Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusanyiko la pekee mwaka wa 1919 lilithibitisha waziwazi kwamba mwishowe watu wa Mungu walikuwa wamewekwa huru kutoka kwa Babiloni Mkubwa

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 9B

Kwa Nini 1919?

Kwa Nini 1919?

Kwa nini tunasema kwamba watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka kwenye utekwa wa Babiloni Mkubwa mwaka wa 1919? Unabii mbalimbali wa Biblia pamoja na mambo yaliyotokea katika historia yanatusaidia kufikia uamuzi huo.

Unabii wa Biblia na historia inathibitisha kwamba Yesu alianza kutawala akiwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914, na hivyo siku za mwisho za mfumo wa Shetani zikaanza hapa duniani. Yesu alifanya nini baada ya kuwa Mfalme? Je, mara moja aliwaweka huru watumishi wake walio duniani kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa? Je, alimweka rasmi “mtumwa [wake] mwaminifu na mwenye busara” mwaka wa 1914 na kuanza kazi kubwa ya mavuno?—Mt. 24:45.

Inaonekana hakufanya hivyo. Kumbuka mtume Petro aliongozwa na roho kuandika kwamba hukumu ingeanza na “nyumba ya Mungu.” (1 Pet. 4:17) Vivyo hivyo, nabii Malaki alitabiri wakati ambapo Yehova angekuja katika nyumba Yake ya ibada akiwa pamoja na “mjumbe wa agano,” yaani, Mwana wa Mungu. (Mal. 3:1-5) Hicho kingekuwa kipindi cha kusafishwa na kujaribiwa. Je, historia inapatana na mambo hayo yaliyotajwa katika unabii?

Ndiyo! Mwaka wa 1914 hadi mwanzoni mwa 1919 kilikuwa kipindi kigumu cha kujaribiwa na kusafishwa kwa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Mwaka wa 1914 watumishi wengi wa Mungu duniani walivunjika moyo mwisho wa mfumo wa mambo ulipokosa kufika kama walivyotarajia. Walihuzunika hata zaidi mwaka wa 1916, Charles T. Russell, aliyekuwa akiwaongoza watu wa Mungu kwa bidii alipokufa. Baadhi ya watu waliokuwa karibu sana na Ndugu Russell walipinga vikali jitihada za Joseph F. Rutherford, aliyechukua mahali pa Russell katika kuongoza. Mwaka wa 1917 kulitokea migawanyiko ambayo ilikuwa karibu kuvunja tengenezo. Kisha mwaka wa 1918, inaonekana kupitia uchochezi wa makasisi, Ndugu Rutherford na washiriki wake saba walishtakiwa, wakahukumiwa kimakosa, na kufungwa gerezani. Makao makuu huko Brooklyn yakafungwa. Kwa kweli, bado watu wa Mungu hawakuwa wamewekwa huru kutoka kwa Babiloni Mkubwa!

Hata hivyo, ni nini kilichotokea mwaka wa 1919? Mambo yalibadilika haraka sana! Mwanzoni mwa mwaka huo, Rutherford na washirika wake waliachiliwa kutoka gerezani. Nao wakarudi kazini bila kukawia! Mara moja, wakapanga kusanyiko la pekee, na gazeti jipya, The Golden Age, (sasa ni Amkeni!) likaanza kuchapishwa. Gazeti hilo lilikusudiwa kutumiwa katika kampeni za kuhubiri hadharani. Isitoshe, katika kila kutaniko mwangalizi alichaguliwa ili apange na kuendeleza huduma. Mwaka huohuo, jarida la Bulletin (sasa ni Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo) lilichapishwa ili kusaidia kupanga kazi ya kuhubiri.

Ni nini kilichotokea? Ni wazi kwamba Kristo alikuwa amewaweka huru watu wake kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa. Alikuwa amemweka rasmi mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara. Kazi ya mavuno ilikuwa ikiendelea. Tangu mwaka huo muhimu wa 1919, kazi hiyo imekuwa ikisonga mbele kwa kasi sana.