Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 1A

Ibada Ni Nini?

Ibada Ni Nini?

Ibada inaweza kufafanuliwa kuwa “tendo la kumwonyesha mungu fulani heshima na upendo.” Katika Biblia, maneno ya awali yanayotafsiriwa kuwa “ibada” yanaweza kuwa na wazo la mtu anayeonyesha heshima kubwa, au kujitiisha kwa viumbe. (Mt. 28:9) Maneno hayo yanaweza pia kumaanisha tendo la ibada kuelekea Mungu au miungu. (Yoh. 4:23, 24) Muktadha unasaidia kuelewa maana ya maneno hayo.

Yehova peke yake, Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, ndiye tu tunayepaswa kumwabudu. (Ufu. 4:10, 11) Tunamwabudu Yehova kwa kuheshimu enzi yake kuu na kwa kuliheshimu jina lake. (Zab. 86:9; Mt. 6:9, 10) Mambo hayo mawili—enzi kuu ya Yehova na jina lake—yanatajwa sana katika kitabu cha Ezekieli. Maneno “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova” yanatumiwa mara 217 katika Ezekieli peke yake, na maneno “kujua kwamba mimi ni Yehova,” mara 55.—Eze. 2:4; 6:7.

Hata hivyo, ibada yetu haihusishi hisia tu; badala yake, ibada ya kweli inahusisha matendo. (Yak. 2:26) Tunapojiweka wakfu kwa Yehova, tunatoa kiapo kwamba katika kila jambo maishani mwetu, tutamtii akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu na kuliheshimu sana jina lake. Kumbuka kwamba alipokuwa akijibu jaribu la tatu, Yesu alihusianisha ibada na “utumishi mtakatifu.” (Mt. 4:10) Tukiwa waabudu wa Yehova, tunatamani kumtumikia. * (Kum. 10:12) Tunamtolea Mungu wetu utumishi mtakatifu tunapofanya matendo yanayohusiana moja kwa moja na ibada yetu na yanayohitaji kujidhabihu. Ni matendo gani hayo?

Utumishi mtakatifu unahusisha mambo mengi, na mambo hayo yote ni yenye thamani kwa Yehova. Tunatoa utumishi mtakatifu tunapowahubiria wengine, tunaposhiriki mikutano katika Jumba letu la Ufalme, na tunapotunza na kujenga majengo yetu ya ibada. Isitoshe, tunatoa utumishi mtakatifu tunaposhiriki katika ibada ya familia, tunapounga mkono kazi ya kutoa msaada kwa waabudu wenzetu walio na uhitaji, tunapojitolea kwenye makusanyiko, au kwa kutumikia Betheli. (Ebr. 13:16; Yak. 1:27) Ibada safi inapokuwa jambo muhimu zaidi katika akili na mioyo yetu, tunatoa “utumishi mtakatifu mchana na usiku.” Tunafurahia kumwabudu Mungu wetu, Yehova!—Ufu. 7:15.

^ fu. 5 Neno la Kiebrania linalotoa wazo la ibada pia linamaanisha “kutumikia.” Basi ibada inahusisha utumishi.—Kut. 3:12, maelezo ya chini.