Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 15A

Dada Waliokuwa Makahaba

Dada Waliokuwa Makahaba

Katika Ezekieli sura ya 23, watu wa Mungu wanashutumiwa vikali kwa sababu ya kukosa uaminifu. Sura hii inafanana kwa njia nyingi na sura ya 16. Kama sura ya 16, sura ya 23 inatumia mfano wa ukahaba. Yerusalemu ndiye dada mdogo, na Samaria ndiye dada yake mkubwa. Sura hizo mbili zinaonyesha jinsi dada mdogo alivyomwiga dada yake mkubwa akawa kahaba na akamzidi katika uovu na uasherati. Katika sura ya 23, Yehova anawapa majina dada hao wawili: Ohola ndiye dada mkubwa, yaani, Samaria, jiji kuu la ufalme wenye makabila kumi wa Israeli; Oholiba ndiye dada mdogo, yaani, Yerusalemu, jiji kuu la Yuda. *Eze. 23:1-4.

Sura hizo mbili zinalingana kwa njia nyingine pia. Huenda ulinganifu mkubwa ni huu: Mwanzoni makahaba hao walikuwa wake za Yehova kisha wakamsaliti. Pia, kuna ahadi inayotoa tumaini. Sura ya 23 haitoi tumaini lililo wazi kuhusu kukombolewa, lakini inalingana na sura ya 16 kwa kuwa Yehova anasema: “Nitaukomesha mwenendo wako mchafu na ukahaba wako.”—Eze. 16:16, 20, 21, 37, 38, 41, 42; 23:4, 11, 22, 23, 27, 37.

Je, Wanafananisha Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo?

Zamani, machapisho yetu yalisema kwamba dada hao wawili, Ohola na Oholiba, wanawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo hasa kanisa Katoliki na Waprotestanti. Hata hivyo, kuna maswali ambayo yametokea baada ya kusali na kuchunguza zaidi jambo hilo. Je, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimewahi kuwa mke wa Yehova? Je, ziliwahi kufanya agano naye? Hapana. Yesu alipopatanisha “agano jipya” pamoja na Israeli wa kiroho, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazikuwapo; wala hazikuwahi kamwe kuwa sehemu ya taifa hilo la kiroho la Wakristo watiwa mafuta. (Yer. 31:31; Luka 22:20) Dini zinazodai kuwa za Kikristo zilianzishwa baada ya kifo cha mitume. Zilianza katika karne ya nne W.K. kama shirika lililopotoka la waasi imani lililofanyizwa na Wakristo wa uwongo, “magugu” ambayo Yesu alitabiri katika mfano wa ngano na magugu.—Mt. 13:24-30.

Tofauti nyingine kubwa: Yehova alitoa tumaini la kuwakomboa Yerusalemu na Samaria waliokosa kuwa waaminifu. (Eze. 16:41, 42, 53-55) Je, Biblia inatoa tumaini kama hilo kwa dini zinazodai kuwa za Kikristo? Hapana! Dini hizo ni sehemu ya Babiloni Mkubwa na hazina tumaini lolote.

Basi Ohola na Oholiba sio mifano ya kinabii ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hata hivyo, dini hizo zinatusaidia kuelewa jambo muhimu hata zaidi: jinsi Yehova anavyohisi kuhusu wale wanaoliletea suto jina lake takatifu na kulegeza viwango vya ibada safi. Dini zinazodai kuwa za Kikristo zina hatia kubwa zaidi kuhusiana na hilo kwa sababu makanisa yake mengi yanadai kumwakilisha Mungu na Biblia. Isitoshe, wanadai kwamba kiongozi wao ni Yesu Kristo, Mwana mpendwa wa Yehova. Lakini wanapinga dai hilo kwa kusema kwamba Yesu ni sehemu ya utatu na kwa kutotii amri yake iliyo wazi ya kutokuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 15:19) Kwa kuendelea kujihusisha na ibada ya sanamu na mambo ya kisiasa, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimethibitika kabisa kuwa sehemu ya yule “kahaba mkubwa.” (Ufu. 17:1) Kwa hakika, lazima ataadhibiwa wakati wa kuangamizwa kwa milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo!

^ fu. 3 Majina hayo yana maana. Ohola linamaanisha “Hema Lake [la Ibada]”—inaonekana linamaanisha hatua ya Israeli ya kuanzisha sehemu nyingine za ibada badala ya kumwabudu Yehova katika hekalu huko Yerusalemu. Kwa upande mwingine, Oholiba linamaanisha “Hema Langu [la Ibada] Liko Ndani Yake.” Yerusalemu lilikuwa kituo cha nyumba ya ibada ya Yehova.