Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 21

“Jina la Jiji Hilo . . . Litakuwa, Yehova Yupo Hapo”

“Jina la Jiji Hilo . . . Litakuwa, Yehova Yupo Hapo”

EZEKIELI 48:35

WAZO KUU: Maana ya jiji na mchango

1, 2. (a) Ni eneo gani la pekee lililopaswa kuwekwa kando? (Tazama picha kwenye jalada.) (b) Maono hayo yanawapa wahamishwa uhakikisho gani?

KATIKA maono yake ya mwisho, Ezekieli anaona sehemu ya nchi ambayo inapaswa kuwekwa kando kwa ajili ya kusudi la pekee. Sehemu iliyotengwa, haitolewi kuwa urithi wa kabila fulani la Israeli, bali kama mchango kwa Yehova. Pia, Ezekieli anaona jiji la pekee lenye jina la kushangaza. Sehemu hiyo ya maono inawapa wahamishwa uhakikisho huu muhimu zaidi: Yehova atakuwa pamoja nao watakaporudi katika nchi yao wanayoipenda.

2 Ezekieli anatupatia ufafanuzi wa kina kuhusu mchango huo. Acheni tuchunguze simulizi hili, ambalo lina maana kubwa kwetu waabudu wa kweli wa Yehova.

“Mchango Mtakatifu Pamoja na . . . Jiji”

3. Eneo ambalo Yehova aliweka kando lilikuwa na sehemu gani tano, na sehemu hizo zilitimiza kusudi gani? (Tazama sanduku “Mchango Mtakaoweka Kando.”)

3 Eneo hilo la pekee lilikuwa na urefu wa mikono 25,000 (kilomita 13) kuanzia kaskazini hadi kusini, na mikono 25,000 kuanzia mashariki hadi magharibi. Eneo hilo la mraba liliitwa “mchango mzima.” Liligawanywa katika sehemu tatu. Sehemu ya juu ilikuwa ya Walawi, sehemu ya katikati ilitengwa kwa ajili ya hekalu na makuhani. Sehemu hizo mbili zilifanyiza “mchango mtakatifu.” Sehemu ya chini iliyokuwa ndogo, au ‘sehemu iliyobaki,’ ilikuwa kwa ajili ya “matumizi ya kawaida.” Ilikuwa kwa ajili ya jiji.—Eze. 48:15, 20.

4. Tunajifunza somo gani kutokana na simulizi kuhusu mchango kwa Yehova?

4 Tunajifunza somo gani katika simulizi hili kuhusu mchango kwa Yehova? Kwa kutenga kwanza eneo kwa ajili ya mchango wa pekee na kisha maeneo ya makabila, Yehova alionyesha kwamba kituo hicho cha mambo ya kiroho kilipaswa kuwa muhimu zaidi. (Eze. 45:1) Bila shaka, wahamishwa walijifunza mengi kutokana na mpangilio huo wa kugawa nchi. Walipaswa kutanguliza ibada ya Yehova maishani. Vivyo hivyo, leo tunaona mambo ya kiroho, kama vile kujifunza Neno la Mungu, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri, kuwa mambo muhimu zaidi. Tunaiga mfano wa Yehova wa kutanguliza mambo muhimu kwa kufanya ibada yake iwe jambo kuu katika maisha yetu ya kila siku.

“Jiji Litakuwa Katikati Yake”

5, 6. (a) Jiji lilikuwa la nani? (b) Jiji hilo halikuwa nini, na kwa nini?

5 Soma Ezekieli 48:15. “Jiji” na maeneo yaliyolizunguka yalikuwa na maana gani? (Eze. 48:16-18) Yehova alikuwa amemwambia hivi Ezekieli katika maono: “Jiji . . . [litakuwa la] watu wote wa nyumba ya Israeli.” (Eze. 45:6, 7) Basi, jiji na maeneo yaliyolizunguka hayakuwa sehemu ya “mchango mtakatifu” ambao ulipaswa ‘kuwekwa kando kwa ajili ya Yehova.’ (Eze. 48:9) Tukiwa na hilo akilini, acheni tuchunguze jambo tunalojifunza leo kutokana na mpangilio wa jiji hilo.

6 Ili kujifunza masomo kutokana na jiji hilo, kwanza tunahitaji kujua, jiji hilo halikuwa nini? Halikuwa jiji la Yerusalemu pamoja na hekalu lake lililojengwa upya. Kwa nini? Kwa sababu jiji ambalo Ezekieli aliona katika maono halingekuwa na hekalu ndani yake. Pia, jiji hilo halikuwa jiji lingine katika nchi ya Israeli iliyorudishwa. Kwa nini? Kwa maana wahamishwa waliorudi pamoja na wazao wao hawakujenga jiji lenye mambo yaliyotajwa katika maono. Isitoshe, jiji hilo halikuwa jiji la kimbingu. Kwa nini? Kwa kuwa lilijengwa kwenye eneo lililotengwa kwa ajili ya “matumizi ya kawaida [au, matumizi yasiyo matakatifu]” tofauti na majengo yaliyojengwa kwenye eneo lililotengwa hasa kwa ajili ya ibada takatifu.—Eze. 42:20.

7. Jiji ambalo Ezekieli aliona ni nini, na inaelekea linawakilisha nini? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

7 Basi, jiji ambalo Ezekieli aliona ni nini? Kumbuka kwamba aliona jiji hilo katika maono yaleyale aliyoona nchi. (Eze. 40:2; 45:1, 6) Neno la Mungu linaonyesha kwamba nchi hiyo ni nchi ya kiroho, basi jiji hilo linamaanisha jiji la kiroho. Kwa ujumla, neno “jiji” linamaanisha nini? Neno hilo linatoa wazo la watu wanaoishi pamoja katika kikundi na kufanyiza mfumo wenye utaratibu na mpangilio. Basi, inaonekana jiji lenye mpangilio mzuri ambalo Ezekieli aliona—lililokuwa mraba kamili—linawakilisha kituo cha usimamizi chenye mpangilio mzuri.

8. Kituo hicho cha usimamizi kinaongoza milki, au eneo gani, na kwa nini?

8 Kituo hicho cha usimamizi kinaongoza milki, au eneo gani? Maono ya Ezekieli yanafunua kwamba jiji hilo linafanya kazi katika nchi ya kiroho. Basi, leo kituo hicho cha usimamizi kinaongoza katika utendaji wa watu wa Mungu. Wazo la kwamba jiji hilo liko katika eneo la matumizi ya kawaida, au lisilo takatifu linamaanisha nini? Hilo linatukumbusha kwamba jiji hilo si usimamizi wa kimbingu, bali ulio duniani, ambao umekuwa ukitenda kwa faida ya watu wote walio katika paradiso ya kiroho.

9. (a) Leo, ni nani wanaofanyiza usimamizi huo duniani? (b) Yesu atafanya nini wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja?

9 Ni nani wanaofanyiza usimamizi huo ulio duniani? Katika maono ya Ezekieli, serikali ya jiji iliongozwa na “kiongozi.” (Eze. 45:7) Alikuwa mwangalizi kati ya watu, lakini hakuwa kuhani wala Mlawi. Kiongozi huyo anatukumbusha wazee wa kutaniko leo ambao si watiwa mafuta. Wachungaji hao wa kiroho wenye kujali kutoka kati ya “kondoo wengine” ni watumishi wanyenyekevu walio duniani wa serikali ya Kristo iliyo mbinguni. (Yoh. 10:16) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja unaokuja, Yesu atawachagua na kuwaweka rasmi “katika dunia yote” wazee wanaostahili, au “wakuu.” (Zb. 45:16) Chini ya mwongozo wa Ufalme wa mbinguni, watawatunza watu wa Mungu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja.

“Yehova Yupo Hapo”

10. Jina la jiji hilo ni nini, na hilo linatoa uhakikisho gani?

10 Soma Ezekieli 48:35. Jina la jiji hilo ni “Yehova Yupo Hapo.” Jina hilo linatoa uhakikisho kwamba kuwapo kwa Yehova kunaonekana katika jiji hilo. Yehova alipomwonyesha Ezekieli jiji hilo lililo katikati, ni kana kwamba aliwaambia wahamishwa hivi: ‘Nitakuwa pamoja nanyi tena!’ Kwa kweli uhakikisho huo uliwatia moyo!

11. Tunapata masomo gani kutokana na maono ya Ezekieli kuhusu jiji na jina lake lenye maana kubwa?

11 Tunapata masomo gani kutokana na sehemu hii ya unabii wa Ezekieli? Tukiwa watumishi wa Mungu, jina la jiji hilo la usimamizi linatuhakikishia kwamba Yehova ataendelea kukaa pamoja na watumishi wake waaminifu duniani sasa na milele. Jina hilo lenye maana linakazia ukweli huu muhimu: Kusudi la jiji hilo si kumpa mwanadamu yeyote mamlaka, bali kutekeleza njia za Yehova zenye upendo na usawaziko. Kwa mfano, Yehova hajawapa wasimamizi mamlaka ya kuigawa nchi, wakiongozwa na maoni ya kibinadamu. Badala yake, Yehova anatazamia wasimamizi hao waheshimu urithi, au mapendeleo ambayo yeye mwenyewe amewapa watumishi wake, kutia ndani watu “wa hali ya chini.”—Met. 19:17; Eze. 46:18; 48:29.

12. (a) Ni jambo gani muhimu lililo katika jiji hilo, nalo linamaanisha nini? (b) Waangalizi Wakristo wanapata kikumbusho gani muhimu kutokana na jambo hilo?

12 Ni jambo gani lingine la pekee lililo katika jiji linaloitwa “Yehova Yupo Hapo”? Ingawa majiji ya kale yalikuwa na kuta kwa ajili ya ulinzi na malango machache iwezekanavyo, jiji hili lina malango 12! (Eze. 48:30-34) Idadi hiyo kubwa ya malango (matatu kila upande wa jiji hilo la mraba) inaonyesha kwamba watumishi wote wa Mungu wanaweza kuwafikia wasimamizi wa jiji hilo wakati wowote. Isitoshe, malango 12 ya jiji yanakazia kwamba jiji hilo liko wazi kwa kila mtu, “watu wote wa nyumba ya Israeli.” (Eze. 45:6) Jiji hilo lililo wazi ni kikumbusho muhimu kwa waangalizi Wakristo. Yehova anataka wawe wenye urafiki na wanaoweza kufikiwa wakati wowote na watu wote wanaoishi katika paradiso ya kiroho.

Waangalizi Wakristo ni wenye urafiki na wanapatikana wakati wowote (Tazama fungu la 12)

Watu wa Mungu ‘Wanaingia Ili Kuabudu’ na ‘Kulitumikia Jiji’

13. Yehova alisema nini kuhusu kazi mbalimbali ambazo watu wangefanya?

13 Acheni turudi wakati wa Ezekieli ili tujue mambo zaidi anayoandika katika maono hayo marefu ya kuigawa nchi. Yehova anasema kwamba watu wanashiriki kufanya kazi mbalimbali. Makuhani—“wahudumu wa mahali patakatifu”—wangetoa dhabihu na kumkaribia Yehova ili kumhudumia. Nao Walawi—“wahudumu wa hekaluni”—wangeshughulikia “utumishi wa hekaluni na mambo yote yanayopaswa kufanywa humo.” (Eze. 44:14-16; 45:4, 5) Isitoshe, wafanyakazi wangekuwa na shughuli nyingi karibu na jiji. Wafanyakazi hao ni nani?

14. Wafanyakazi walio karibu na jiji wanatukumbusha nini?

14 Wafanyakazi walio karibu na jiji wanatoka “katika makabila yote ya Israeli.” Wanaunga mkono kazi. Jukumu lao ni kukuza mazao ambayo “yatakuwa chakula cha wale wanaolitumikia jiji.” (Eze. 48:18, 19) Je, mpango huo unatukumbusha nafasi muhimu tuliyo nayo leo? Ndiyo. Leo, wakaaji wote katika paradiso ya kiroho wana nafasi ya kuunga mkono utumishi wa ndugu za Kristo watiwa mafuta na utumishi wa wale walio kati ya “umati mkubwa” ambao Yehova amewaweka rasmi waongoze. (Ufu. 7:9, 10) Njia kuu tunayounga mkono kazi hiyo ni kwa kutii kwa hiari mwongozo wa mtumwa mwaminifu.

15, 16. (a) Tunapata habari gani nyingine katika maono ya Ezekieli? (b) Tuna nafasi gani ya kufanya kazi kama hiyo?

15 Maono ya Ezekieli yana jambo lingine linalotufundisha somo kuhusu huduma yetu. Ni jambo gani? Yehova anasema kwamba watu wa makabila 12 yasiyo ya Walawi wangefanya kazi mbalimbali katika maeneo mawili: katika ua wa hekalu na kwenye viwanja vya malisho vya jiji. Wanafanya kazi gani katika maeneo hayo? Katika ua wa hekalu, makabila yote ‘yanaingia ili kuabudu’ kwa kumtolea Yehova dhabihu. (Eze. 46:9, 24) Kwenye eneo la jiji, watu kutoka makabila yote wanakuja kuunga mkono kwa kulima eneo hilo. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa wafanyakazi hao?

16 Leo, washiriki wa umati mkubwa wana nafasi ya kufanya kazi kama zile zilizofanywa katika maono ya Ezekieli. Wanamwabudu Yehova “katika hekalu lake” kwa kumtolea dhabihu za sifa. (Ufu. 7:9-15) Wanafanya hivyo kwa kuhubiri na pia kutoa maelezo na kuimba katika mikutano ya Kikristo. Wanaona kumwabudu Yehova kuwa jukumu lao muhimu zaidi. (1 Nya. 16:29) Isitoshe, wengi kati ya watu wa Mungu wanaunga mkono tengenezo la Mungu kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wanasaidia kujenga na kudumisha Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi, na kusaidia katika miradi mingine mingi inayofanywa na tengenezo la Yehova. Wengine wanaunga mkono miradi hiyo kwa kutoa michango ya kifedha. Kwa njia ya mfano, wanalima “kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Wanafanya kazi yao kwa bidii na shangwe kwa sababu wanajua kwamba Yehova “hupendezwa na dhabihu kama hizo.” (Ebr. 13:16) Je, unatumia nafasi hizo kikamili?

Tunajifunza masomo gani kutokana na maelezo ya Ezekieli kuhusu kazi mbalimbali zilizofanywa katika malango ya jiji? (Tazama fungu la 14-16)

“Tunangojea Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

17. (a) Tutaona utimizo gani mkubwa wa maono ya Ezekieli wakati ujao? (b) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, ni nani watakaofaidika na jiji la usimamizi?

17 Je, wakati ujao tutaona utimizo mkubwa zaidi wa maono ya Ezekieli kuhusu mchango? Ndiyo! Fikiria jambo hili: Ezekieli aliona kwamba eneo lililoitwa “mchango mtakatifu” lilikuwa katikati ya nchi. (Eze. 48:10) Vivyo hivyo, baada ya Har–Magedoni, hata iwe tutaishi wapi duniani, Yehova atakaa pamoja nasi. (Ufu. 21:3) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, jiji la usimamizi—yaani, wale walio duniani ambao watachaguliwa ili kushughulikia masilahi ya watu wa Mungu—wataongoza mambo ulimwenguni pote kwa kutoa mwongozo wenye upendo kwa wote watakaofanyiza “dunia mpya,” yaani, jamii mpya ya wanadamu.—2 Pet. 3:13.

18. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba jiji la usimamizi litakuwa na upatano na utawala wa Mungu? (b) Tunapata uhakikisho gani thabiti kutokana na jina la jiji hilo?

18 Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba jiji la usimamizi litaendelea kutenda kwa upatano na utawala wa Mungu? Kwa sababu Neno la Mungu linaonyesha kwamba jiji la kidunia lenye malango 12 linapatana na jiji la mbinguni lenye malango 12, Yerusalemu Jipya, linalofanyizwa na watawala wenzi wa Kristo 144,000. (Ufu. 21:2, 12, 21-27) Jambo hilo linaonyesha kwamba usimamizi huo ulio duniani utafuata maamuzi yote yanayofanywa na Ufalme wa Mungu na kuyatekeleza kwa makini. Jina la jiji “Yehova Yupo Hapo” linatuhakikishia sote kwamba ibada safi itadumu na kusitawi milele katika Paradiso. Kwa kweli tunatazamia wakati ujao utakaokuwa mzuri sana!