi watu wake kwamba ibada safi ingerudishwa na kuinuliwa. Angebariki nyumba yake kwa kuwapo kwake, na angefanya baraka hizo zitiririke kutoka kwa hekalu hilo na kuleta uponyaji, uhai, na utaratibu katika nchi iliyorudishwa.

Hekalu aliloona Ezekieli liliwakilisha kwa utukufu jinsi ambavyo Yehova angerudisha ibada safi (Tazama fungu la 17)

18. Je, maono ya hekalu yalipaswa kueleweka kihalisi? Eleza.

18 Pili, je, maono hayo yalipaswa kueleweka kihalisi? Hapana. Inaelekea Ezekieli na wahamishwa wenzake ambao aliwafafanulia maono hayo walitambua mara moja kwamba hayakupaswa kueleweka kihalisi. Kwa nini? Kumbuka kwamba Ezekieli aliona hekalu hilo likiwa juu ya “mlima mrefu sana.” Ingawa jambo hilo lilipatana vizuri na unabii wa Isaya, halikupatana na mahali ambapo hekalu lilikuwa kihalisi. Hekalu la Sulemani lilikuwa juu ya Mlima Moria huko Yerusalemu, nalo lingejengwa upya mahali hapo. Lakini je, huo ulikuwa “mlima mrefu sana”? Hapana. Kwa kweli, Mlima Moria umezungukwa na milima mingine yenye urefu sawa nao au mirefu zaidi. Pia, majengo ya hekalu ambayo Ezekieli aliona yalikuwa makubwa. Eneo lake lililo pana sana lilikuwa limezungukwa na ukuta, na halingetoshea juu ya Mlima Moria. Hata halingetoshea katika jiji la Yerusalemu katika siku za Sulemani! Vilevile, wahamishwa hawakutazamia kwamba mto halisi ungetiririka kutoka patakatifu pa hekalu na kuingia katika Bahari ya Chumvi, ambako ungeponya maji hayo yasiyo na uhai. Mwishowe, eneo lenye milima la Nchi ya Ahadi halingekuwa na mipaka iliyonyooka na iliyo sambamba kati ya makabila, kama ilivyofafanuliwa kwenye maono. Basi maono hayo hayapaswi kufafanuliwa kihalisi.

19-21. Yehova alitaka maono ya Ezekieli yawaathirije watu, na kwa nini hilo liliwachochea?

19 Tatu, Waisraeli walipaswa kuathiriwaje na maono hayo? Walipotafakari viwango vya juu vya Yehova kuhusu ibada safi, watu walipaswa kuaibika. Yehova alimwambia Ezekieli “waeleze watu wa nyumba ya Israeli kuhusu hekalu.” Ezekieli alipaswa kulifafanua hekalu hilo kwa kina ili Waisraeli waweze “kuichunguza ramani yake.” Kwa nini watu walipaswa kutafakari kuhusu hekalu hilo? Kama tulivyoona, hawakufanya hivyo ili walijenge. Badala yake, ni kama Yehova alivyosema, “ili waaibike kwa sababu ya makosa yao.”—Soma Ezekieli 43:10-12.

20 Kwa nini maono hayo yangeweza kugusa dhamiri za watu wenye mioyo minyoofu na kuwafanya waaibike? Ona jambo ambalo Ezekieli aliambiwa: “Mwana wa binadamu, kaza fikira, angalia, na usikilize kwa makini nitakayokuambia kuhusu maagizo na sheria za hekalu la Yehova.” (Eze. 44:5) Ezekieli alisikia tena na tena kuhusu maagizo na sheria. (Eze. 43:11, 12; 44:24; 46:14) Mara kwa mara, Ezekieli alikumbushwa pia kuhusu viwango vya Yehova—hata viwango vya urefu wa mkono na viwango vya mizani sahihi. (Eze. 40:5; 45:10-12; linganisha na Methali 16:11.) Katika maono hayo, Ezekieli aliandika zaidi ya mara 50 maneno “pima” na “kipimo” katika lugha ya awali!

21 Yehova alikuwa akiwaambia nini watu wake alipotaja vipimo, uzani, sheria, na maagizo? Inaonekana alikuwa akiwakumbusha, kwa maneno mazito, kuhusu ukweli huu muhimu: Yehova peke yake ndiye anayeweka viwango vya ibada safi. Wale ambao walikuwa wameacha kufuata viwango hivyo walipaswa kuaibika! Hata hivyo, Wayahudi walijifunzaje masomo hayo kutokana na maono hayo? Tutachunguza mifano hususa katika sura inayofuata. Hilo litatusaidia kuona wazi zaidi maana ya unabii huu muhimu katika siku zetu.

Kwa nini maono ya hekalu yangewafanya watu wenye mioyo minyoofu waaibike? (Tazama fungu la 19-21)

^ fu. 4 Hekalu la kiroho ni mpango wa Yehova wa ibada safi kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Tunaelewa kwamba hekalu hilo lilianzishwa mwaka wa 29 W.K.

^ fu. 12 Kwa mfano, Paulo alikazia kuhani mkuu na jukumu lake kila mwaka katika Siku ya Kufunika Dhambi. (Ebr. 2:17; 3:1; 4:14-16; 5:1-10; 7:1-17, 26-28; 8:1-6; 9:6-28) Lakini maono ya Ezekieli hayataji kuhani mkuu wala Siku ya Kufunika Dhambi.