Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 1B

Muhtasari wa Ezekieli

Muhtasari wa Ezekieli

Kwa ujumla, kitabu cha Ezekieli kinaweza kupangwa katika sehemu zifuatazo:

SURA YA 1 HADI 3

Mwaka wa 613 K.W.K., akiwa anaishi kati ya Wayahudi waliopelekwa uhamishoni Babiloni, Ezekieli anaona maono ya Yehova na anaagizwa awatolee unabii Wayahudi wanaoishi kando ya mto Kebari.

SURA YA 4 HADI 24

Kati ya mwaka wa 613 na 609 K.W.K., Ezekieli anatangaza ujumbe wa kinabii ulio na hukumu hasa dhidi ya Yerusalemu na watu wake walioasi na wanaoabudu sanamu.

SURA YA 25 HADI 32

Kuanzia mwaka wa 609 K.W.K., mwaka ambao Yerusalemu lilianza kuzingirwa mara ya mwisho, ujumbe wa Ezekieli wa hukumu hauelekezwi kwa Yerusalemu bali kwa mataifa jirani yaliyokuwa maadui—Amoni, Edomu, Misri, Moabu, Ufilisti, Sidoni, na Tiro.

SURA YA 33 HADI 48

Kuanzia mwaka wa 606 K.W.K., Yerusalemu likiwa magofu mamia ya kilomita huko mbali, sasa Ezekieli anatangaza ujumbe wa tumaini—ujumbe wa kusisimua kuhusu kurudishwa kwa ibada safi ya Yehova Mungu.

Basi, kimsingi kitabu cha Ezekieli kimepangwa kulingana na mfuatano wa matukio na kulingana na mambo makuu. Unabii kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake unatangulia unabii mwingi kuhusu kurudishwa kwa ibada safi. Hilo linapatana na akili, kwa maana unabii wa kurudishwa unaonyesha kwamba ibada ilikuwa imekomeshwa hekaluni.

Kwa kuongezea, unabii wa Ezekieli dhidi ya mataifa jirani yaliyokuwa maadui (sura ya 25 hadi 32) uko kati ya ujumbe wake wa hukumu dhidi ya Yerusalemu na unabii kuhusu kurudishwa kwa ibada safi. Akizungumza kuhusu ujumbe wa Ezekieli wa hukumu kwa mataifa, msomi mmoja alisema hivi: “Unatokeza badiliko zuri kutoka kutangazwa kwa ghadhabu ya Mungu na kisha kuwa ujumbe wa kuwaonyesha watu wake rehema, kwa sababu kuadhibiwa kwa maadui wao ni sehemu ya kukombolewa kwa watu wake.”

Angalia sura ya 1, fungu la 18